Jifunze Biblia na Watu Wanaochukua Magazeti
1. Tutakuwa na lengo gani mwezi Aprili na Mei?
1 Mwezi wa Aprili na Mei, tutakuwa tukitoa magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! tukiwa na lengo la kuanzisha mafunzo ya Biblia tukitumia kitabu Biblia Inafundisha tunapowarudia wale tuliowaachia magazeti. Hapa chini kuna mapendekezo yanayoweza kutusaidia. Kumbuka kwamba unapaswa kubadili mapendekezo hayo yafae eneo lenu. Jihisi huru kutumia njia nyingine inayofaa eneo lenu.
2. Tunawezaje kutumia kurasa za utangulizi za kitabu Biblia Inafundisha kuanzisha funzo la Biblia?
2 Tumia Kurasa za Utangulizi: Unaweza kusema hivi unapofanya ziara ya kurudia: “Magazeti niliyokuachia yanakazia kusoma Biblia. Ona kwa nini kusoma Biblia ni muhimu sana.” Soma Isaya 48:17, 18; Yohana 17:3; au andiko lingine lolote linaloweza kufaa. Kisha baada ya kumwonyesha na kumpa kitabu Biblia Inafundisha, unaweza kuendelea kusema hivi:
◼ “Biblia inatupa tumaini hakika la wakati ujao.” Mwonyeshe mwenye nyumba ukurasa wa 4 na 5 na umuulize, “Ungependa kuona ahadi gani kati ya hizi ikitimizwa?” Mwonyeshe mwenye nyumba sura ambayo inazungumzia ahadi ya Kimaandiko aliyoichagua, na ikiwa anaruhusu, chunguza naye fungu moja au mawili kwa ufupi.
◼ Au unaweza kusema hivi, “Biblia ina majibu ya maswali muhimu sana katika maisha.” Mwonyeshe mwenye nyumba ukurasa wa 6, na umuulize kama amewahi kujiuliza swali lolote kati ya yale yanayoonyeshwa chini kwenye ukurasa huo. Fungua sura inayojibu swali hilo, na kwa ufupi unaweza kuchunguza naye fungu moja au mawili.
◼ Au unaweza kumwonyesha baadhi ya vichwa kwenye jedwali ya yaliyomo na umuulize anapendezwa na somo gani. Fungua sura hiyo, na kwa ufupi mwonyeshe jinsi funzo linavyofanywa.
3. Unaweza kuanzishaje funzo la Biblia baada ya kumwachia mwenye nyumba magazeti yanayozungumzia (a) hali za ulimwengu zinazozorota? (b) mambo ya familia? (c) kutegemeka kwa Biblia?
3 Acha Swali Unapomhubiria kwa Mara ya Kwanza: Jambo lingine unaloweza kufanya ni kuweka msingi kwa ajili ya ziara ya kurudia unapomhubiria mtu kwa mara ya kwanza. Mwenye nyumba anapochukua magazeti, muulize swali na uahidi kwamba utakuja kujibu utakaporudi. Jitahidi kupanga wakati hususa utakaorudi na uhakikishe umerudi. (Mt. 5:37) Unaporudi, mkumbushe mwenye nyumba swali ulilomuuliza, kisha usome na kuchunguza naye fungu moja au mawili kutoka kwenye kitabu Biblia Inafundisha ambalo litajibu swali hilo. Mpe kitabu ili aweze kufuatana nawe. Ona mifano michache ifuatayo.
◼ Kama gazeti unalomwachia mwenye nyumba linazungumzia hali za ulimwengu zinazozorota, unaweza kusema hivi, “Nitakaporudi tutazungumzia majibu ya Biblia kwa swali hili, Mungu ataleta mabadiliko gani duniani?” Unaweza kutumia ukurasa wa 4 na 5 unaporudi. Au unaweza kuuliza swali hili, “Je, mambo mabaya yanayotupata yanasababishwa na Mungu?” Unaporudi mwonyeshe mwenye nyumba fungu la 7 na 8 katika sura ya 1.
◼ Kama gazeti unalomwachia mwenye nyumba linashughulikia mambo ya familia, kabla hujaondoka unaweza kumuuliza swali hili, “Kila mmoja anaweza kufanya nini ili kuchangia furaha katika familia?” Unaporudi mnaweza kuchunguza fungu la 4 katika sura ya 14.
◼ Kama gazeti unalomwachia mwenye nyumba linazungumzia kutegemeka kwa Biblia, unaweza kumuuliza swali hili mtakalozungumzia utakaporudi, “Je, Biblia ni sahihi kisayansi?” Unaporudi, mnaweza kuchunguza fungu la 8 katika sura ya 2.
4. Tunapaswa kufanya nini ikiwa mwenye nyumba anakataa kuchukua kitabu Biblia Inafundisha?
4 Mwishoni mwa kila ziara, muulize swali utakalojibu kwenye ziara itakayofuata. Baada ya funzo kuwa la kawaida, jifunzeni kitabu hicho kwa utaratibu mzuri kuanzia mwanzo. Vipi ikiwa mwenye nyumba anakataa kuchukua kitabu Biblia Inafundisha? Unaweza kuendelea kumpelekea magazeti na kuwa na mazungumzo ya Kimaandiko pamoja naye. Unapoendelea kustawisha upendezi wake, baada ya muda fulani huenda atakubali kujifunza Biblia.
5. Kwa nini tunapaswa kujitahidi kufanya mengi zaidi ya kuwaachia tu watu magazeti?
5 Yesu alituagiza ‘tufanye wanafunzi na kuwafundisha.’ (Mt. 28:19, 20) Hivyo, lengo letu tunapowaachia watu magazeti ni kuwafundisha kweli wenye mioyo minyoofu. Mwezi wa Aprili na Mei, fanya jitihada za pekee ili kuanzisha funzo la Biblia baada ya kumwachia mtu magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni!