‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’
1. Funzo la Biblia la Kutaniko katika miezi ijayo litatupa fursa gani?
1 Vitabu vinne vya Injili kuhusu maisha ya Yesu alipokuwa duniani, vina habari nyingi sana kumhusu Mwana wa Mungu. Kwa kuwa Wakristo wanapaswa ‘kufuata hatua zake kwa ukaribu,’ tutahitaji kujitayarisha vizuri na kusikiliza kwa makini tutakapojifunza kitabu ‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’ kwenye Funzo la Biblia la Kutaniko kuanzia juma la Machi 1. (1 Pet. 2:21; Marko 10:21) Tunapaswa kuzingatia sana matukio katika maisha ya Yesu yanayoweza kututia moyo katika huduma.
2. Mfano wa Yesu wa kuvumilia unaweza kutunufaishaje?
2 Mfano Ambao Yesu Aliweka: Je, umewahi kukutana na watu wanaokataa ujumbe wetu unapohubiri nyumba kwa nyumba? Wanapokataa ujumbe wetu, tunatambua umuhimu wa maneno ya Yesu: “Ikiwa wamenitesa mimi, watawatesa ninyi pia.” (Yoh. 15:20) Ni kweli kwamba si sikuzote tunaweza kusema tunateswa watu wanapokataa ujumbe wetu. Hata hivyo, Yesu aliweza kuvumilia aina zote za mateso na majaribu kwa ajili ya shangwe iliyowekwa mbele yake. Sisi pia tunaweza kujitahidi ili kukubaliwa na Yehova na kupata thawabu kwa ajili ya uaminifu wetu. Hilo litatusaidia ‘tusichoke na kuzimia katika nafsi zetu.’ (Ebr. 12:2, 3; Met. 27:11) Tunapoendelea na huduma licha ya upinzani, tunaweza kuwa na hakika kwamba Kristo Yesu atatutegemeza.—Mt. 28:20.
3. Tunawezaje kuwa na maoni ya Yesu kuhusu huduma?
3 “Nilitumwa Kufanya Hivyo”: Kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme ndiyo iliyokuwa utendaji muhimu katika maisha ya Yesu. (Luka 4:43) Alijitoa kabisa katika huduma. Aliiona huduma kuwa kazi ya haraka, na nyakati zote alitafuta fursa za kuwaeleza wengine kuhusu Ufalme. Kwa kuwa sisi ni wafuasi wa Yesu, hatua zake zinatuelekeza wapi? Tunapoendelea na shughuli zetu za kila siku, je, kuna watu ambao tunaweza kuwahubiria habari njema? Upendo alio nao Kristo na utusukume tuzungumze na watu wengi iwezekanavyo kuhusu habari njema!—2 Kor. 5:14.
4. Tunawezaje kuboresha utumishi wetu?
4 “Mtu Mwingine Hajapata Kamwe Kusema Kama Huyu”: Njia ya Yesu ya kufundisha iliwashangaza wasikilizaji wake. (Yoh. 7:46; Mt. 7:28, 29) Alikuwa tofauti na walimu wengine kwa njia gani? Alipenda kweli alizofundisha, aliwapenda watu aliowafundisha, na alitumia kwa ustadi njia mbalimbali za kufundisha. Kwa kumwiga Mwalimu Mkuu tunaweza kuboresha utumishi wetu.—Luka 6:40.
5. Tunapaswa kuwa na lengo gani tunapojifunza kitabu ‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’?
5 Hayo ni baadhi ya mambo muhimu tunayoweza kujifunza kutokana na maisha ya Yesu. Tunaweza kujifunza mambo gani mengine muhimu? Tunapochunguza maisha ya Yesu wakati wa Funzo la Biblia la Kutaniko, na tujitahidi “kuujua upendo wa Kristo” kwa kuiga maneno na matendo yake.—Efe. 3:19.