‘Hii Habari Njema Itahubiriwa’!
1. Tunajuaje kwamba hakuna chochote kinachoweza kukomesha kazi ya kuhubiri?
1 Hakuna chochote kinachoweza kumzuia Yehova asitimize mapenzi yake. (Isa. 14:24) Ingawa ilionekana kuwa Mwamuzi Gideoni pamoja na wanaume wake 300 hawangeweza kushinda askari-jeshi Wamidiani wapatao 135,000, Yehova alimwambia hivi: “Hakika utawaokoa Israeli kutoka katika mkono wa Midiani. Je, si mimi ninayekutuma?” (Amu. 6:14) Ni kazi gani ambayo inategemezwa na Yehova leo? Yesu alisema: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa.” (Mt. 24:14) Hakuna mtu anayeweza kuikomesha kazi hii!
2. Kwa nini tunaweza kutarajia kwamba Yehova atamsaidia kila mmoja wetu katika huduma?
2 Yehova Anamsaidia Kila Mmoja Wetu: Ingawa tunajua Yehova atawafanikisha Mashahidi wake wakiwa kikundi, je, tunaweza kutarajia kwamba Yehova atatusaidia sisi binafsi? Alipokuwa na uhitaji, mtume Paulo alihisi kuwa Yehova alimsaidia kupitia Mwanaye, Yesu. (2 Tim. 4:17) Tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atabariki pia jitihada za kila mmoja wetu za kufanya mapenzi yake.—1 Yoh. 5:14.
3. Yehova anatusaidia katika hali zipi mbalimbali?
3 Je, mahangaiko ya kila siku hufanya ukose nguvu za kuhubiri? “Yeye anampa nguvu mtu aliyechoka.” (Isa. 40:29-31) Je, unakabili mateso au upinzani? “Mtupie Yehova mzigo wako, naye mwenyewe atakutegemeza.” (Zab. 55:22) Je, nyakati nyingine unashikwa na woga wa kuhubiri? “Nenda, nami nitakuwa pamoja na kinywa chako.” (Kut. 4:11, 12) Je, matatizo ya afya yanakuzuia usifanye mengi katika utumishi? Yehova anathamini jitihada zako za moyo wote na anaweza kuzitumia, hata usipoweza kufanya mengi.—1 Kor. 3:6, 9.
4. Kuwa na hakika kwamba Yehova anabariki huduma yetu kutatuchochea tufanye nini?
4 Mkono wa Yehova “umenyooshwa, na ni nani anayeweza kuurudisha nyuma?” (Isa. 14:27) Kwa kuwa tuna hakika kwamba Yehova anabariki huduma yetu, acheni tuendelee kuhubiri “kwa ujasiri kwa mamlaka ya Yehova.”—Mdo. 14:3.