Kazi Yenye Kufurahisha Zaidi
1. Ni kazi gani ya uponyaji wa kiroho inayofanywa katika siku zetu?
1 Watu walioshuhudia uponyaji wa kimwili katika karne ya kwanza walijawa na shangwe. (Luka 5:24-26) Katika siku zetu, tunashangilia kazi ya uponyaji wa kiroho. (Ufu. 22:1, 2, 17) Inafurahisha kama nini kusoma masimulizi mbalimbali yanayoonyesha jinsi ambavyo Neno la Yehova na roho yake takatifu zimebadili maisha ya watu! Hata hivyo, linalofurahisha hata zaidi ni kushiriki katika kazi hii kwa kuongoza funzo la Biblia lenye maendeleo.
2. Tunaweza kupata shangwe gani tunapomfundisha mtu kweli?
2 Mungu anaitwa nani? Kwa nini anaacha watu wateseke? Ufalme wa Mungu utawafanyia nini wanadamu? Tunafurahi tunapojibu maswali kama hayo na pia tunapoona shangwe ambayo mwanafunzi anapata anapojifunza kweli. (Met. 15:23; Luka 24:32) Kadiri mwanafunzi anavyofanya maendeleo, huenda akaanza kutumia jina la Yehova, akabadili njia yake ya kuvaa na kujipamba, akaacha mazoea yenye kudhuru, na kuanza kuwahubiria wengine. Ikiwa atafanya maendeleo na kujiweka wakfu na kubatizwa, atakuwa ndugu yetu na mfanyakazi mwenzi. Kila moja ya hatua hizo nzuri zinafanya tushangilie.—1 The. 2:19, 20.
3. Tunaweza kuchukua hatua gani ili kuanzisha funzo la Biblia?
3 Unaweza Kushiriki? Ikiwa ungependa kushiriki kazi hii yenye kufurahisha zaidi, mwombe Yehova akusaidie uongoze funzo la Biblia, kisha utende kulingana na sala zako. (1 Yoh. 5:14) Hubiri mahali na wakati ambapo watu wanaweza kupatikana. Eleza watu kuhusu mpango wa funzo la Biblia katika kila pindi inayofaa. (Mhu. 11:6) Unapopata mtu anayependezwa na upande mbegu ya kweli, rudi uitie maji.—1 Kor. 3:6-9.
4. Kwa nini tunapaswa kuanzisha mafunzo ya Biblia tukizingatia nyakati tunamoishi?
4 Bado kuna watu wengi sana ambao wana njaa na kiu kwa ajili ya uadilifu. Ni nani atakayewasaidia kutimiza uhitaji wao wa kiroho kwa kujifunza Biblia pamoja nao? (Mt. 5:3, 6) Acheni tujitolee kwa hiari kukamilisha kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi kabla ya kazi ya mavuno kufikia kikomo.—Isa. 6:8.