Kuonyesha Shukrani kwa Zawadi Bora Kutoka kwa Mungu
1. Kwa nini sisi humshukuru sana Yehova?
1 Fidia ambayo Yehova aliandaa kupitia Mwana wake mpendwa ndiyo zawadi bora kati ya “zawadi njema” nyingi kutoka kwake. (Yak. 1:17) Kupitia fidia tunaweza kupata baraka nyingi kutia ndani msamaha wa dhambi. (Efe. 1:7) Kwa sababu hiyo tunamshukuru Yehova siku zote. Hasa katika majira ya Ukumbusho sisi hutafakari juu ya fidia.
2. Tunawezaje kukuza uthamini wetu na wa familia yetu kuelekea fidia?
2 Saidia Familia Yako Ithamini Fidia: Katika majuma yanayotangulia Ukumbusho ambao utafanywa Machi 30, unaweza kupitia habari juu ya fidia wakati wa Ibada ya Familia, ili kuisaidia familia yako iithamini fidia. Pia, mkiwa familia, mnaweza kusoma Biblia kila siku kwa kufuata ratiba ya pekee ya usomaji wa Biblia wa Ukumbusho. Fikiria jinsi ambavyo fidia imekufaidi wewe binafsi na kuboresha mtazamo wako kumhusu Yehova, kujihusu mwenyewe, kuwahusu wengine, na kuhusu wakati ujao. Vilevile, utanufaika ukijizoeza kuimba nyimbo mbili mpya, yaani, namba 8 na 109, ambazo zitaimbwa katika Ukumbusho.—Zab. 77:12.
3. Tunaweza kuonyesha shukrani kwa fidia jinsi gani?
3 Kuonyesha Shukrani: Uthamini wetu kwa fidia hutusukuma tuwaeleze wengine kumhusu Yehova na upendo wake mwingi alioonyesha kwa kumtuma Mwana wake duniani. (Zab. 145:2-7) Baadhi ya familia huonyesha shukrani kwa kupanga ili angalau mmoja wao awe painia msaidizi katika mwezi wa Machi, Aprili, au Mei. Ikiwa hilo haliwezekani, je, unaweza ‘kununua wakati’ ili upanue utumishi wako? (Efe. 5:16) Pia, uthamini wetu kwa fidia utatuchochea tuwasaidie wengine wahudhurie Ukumbusho pamoja nasi. (Ufu. 22:17) Anza kuandika orodha ya watu ambao utawakaribisha, yaani, watu unaowarudia, wanafunzi wa Biblia, watu wa ukoo, wafanyakazi wenzako, na majirani, na kisha ushiriki kikamili katika kampeni ya pekee ya kuwakaribisha watu kwenye Ukumbusho.
4. Tunawezaje kutumia majira ya Ukumbusho kwa hekima?
4 Majira ya Ukumbusho yanaandaa fursa nzuri ya kumwonyesha Yehova kwamba tunathamini sana zawadi yake ya fidia kwa wanadamu. Acheni tutumie pindi hii kusitawisha uthamini wetu na kuonyesha shukrani kwa fidia na ‘utajiri wote usiopimika wa Kristo.’—Efe. 3:8.