Wasaidie Watu Wamsikilize Mungu
1. Ni broshua gani zilizotolewa katika Kusanyiko la Wilaya la “Ufalme wa Mungu na Uje!,” na ni nini kinachofanya broshua hizo kuwa vifaa vizuri sana?
1 Katika Kusanyiko la Wilaya la “Ufalme wa Mungu na Uje!,” broshua mbili mpya zilitolewa. Moja ina kichwa Msikilize Mungu Uishi Milele na ile nyingine ambayo ni toleo lililorahisishwa ina kichwa Msikilize Mungu. Kwa kuwa zina maneno machache, zinaweza kutafsiriwa haraka na kwa urahisi. Isitoshe, wakati ambapo broshua Msikilize Mungu Uishi Milele ilitolewa katika Kiingereza, tayari ilikuwa imeidhinishwa itafsiriwe katika lugha 431.
2. Ni nani watakaonufaika na broshua hizo?
2 Ni nani hasa watakaonufaika na broshua hizo? Fikiria hali zifuatazo ambazo hutukia mara nyingi ulimwenguni kote:
• Mhubiri anayezungumza na mwenye nyumba, katika ziara ya kwanza au anapomrudia, anatambua kwamba hajui kusoma au hawezi kusoma vizuri.
• Mhubiri anawahubiria watu wanaozungumza lugha ambayo hakuna chapisho lolote lililotafsiriwa katika lugha hiyo au ni machapisho machache tu yanayopatikana. Au watu wengi katika eneo hawawezi kusoma lugha ambayo wanapenda kuzungumza.
• Mhubiri anatumia lugha ya ishara kuwahubiria viziwi katika eneo lake.
• Mzazi anataka kumfundisha kweli mtoto wake mchanga ambaye bado hajajua kusoma.
3. Habari katika broshua Msikilize Mungu zina mpangilio gani?
3 Mpangilio wa Yaliyomo: Msikilize Mungu ina maandishi machache sana kwenye sehemu ya chini ya kila ukurasa ambayo ni sentensi rahisi na andiko ambalo linakazia jambo kuu. Kwa nini? Wazia kwamba mtu fulani amekupa broshua ambayo imeandikwa katika lugha usiyoelewa, na labda katika herufi ambazo hufahamiani nazo. Je, ungevutiwa nayo, hata kama ina picha zinazopendeza? Yaelekea haingekuvutia. Vivyo hivyo, watu ambao hawawezi kusoma hawavutiwi na machapisho yenye maandishi. Hivyo basi, katika kila ukurasa, jambo linalojitokeza sana ni picha zilizotayarishwa kwa uangalifu, na alama za mshale zinazosaidia kuelekeza mazungumzo kutoka picha moja hadi nyingine.
4. Habari katika broshua Msikilize Mungu Uishi Milele zina mpangilio gani?
4 Msikilize Mungu Uishi Milele ina picha zinazofanana na zile zilizo katika broshua Msikilize Mungu. Imekusudiwa kutumiwa tunapojifunza na watu ambao hawawezi kusoma vizuri au wanaojifunza kusoma. Mhubiri anaweza kutumia broshua hii hata anapojifunza Biblia pamoja na mtu ambaye anatumia broshua Msikilize Mungu. Kwenye pembe ya juu ya upande wa kushoto wa kila somo lenye kurasa mbili, kuna swali ambalo jibu lake linapatikana katika kurasa hizo. Pamoja na picha hizo, kuna maelezo na maandiko. Kuelekea pembe ya chini ya kurasa nyingi, kuna sanduku lenye rangi ambalo lina hoja za ziada na Maandiko ambayo yanaweza kuzungumziwa, kulingana na uwezo wa mwanafunzi.
5. Tunaweza kutumia broshua hizo wakati gani na jinsi gani?
5 Jinsi ya Kuzitumia: Unaweza kuzitumia katika huduma ya nyumba kwa nyumba wakati wowote unapoona ni vizuri kufanya hivyo, hata wakati ambapo hatuwatolei watu broshua mwezi huo. (Ona sanduku “Jinsi Zinavyoweza Kutolewa.”) Unaweza kuanza kuzitumia katika ziara za kurudia kwa kumweleza mtu aliyependezwa kwamba una kitu fulani cha kumwonyesha na kisha umpe mojawapo ya broshua hizo.
