Linda Akili Yako
1. Programu ya kusanyiko la mzunguko la mwaka wa utumishi wa 2013 ina kichwa gani, na ni nini kusudi la programu hiyo?
1 Yesu aliwaagiza wanafunzi wake wampende Yehova kwa moyo, nafsi, na akili zao zote. (Mt. 22:37, 38) Programu za kusanyiko la wilaya, la mzunguko, na la pekee tunazotarajia zimekusudiwa kutusaidia kujiimarisha jinsi tulivyo kwa ndani. Kama unavyokumbuka, kichwa cha kusanyiko letu la wilaya ni “Linda Moyo Wako! ” Kichwa cha programu ya kusanyiko la siku ya pekee la mwaka wa utumishi wa 2013 ni, “Linda Dhamiri Yako.” Na makusanyiko ya mzunguko ambayo yataanza mwezi ujao ni yenye kichwa “Linda Akili Yako,” kinachotegemea Mathayo 22:37. Programu hiyo imekusudiwa kumsaidia kila mmoja wetu achanganue fikira zake akiwa na lengo la kuzifanya zimpendeze Yehova zaidi.
2. Tunaposikiliza programu, tunapaswa kutafuta majibu ya maswali gani?
2 Mambo Yatakayozungumziwa: Tunaposikiliza programu ya kusanyiko la mzunguko, tunapaswa kutafuta majibu ya maswali yafuatayo ambayo yanakazia mambo makuu:
• Tunaweza kuepukaje kuwa na ‘fikira za wanadamu’?
• Tunawezaje kuuondoa utaji unaopofusha akili za wasioamini?
• Tunataka kuwa na mtazamo gani wa akili?
• Kutafakari kunakofaa kuna faida gani?
• Tunawezaje kumruhusu Yehova afinyange kufikiri kwetu?
• Waume, wake, wazazi, na watoto wanawezaje kuchangia furaha ya familia?
• Tunaweza kufanya nini ili tuwe tayari kwa ajili ya siku ya Yehova?
• Kukaza akili zetu kwa ajili ya utendaji kunamaanisha nini?
• Ni faida gani inayopatikana na wale wanaotumia mambo wanayojifunza?
3. Kwa nini ni muhimu tuhudhurie siku zote mbili, tusikilize kwa makini, na tutumie mambo tunayojifunza?
3 Shetani anapigana vita ili kuharibu akili zetu. (2 Kor. 11:3) Hivyo basi, ni lazima tulinde akili zetu na kudhibiti mawazo yetu. Tunahitaji kuendelea kuwa na akili ya Kristo na kupinga uvutano wa ulimwengu huu wenye kuasi sheria. (1 Kor. 2:16) Hivyo basi, fanya mipango ya kuhudhuria siku zote mbili za kusanyiko la mzunguko. Sikiliza kwa makini. Kutumia habari hiyo muhimu itakayozungumziwa kutatusaidia kukaza akili zetu ili tuwe wenye bidii katika utumishi wa Ufalme.—1 Pet. 1:13.