Fundisha kwa Ushawishi
1. Kutumia Neno la Mungu vizuri katika utumishi kunahusisha nini?
1 Wahudumu stadi kama mtume Paulo wanajua kwamba ‘kulitumia sawasawa neno la kweli’ kunahusisha mengi zaidi ya kunukuu tu andiko fulani la Biblia. (2 Tim. 2:15) Tunapotumia Neno la Mungu, tunawezaje kufundisha kwa “ushawishi?”—Mdo. 28:23.
2. Tunawezaje kuwasaidia watu waiheshimu Biblia zaidi?
2 Soma Moja kwa Moja Katika Biblia: Kwanza, elekeza fikira za msikilizaji kwenye Biblia kwa njia ambayo itamchochea aheshimu hekima ya kimungu inayopatikana ndani ya Biblia. Uhakika wetu katika Neno la Mungu unaweza kumchochea msikilizaji alikazie fikira andiko linalosomwa. (Ebr. 4:12) Tunaweza kusema hivi: “Nimeona kwamba kuna manufaa ya kujua maoni ya Mungu kuhusu jambo hili. Ona kile ambacho Neno lake linasema.” Inapowezekana, ni vyema kuonyesha yale ambayo Neno la Mungu linasema kwa kusoma moja kwa moja katika Biblia.
3. Baada ya kusoma andiko, tunaweza kufanya nini ili kumsaidia msikilizaji aelewe maana yake?
3 Pili, fafanua andiko ambalo umesoma. Watu wengi huona vigumu kuelewa andiko linaposomwa kwa mara ya kwanza. Hivyo, mara nyingi tunahitaji kuwaonyesha jinsi ambavyo andiko hilo linahusiana na ujumbe ambao tunamweleza. (Luka 24:26, 27) Kazia maneno yanayotegemeza ujumbe wako. Unaweza kumuuliza swali ili ujue kama ameelewa jambo kuu katika andiko hilo.—Met. 20:5; Mdo. 8:30.
4. Tunapowafundisha watu kwa ushawishi tunahitaji kufanya jambo gani lingine?
4 Msaidie Msikilizaji Afikiri Kuhusu Andiko: Tatu, jitahidi kufikia akili na moyo wa msikilizaji. Msaidie mwenye nyumba aone jinsi andiko hilo linavyomhusu yeye binafsi. Kutoa sababu kwa kutumia Maandiko kunaweza kumsadikisha msikilizaji abadili maoni yake. (Mdo. 17:2-4; 19:8) Kwa mfano, baada ya kusoma Zaburi 83:18 unaweza kuzungumzia umuhimu wa kujua jina la mtu ambaye unataka kujenga urafiki naye. Kisha unaweza kumuuliza, “Je, unafikiri kwamba kulijua jina la Mungu kutafanya sala zako ziwe za maana zaidi?” Tunapomwonyesha mwenye nyumba jinsi anavyoweza kutumia andiko fulani maishani, tunamsaidia aone thamani ya andiko hilo. Kufundisha Neno la Mungu kwa njia hiyo huwavuta watu wenye mioyo minyoofu kwenye ibada ya Mungu wa kweli na aliye hai, Yehova.—Yer. 10:10.