Tunapaswa Kuwarudia Wanaopendezwa Baada ya Muda Gani?
1. Kufanya wanafunzi kunahusisha nini?
1 Kufanya wanafunzi kunahusisha kumrudia kila mtu anayeonyesha kwamba yuko tayari kujifunza kuhusu Ufalme wa Yehova. (Mt. 28:19, 20) Wakati unaofaa wa kufanya ziara ya kurudia mara nyingi unategemea fursa tuliyo nayo na vilevile fursa ya yule mtu anayependezwa. Kwa nini tunapaswa kurudi upesi baada ya ziara yetu ya kwanza?
2, 3. Kwa nini tunapaswa kujitahidi kurudi upesi iwezekanavyo?
2 Kwa Nini Turudi Upesi? Kazi ya kuhubiri “hii habari njema ya ufalme” imesonga sana, na mwisho wa ulimwengu huu umekaribia. (Mt. 24:14; 1 Pet. 4:7) Kwa hiyo, maadamu “siku ya wokovu” ingali ipo kwa watu wanaopendezwa, ni lazima ‘tuhubiri neno kwa bidii.’ Ili kutii agizo hilo tunapaswa kurudi upesi iwezekanavyo ili kumchochea mwenye nyumba aendelee kupendezwa.—2 Kor. 6:1, 2; 2 Tim. 4:2.
3 Lengo la Shetani ni kuharibu mbegu yoyote ya Ufalme ambayo huenda tukapanda katika moyo wa mtu anayependezwa. (Marko 4:14, 15) Mara nyingi wale wanaopendezwa wanadhihakiwa na watu wao wa familia, wafanyakazi wenzao, na wengineo. Tunaporudi upesi tunaweza kuendeleza mazungumzo tuliyoanzisha katika ziara iliyopita, na hivyo, kuwatia moyo waendelee kupendezwa na Biblia, kabla wengine hawajawavunja moyo.
4. Katika ziara ya kwanza, tunawezaje kuweka msingi kwa ajili ya ziara ya kurudia?
4 Fanya Mpango wa Kurudi: Ni vizuri kufanya mpango hususa wa kurudi, wakati wa ziara ya kwanza. Uliza swali ambalo utajibu katika ziara inayofuata. Ni muhimu kuandika mambo mliyozungumzia na pia siku na saa ambayo uliahidi utarudi. Ukiwa na nafasi, unaweza kumwuliza mwenye nyumba kama unaweza kurudi siku inayofuata au muda mfupi baadaye. Ikiwa ulimpata mwenye nyumba mwishoni mwa juma na anafanya kazi katikati ya juma, huenda akataka urudi mwishoni mwa juma linalofuata. Unapofanya mpango wa kurudi, hakikisha unatimiza ahadi yako.—Mt. 5:37.
5. Kwa kurudi bila kukawia, tunawezaje kutimiza vizuri zaidi utume wa kufanya wanafunzi tuliopewa na Yesu?
5 Tuna sababu nzuri sana za kuwarudia watu wanaopendezwa upesi iwezekanavyo. Kwa hiyo, fanya mpango na urudi upesi, kwa maana “wakati uliobaki umepungua.” (1 Kor. 7:29) Tunapowarudia upesi iwezekanavyo watu wanaopendezwa na ujumbe wa Ufalme, yaelekea jitihada zetu zitakuwa na mafanikio zaidi.