6. Tutaongozaje funzo la Biblia kwa kutumia broshua hizo?
6 Kwa kuwa Msikilize Mungu haina maswali yaliyochapishwa, mazungumzo hayatakuwa ya maswali-na-majibu kama tunavyofanya tunapoongoza funzo kwa kutumia kitabu Biblia Inafundisha. Katika kila tamaduni, watu hupenda kusikiliza hadithi. Kwa hiyo, tumia picha kueleza hadithi za mambo ambayo yameandikwa katika Biblia kwa mwongozo wa roho ya Mungu. Zungumzia picha. Uwe mwenye shauku. Mwombe mwanafunzi atoe maoni yake kuhusu picha hizo. Soma maandiko yaliyo kwenye sehemu ya chini ya ukurasa na mzungumzie maandiko hayo. Muulize maswali ili ashiriki katika mazungumzo na ili utambue ikiwa ameelewa. Iwapo anatumia Msikilize Mungu Uishi Milele, someni pamoja maelezo na maandiko yaliyopo mnapozungumzia kila picha.
7. Tunaweza kumsaidiaje mwanafunzi wa Biblia afanye maendeleo?
7 Msaidie Mwanafunzi Afanye Maendeleo: Tunatumaini kwamba mazungumzo pamoja na mwanafunzi wako wa Biblia yatamchochea kutaka kujifunza kusoma ili aweze kujifunza mwenyewe kumhusu Yehova. (Mt. 5:3; Yoh. 17:3) Hivyo basi, ikiwa mazungumzo yanategemea Msikilize Mungu, labda unaweza kujitolea kumfundisha mwanafunzi huyo kusoma iwapo utaona kwamba yuko tayari kufanya hivyo. Unaweza pia kuanza kujifunza naye kwa kutumia broshua Msikilize Mungu Uishi Milele. Hata iwe mtatumia broshua gani, mwanafunzi hatakuwa tayari kwa ubatizo baada ya kumaliza kujifunza broshua hiyo. Unapaswa kuanza kujifunza naye kitabu Biblia Inafundisha au chapisho lingine lolote linalofaa ambalo litamwezesha kuielewa Biblia vizuri zaidi.
8. Kwa nini unathamini vifaa hivi vipya tutakavyotumia katika huduma?
8 Ni lazima watu wamsikilize Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu ili waishi milele. (Isa. 55:3) Na mapenzi ya Yehova ni kwamba “watu wa namna zote,” kutia ndani wale wasiojua kusoma, wajifunze jinsi ya kumsikiliza. (1 Tim. 2:3, 4) Tunashukuru kama nini kupokea vifaa hivi vipya ambavyo tunaweza kuvitumia kuwafundisha watu jinsi ya kumsikiliza Mungu!
[Sanduku katika ukurasa wa 3]
Jinsi Zinavyoweza Kutolewa
Mwonyeshe mwenye nyumba ukurasa wa 2-3 na useme: “Ungependa kuishi katika ulimwengu ulio kama huu? [Mruhusu ajibu.] Maandiko yanatoa ahadi [au kitabu hiki kitakatifu kinatoa ahadi] kwamba karibuni Mungu ataifanya dunia iwe mahali penye kupendeza, na penye amani bila umaskini au magonjwa. Ona kile tunachopaswa kufanya ili tuishi katika ulimwengu kama huo. [Soma andiko la Isaya 55:3, ambalo limetajwa katika sehemu ya juu ya ukurasa wa 3.] Andiko hili linatuambia tumwendee Mungu na ‘kumsikiliza.’ Lakini tunamsikilizaje Mungu?” Fungua ukurasa wa 4-5, na mzungumzie jibu. Ikiwa hana wakati, mwachie broshua na ufanye mipango ya kurudi ili kuzungumzia jibu.