Funzo la Kibinafsi na Funzo la Biblia la Familia Ni Muhimu!
1. Baraza Linaloongoza lina hangaiko gani la pekee kwa ajili yetu wakati huu, na kwa nini?
1 Kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza, Baraza Linaloongoza linahangaikia sana hali ya watu wa Yehova. (Mdo. 15:6, 28) Kadiri hali hatari ya dhiki kuu inavyokaribia, ni muhimu kila mhubiri wa Ufalme awe na uhusiano ulio imara pamoja na Yehova. Utatumiaje wakati ambao hapo awali ulitumiwa kwa ajili ya Funzo la Kitabu la Kutaniko? Wote wanatiwa moyo watumie wakati huo kwa ajili ya ibada ya familia. Kutumia kwa hekima wakati huo kutaturuhusu kuchimba ndani zaidi ya Neno la Mungu lililoongozwa na roho na kufaidika na maji yake ya uzima.—Zab. 1:1-3; Rom. 11:33, 34.
2. Tunaweza kufanya mipango gani kwa ajili ya jioni ya ibada ya familia?
2 Jioni ya Ibada ya Familia: Vichwa vya familia wanatiwa moyo wachukue kwa uzito daraka lao mbele za Yehova kwa kuhakikisha kwamba wanafuata programu ya kawaida ya funzo la Biblia la familia. (Kum. 6:6, 7) Ndugu na dada waseja ambao hawana madaraka ya familia wataweza kutumia wakati huo kujifunza Biblia kibinafsi na kufanya utafiti. Ni muhimu sote ‘tununue wakati unaofaa’ wa kujifunza na kutafakari ili tuwe na nguvu za kiroho tunapokabili ‘siku zenye uovu.’—Efe. 5:15, 16.
3, 4. Ni mapendekezo gani yametolewa kuhusu vifaa tunavyoweza kutumia, na tunapaswa kufanya hivyo tukiwa na kusudi gani akilini?
3 Mambo ya Kujifunza: Fahirisi au Watchtower Library katika CD-ROM inaweza kuwasaidia mnapochagua habari ambayo itafanya vipindi vyenu vya kujifunza Biblia vifurahishe. Familia zinaweza kujifunza makala za kawaida za Mnara wa Mlinzi, kama vile “Siri ya Furaha ya Familia,” “Wafundishe Watoto Wako,” na “Kwa Ajili ya Vijana Wetu.” Pia, gazeti la Amkeni! lina mfululizo wenye kichwa “Vijana Huuliza” na makala zenye kuvutia sana kuhusu maajabu ya uumbaji.
4 Kusoma Biblia bila haraka kunaweza kukazia masomo na kanuni za kimungu katika akili na mioyo ya washiriki wote wa familia. (Ebr. 4:12) Nyakati nyingine, mnaweza kutazama na kuzungumzia moja ya vidio za tengenezo. Mnaweza kutumia njia mbalimbali ili kufanya funzo liwe lenye ubunifu na lenye kupendeza. Kwa nini msiwaulize washiriki wa familia zenu mambo ambayo wangependa kujifunza na jinsi wanavyotaka kujifunza?
5. Kwa nini funzo la Biblia la kibinafsi na la familia ni muhimu sana katika maisha yetu sasa?
5 kwa Nini Ni Muhimu Kujifunza Sasa? Tukiimarisha hali yetu ya kiroho tutakuwa tayari ‘kusimama imara na kuuona wokovu wa Yehova.’ (Kut. 14:13) Wazazi wanahitaji mwongozo wa Mungu ili wawalee watoto “katikati ya kizazi kilicho kombo na kilichopotoka.” (Flp. 2:15) Leo, watoto wanahitaji kusaidiwa kukabiliana na mazingira ya shule yanayozidi kuzorota kiadili. (Met. 22:3, 6) Wenzi wa ndoa wanapaswa kuimarisha ‘kamba yao yenye nyuzi tatu’ pamoja na Yehova. (Mhu. 4:12) Basi acheni tutumie wakati unaobaki kwa hekima kujijenga wenyewe juu ya ‘imani yetu iliyo takatifu’!—Yuda 20.