Tufanye Yote Tuwezayo Kuonyesha Uthamini Wetu
Ukumbusho Utaadhimishwa Aprili 17
1. Ni mtazamo gani wa mtunga-zaburi unaofaa sana wakati wa Ukumbusho?
1 Mtunga-zaburi aliyethamini sana matendo mengi ya rehema na ya ukombozi ya Yehova, aliuliza hivi: “Nitamlipa Yehova nini kwa ajili ya faida zake zote kwangu?” (Zab. 116:12) Leo, watumishi wa Mungu wana sababu nyingi zaidi za kuonyesha shukrani. Mamia ya miaka baada ya maneno hayo kuandikwa, Yehova aliwapa wanadamu zawadi kubwa kuliko zote, yaani, fidia. Tunapojitayarisha kuadhimisha kifo cha Kristo siku ya Aprili 17, tuna sababu nzuri ya kuwa wenye shukrani.—Kol. 3:15.
2. Taja baadhi ya mambo yanayofanya tuthamini fidia.
2 Baraka Zinazotokana na Fidia: Kupitia fidia tunaweza “kusamehewa dhambi zetu.” (Kol. 1:13, 14) Hivyo, tunaweza kumwabudu Yehova kwa dhamiri safi. (Ebr. 9:13, 14) Tuna uhuru wa kusema tunaposali kwa Yehova. (Ebr. 4:14-16) Watu wanaoamini fidia wana tumaini zuri ajabu la kuishi milele!—Yoh. 3:16.
3. Tunaweza kumwonyesha Yehova jinsi gani kwamba tunathamini fidia?
3 Tunavyoonyesha Uthamini: Njia moja ya kuonyesha kwamba tunaithamini sana fidia ni kusoma Usomaji wa Biblia wa Ukumbusho na kutafakari kuuhusu. Makala katika Mnara wa Mlinzi, wa Februari 1, 2011, yenye kichwa “Je, Umejitayarisha kwa Ajili ya Siku Muhimu Zaidi Katika Mwaka?” ilitayarishwa ili kutusaidia kufanya hivyo. Tunaweza pia kumwambia Yehova katika sala kwamba tunathamini sana fidia. (1 The. 5:17, 18) Vilevile, tunaonyesha uthamini wetu kwa kutii amri ya Yesu ya kuhudhuria maadhimisho ya Ukumbusho. (1 Kor. 11:24, 25) Zaidi ya hayo, tunaweza kuiga upendo mkuu wa Yehova kwa kuwaalika watu wengi iwezekanavyo wajiunge nasi kuadhimisha Ukumbusho.—Isa. 55:1-3.
4. Tunapaswa kuazimia nini?
4 Watumishi wa Yehova wenye shukrani hawayaoni maadhimisho ya Ukumbusho kuwa mkutano wa kawaida tu. Ni mkutano muhimu kuliko yote katika mwaka! Siku ya Ukumbusho inapokaribia, na tuazimie kufanya kama mtunga-zaburi aliyeandika hivi: “Mbariki Yehova, Ee nafsi yangu, wala usiyasahau matendo yake yote.”—Zab. 103:2.