Fanya Mipango Sasa ya Kuongeza Utendaji Wako Katika Huduma
1. Tuna fursa gani kila mwaka katika majira ya Ukumbusho, na tunaweza kujitayarisha kwa njia gani?
1 Kila mwaka katika majira ya Ukumbusho tunapata fursa mpya za ‘kumsifu sana Yehova.’ (Zab. 109:30) Je, utaongeza utendaji wako katika huduma mwezi wa Machi? Hiyo ni njia moja ya kuonyesha kwamba unampenda Mungu aliyetoa fidia. Huu ndio wakati wa kuanza kufanya mipango.—Met. 21:5.
2. Wewe ulionaje kupunguzwa kwa takwa la saa kwa mapainia wasaidizi katika mwezi wa Aprili mwaka uliopita, na baadhi ya ndugu waliuunga mkono mpango huo jinsi gani?
2 Utumishi wa Painia Msaidizi: Mwaka uliopita ndugu walisisimuka sana waliposikia kwamba takwa la saa kwa mapainia wasaidizi lilipunguzwa katika mwezi wa Aprili. Ndugu mmoja aliandika hivi: “Mimi bado ninasoma shule ya sekondari, na sijafaulu kuwa painia wa kawaida. Lakini nitaomba kuwa painia msaidizi katika mwezi wa Aprili. Nitaomba kuhubiri kwa saa 30 nikiwa na lengo la kuhubiri kwa saa 50.” Dada anayefanya kazi ya wakati wote aliandika: “Ni rahisi sana kutimiza takwa la saa 30!” Mpango huo ulipotangazwa, dada aliyekuwa painia hapo awali na ambaye sasa ana umri wa miaka zaidi ya 80, alisema: “Nimengoja siku hii! Yehova anajua kwamba kipindi bora cha maisha yangu ni wakati nilipokuwa painia!” Ndugu na dada ambao hawakuweza kuwa mapainia wasaidizi walikuwa na lengo la kuongeza utendaji wao katika huduma.
3. Taja sababu za kushiriki katika utumishi wa painia msaidizi katika mwezi wa Machi, Aprili, na Mei.
3 Mwezi wa Machi utakuwa mwezi mzuri wa kuwa painia msaidizi kwa sababu tutaweza tena kuchagua takwa la saa 30 au la saa 50. Zaidi ya hayo, kuanzia Jumamosi, Machi 17, tutashiriki katika kampeni ya pekee ya kuwaalika watu kwenye Ukumbusho siku ya Aprili 5. Wengi watafurahia sana utendaji wao katika huduma mwezi wa Machi, hivi kwamba huenda wakataka kuwa mapainia wasaidizi pia katika mwezi wa Aprili na Mei, wakitimiza takwa la saa 50.
4. Tunaweza kuongeza utendaji wetu katika huduma jinsi gani, na matokeo yatakuwa nini?
4 Katika jioni ya Ibada ya Familia inayofuata, zungumzeni jinsi kila mtu katika familia atakavyoweza kufanya zaidi katika huduma katika majira ya Ukumbusho. (Met. 15:22) Omba Yehova abariki jitihada zenu. (1 Yoh. 3:22) Kwa kuongeza utendaji wako katika huduma, utamsifu Yehova zaidi, na utaongeza furaha yako.—2 Kor. 9:6.