Ni Nini ‘Sababu Yako ya Kufurahi?’
1. Tuna sababu gani ya kufurahi kila mwisho wa mwezi?
1 Tunapoombwa kutoa ripoti zetu za utumishi wa shambani kila mwisho wa mwezi, ‘sababu yako ya kufurahi’ huwa nini? (Gal. 6:4) Iwe sisi ni mapainia wa pekee tunaoripoti saa 130 katika huduma au wahubiri waliokubaliwa kuripoti vipindi vya dakika 15, sote tunapaswa kushangilia kwamba tumemtolea Yehova utumishi wa nafsi yote.—Zab. 100:2.
2. Kwa nini tunapaswa kujitahidi sana katika utumishi wa Yehova?
2 Akiwa Bwana Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu wote, Yehova anastahili kupokea kilicho bora kutoka kwetu. (Mal. 1:6) Kwa sababu tunampenda, tumeweka maisha yetu wakfu kwake ili kufanya mapenzi yake. Hivyo basi, mwishoni mwa siku au mwezi, kila mmoja wetu ana sababu ya kufurahi ikiwa ana hakika kwamba ametoa “matunda ya kwanza” ya wakati, vipawa, na nguvu zake katika utumishi wa Yehova. (Met. 3:9) Hata hivyo, ikiwa dhamiri yetu inatuambia kwamba tunaweza kufanya vema zaidi, tunapaswa kuzingatia yale tunayoweza kufanya ili kuboresha hali yetu.—Rom. 2:15.
3. Kwa nini si jambo la hekima kujilinganisha na wengine?
3 “Si kwa Kujilinganisha na Mtu Yule Mwingine”: Si jambo la hekima kujilinganisha na wengine au kujilinganisha na jinsi tulivyokuwa wakati fulani tulipokuwa na nguvu nyingi zaidi. Hali hubadilika. Uwezo hutofautiana. Kujilinganisha huongoza kwenye mashindano au hisia za kujiona hatufai. (Gal. 5:26; 6:4) Yesu hakulinganisha mtu na yule mwingine. Badala yake, alimpongeza mtu kulingana na kile ambacho angeweza kutimiza.—Marko 14:6-9.
4. Ni masomo gani muhimu tunayoweza kujifunza kutokana na mfano wa Yesu kuhusu talanta?
4 Katika mfano wa Yesu kuhusu talanta, kila mfanyakazi alipokea talanta “kulingana na uwezo wake mwenyewe.” (Mt. 25:15) Bwana wao aliporudi na kuwaomba watoe ripoti kuhusu kazi yao, wale ambao walikuwa wamefanya kazi kwa bidii kulingana na hali na uwezo wao mbalimbali walipongezwa na kuingia katika shangwe ya bwana wao. (Mt. 25:21, 23) Vivyo hivyo, tunapoendelea kuwa na mengi ya kufanya katika kazi ya kuhubiri Ufalme, tunaweza kuwa na hakika kwamba tuna kibali cha Mungu na hivyo kuwa na sababu ya kufurahi!