Changia Shangwe Katika Majira Haya ya Ukumbusho!
1. Ni katika njia gani tunaweza kuongeza shangwe yetu katika majira haya ya Ukumbusho?
1 Je, ungependa kuongeza shangwe yako katika mwezi wa Machi, Aprili, na Mei? Njia moja ya kufanya hivyo ni kufanya mengi zaidi katika huduma na ikiwezekana, kufanya upainia msaidizi. Kufanya hivyo kutaongeza shangwe yako jinsi gani?
2. Ni jinsi gani kuongeza utumishi wetu kutatufanya tuwe wenye shangwe zaidi?
2 Ongeza Shangwe Yako: Yehova ametuumba na uwezo wa kupata shangwe na uradhi tukimwabudu na tukitosheleza uhitaji wetu tuliozaliwa nao wa mambo ya kiroho. (Mt. 5:3) Pia ametuumba katika njia ya kwamba tunaweza kupata furaha tunapotoa. (Mdo. 20:35) Utumishi hutuwezesha kutimiza mambo hayo mawili, yaani kumwabudu Yehova na kusaidia watu. Inapatana na akili kwamba kadiri tunavyoongeza utumishi wetu ndivyo shangwe yetu inavyoongezeka. Isitoshe, tunapohubiri zaidi, ustadi wetu unaongezeka. Kadiri tunavyopata ustadi ndivyo tunavyojiamini zaidi. Tutapata fursa nyingi za kuhubiri na kuanzisha mafunzo ya Biblia. Mambo haya yote yanafanya tufurahie sana huduma.
3. Kwa nini Machi na Aprili itakuwa miezi mizuri sana ya kufanya upainia msaidizi?
3 Machi na Aprili itakuwa miezi mizuri sana kufanya upainia msaidizi kwa sababu tunaweza kuchagua kutimiza takwa la saa 30 au 50. Kwa kuongezea, kuanzia Jumamosi, Machi 22, na kuendelea mpaka Jumatatu ya Ukumbusho, Aprili 14, tutashiriki kampeni yenye kufurahisha ya kukaribisha wengine wahudhurie Ukumbusho. Makutaniko yatasisimuka kwa kuwa wengi watafanya kazi “bega kwa bega” kugawa mialiko kwenye eneo ili wawafikie watu wengi iwezekanavyo katika muda uliowekwa.—Sef. 3:9.
4. Tunapaswa kufanya nini ikiwa tunataka kufanya upainia msaidizi?
4 Jitayarishe Sasa: Ikiwa bado hujachukua hatua ya kufanya upainia msaidizi, tumia wakati kupitia ratiba yako na kuona ni mabadiliko gani unayoweza kufanya ili kuongeza huduma yako kwa mwezi mmoja au zaidi. Sali kuhusu jambo hilo. (Yak. 1:5) Ongea na familia yako na wengine kutanikoni kuhusu jambo hilo. (Met. 15:22) Huenda ukaona kwamba licha ya matatizo ya afya au ratiba yenye mambo mengi, wewe pia unaweza kupata shangwe inayotokana na kufanya upainia msaidizi.
5. Kutakuwa na matokeo gani ikiwa tutaongeza utumishi wetu katika majira haya ya Ukumbusho?
5 Yehova anataka watumishi wake wawe wenye shangwe. (Zab. 32:11) Tunapojitahidi kuongeza utumishi wetu katika majira haya ya Ukumbusho, tutaongeza shangwe yetu na kufanya Baba yetu wa mbinguni ashangilie.—Met. 23:24; 27:11.