Lazima Mbegu Zitiwe Maji ili Zikue
1. Ni nini kinachopaswa kutiwa maji ili kikue?
1 Mbegu zilizopandwa shambani lazima zitiwe maji ili zikue. Ndivyo ilivyo pia na mbegu za kweli zinazopandwa katika mioyo ya watu katika eneo letu. (1 Kor. 3:6) Ni lazima tufanye ziara za kurudia na kuzitia maji mbegu hizo za mfano kwa kutumia Neno la Mungu ikiwa tunataka zitie mizizi, zikue na kusitawi.
2. Ni jinsi gani tunaweza kuweka msingi wa mazungumzo kwa ajili ya ziara itakayofuata?
2 Uliza Swali: Unapotayarisha mambo utakayozungumzia, tayarisha swali linaloamsha upendezi ambalo unaweza kujibu katika ziara ya kurudia. Uliza swali hilo unapomalizia mazungumzo katika ziara ya kwanza, kisha ufanye mipango hususa ya kurudi. Wengi hupata matokeo mazuri wanapochagua jambo fulani kutoka kwa kitabu Biblia Inafundisha wanaloweza kutumia kuonyesha jinsi ya kuongoza funzo la Biblia.
3. Ni mambo gani tunayoweza kutia ndani tunapoandika rekodi kuhusu mtu aliyependezwa?
3 Andika Rekodi: Mara tu unapomaliza ziara ya kwanza, hakikisha unaandika mambo yote mliyozungumzia. Andika jina la mtu huyo na anwani yake. Ni vizuri pia kuandika tarehe na wakati mlipozungumza naye, mambo mliyozungumzia, na chapisho ambalo ulimwachia. Je, alisema anashirikiana na dini fulani? Je, ana familia? Alitaja mambo yanayompendeza na yanayomhangaisha? Habari hiyo itakusaidia uweze kuzungumzia mambo yanayomfaa wakati ujao. Pia andika wakati mliokubaliana kurudi na swali utakalojibu.
4. Kwa nini tuendelee bila kuacha kuwarudia wanaopendezwa na ujumbe wetu?
4 Vumilia: Shetani hatapunguza bidii yake ya “kuliondoa neno” lililopandwa katika moyo wa mtu. (Marko 4:14, 15) Kwa hiyo, usikate tamaa inapokuwa vigumu kumpata tena mtu aliyependezwa. Je, unaweza kumtumia barua au kuacha ujumbe mfupi chini ya mlango? Painia mmoja alianzisha funzo la Biblia mlangoni na mwanamke fulani lakini hakuweza kumpata nyumbani tena, kwa hiyo akamtumia barua. Hatimaye, dada huyo alipompata nyumbani, mwanamke huyo alieleza jinsi moyo wake ulivyoguswa sana kwa sababu ya kuonyeshwa upendezi. Tunapozitia maji mbegu za kweli, tunaweza kupata shangwe inayotokana na kuona mbegu hizo zikichipuka, zikikua na kukomaa, na “kuzaa matunda mara 30 na 60 na 100.”—Marko 4:20.