Thamini Pendeleo Lako la Utumishi
1. Watu wengi ulimwenguni wanaionaje kazi yetu ya kuhubiri?
1 Wengi katika ulimwengu wa Shetani wanaiona kazi yetu ya kuhubiri kuwa “upumbavu.” (1 Kor. 1:18-21) Tusipokuwa waangalifu, maoni haya yaliyopotoka yanaweza kutuvunja moyo na kutufanya tupunguze bidii yetu. (Met. 24:10; Isa. 5:20) Tuna sababu gani za kuthamini pendeleo letu la kuwa Mashahidi wa Yehova?—Isa. 43:10.
2. Kwa nini huduma yetu inaweza kuitwa “kazi takatifu”?
2 “Kazi Takatifu”: Mtume Paulo alirejelea huduma kuwa “kazi takatifu.” (Rom. 15:15, 16) Ni kwa njia gani huduma yetu ni “kazi takatifu”? Kushiriki katika kazi ya kuhubiri hutufanya “wafanyakazi wenzi” na aliye “Mtakatifu,” Yehova, na huchangia kutakaswa kwa jina lake. (1 Kor. 3:9; 1 Pet. 1:15) Yehova huona kazi yetu ya kuhubiri kuwa “dhabihu ya sifa,” kwa hiyo huduma yetu ni sehemu muhimu ya ibada yetu.—Ebr. 13:15.
3. Ni nini kinachofanya kuhubiri habari njema kuwa pendeleo kubwa?
3 Kuhubiri habari njema ni pendeleo kubwa ambalo ni wachache tu wanaolifurahia. Malaika wangefurahia kushiriki katika mgawo huo na bila shaka wangeutimiza vizuri sana. (1 Pet. 1:12) Hata hivyo, Yehova ametuchagua sisi wanadamu wasio wakamilifu, “vyombo vya udongo,” kushiriki pendeleo hili kubwa sana!—2 Kor. 4:7.
4. Ni kwa njia gani tunaweza kuonyesha kwamba tunathamini utumishi?
4 Kazi ya Kutangulizwa: Kwa sababu tunathamini kikweli pendeleo letu, tunaona utumishi kama mojawapo ya “mambo yaliyo ya maana zaidi” katika maisha yetu. (Flp. 1:10) Kwa hiyo, tunapanga wakati kila juma ili tushiriki katika utumishi. Mwanamuziki anayethamini pendeleo lake la kucheza na kikundi fulani cha wanamuziki maarufu ulimwenguni atajitayarisha kwa kila onyesho na atajitahidi kuboresha ustadi wake. Vivyo hivyo, tutajitayarisha kabla ya kwenda katika utumishi ili tuweze ‘kulitumia sawasawa neno la kweli,’ na tutajitahidi kuboresha ‘ufundi wetu wa kufundisha.’—2 Tim. 2:15; 4:2.
5. Ni nani wanaothamini utumishi wetu?
5 Usiruhusu mtazamo wa watu wengi ukuvunje moyo. Kumbuka kwamba bado kuna wengi katika eneo letu wanaothamini tunapowatembelea. Hata hivyo, sisi hatutafuti kibali cha wanadamu. Jambo la maana zaidi ni jinsi Yehova anavyohisi, na anathamini sana jitihada zetu.—Isa. 52:7.