Sanduku La Swali
◼ Wimbo wa kufungua Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, Mkutano wa Utumishi, Mkutano wa Watu Wote. na Funzo la Mnara wa Mlinzi unapaswa kutangazwa lini, na ni nani anayepaswa kufanya hivyo?
Nyimbo za kufungua mkutano wa Shule ya Huduma ya Kitheokrasi huorodheshwa katika Ratiba ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi inayopatikana katika nyongeza ya Huduma Yetu ya Ufalme ya Oktoba. Nyimbo za kufungua na kumalizia Mkutano wa Utumishi wa kila juma huonyeshwa kwenye ukurasa wa 2 wa Huduma Yetu ya Ufalme. Pia, namba za nyimbo za Funzo la Mnara wa Mlinzi la kila juma zinapatikana kwenye ukurasa wa 2 wa kila gazeti la Mnara wa Mlinzi. Kwa kuwa nyimbo zilizoteuliwa ni sehemu ya mkutano fulani hususa, zinapaswa kutangazwa na ndugu anayeongoza mkutano huo bali si na mwenyekiti wa mkutano uliotangulia.
Kwa mfano, mwangalizi wa Shule ya Huduma ya Kitheokrasi atakaribisha wasikilizaji, atatangaza wimbo wa kufungua, ataongoza shule, kisha atamkaribisha jukwaani msemaji wa kwanza wa Mkutano wa Utumishi. Ndugu aliye na sehemu hiyo ya Mkutano wa Utumishi ndiye anayepaswa kutangaza wimbo unaofungua Mkutano wa Utumishi.
Vivyo hivyo, Mkutano wa Watu Wote utaanzishwa na mwenyekiti. Atawakaribisha kwa uchangamfu wote waliohudhuria na kuwaalika washiriki kuimba wimbo wa kufungua ambao umeteuliwa na msemaji. Mwenyekiti (au labda ndugu mwingine anayestahili aliyepewa mgawo mapema) atafungua mkutano huo kwa sala. Kisha mwenyekiti atamtaja msemaji na kichwa cha hotuba yake. Baada ya hotuba, mwenyekiti atatoa shukrani kwa ufupi kwa ajili ya mafundisho hayo bila kurudia kwa muhtasari mambo ambayo msemaji amekwisha kuyasema. Mwenyekiti atatangaza kichwa cha hotuba ya watu wote itakayotolewa juma linalofuata, kisha atawaomba wote waliohudhuria wabaki kwa ajili ya Funzo la Mnara wa Mlinzi. Hakuna haja ya mwenyekiti kuomba wasikilizaji watume salamu kwenye kutaniko la msemaji anayezuru. Kisha, mwenyekiti atamkaribisha jukwaani kiongozi wa Funzo la Mnara wa Mlinzi.
Kiongozi wa Funzo la Mnara wa Mlinzi atatangaza wimbo wa kwanza wa funzo hilo. Ataongoza funzo hilo kupatana na maagizo yaliyochapishwa kisha atatangaza wimbo wa kumalizia. Kwa kawaida, kiongozi wa Funzo la Mnara wa Mlinzi atamkaribisha ndugu aliyetoa hotuba ya watu wote atoe sala ya kumalizia.
Miongozo hii ikifuatwa, mikutano yetu ya kutaniko itaendeshwa kwa umoja.