Uandalizi kwa Wahudumu Wakristo
1. Ni mpango gani mpya ulioanzishwa mwaka wa 1938, na kwa kusudi gani?
1 Katika mwaka wa 1938, tengenezo la Yehova lilianzisha mpango mpya. Vikundi vya makutaniko vilialikwa kuhudhuria makusanyiko ya kanda ya dunia, ambayo sasa ni makusanyiko ya mzunguko. Kwa kusudi gani? Informant (ambayo sasa ni Huduma Yetu ya Ufalme) ya Januari 1939 ilijibu: “Makusanyiko haya ni sehemu ya Tengenezo la Yehova la Kitheokrasi kwa ajili ya utendaji wa utumishi wake wa Ufalme. Maagizo yanayotolewa katika makusanyiko haya ni muhimu kwa kila mmoja ili kufanya vizuri kazi tuliyopewa.” Tunapoona ongezeko la watangazaji wa Ufalme kutoka 58,000 tu katika mwaka wa 1938 hadi zaidi ya 7,000,000 katika mwaka 2009, ni wazi kwamba makusanyiko ya mzunguko yanatimiza kusudi lake la kuwasaidia wahudumu “kufanya kazi tuliyopewa”!
2. Ni habari gani zitakazozungumziwa katika kusanyiko letu la mzunguko la mwaka mpya wa utumishi?
2 Kichwa cha Kusanyiko la Mzunguko la Mwaka Ujao: Tunatazamia kwa hamu kusanyiko la mzunguko na kitia moyo tutakachopata katika kusanyiko hilo kuanzia mwezi wa Septemba. Kichwa cha kusanyiko hilo “Ninyi Si Sehemu ya Ulimwengu” kinategemea andiko la Yohana 15:19. Ni zipi baadhi ya hotuba ambazo kwa kweli zitawanufaisha wahudumu Wakristo? Siku ya Jumamosi tutasikiliza hotuba yenye kichwa “Jinsi Utumishi wa Wakati Wote Unavyotulinda.” Pia tutafurahia mfululizo wenye sehemu tatu ulio na kichwa “Usichafuliwe na . . .” “Mnyama-Mwitu,” “Kahaba Mkubwa,” na “Wanabiashara Wanaosafiri.” Siku ya Jumapili tutasikiliza mfululizo wenye kichwa “Mpende Yehova, Usiupende Ulimwengu.” Hotuba nyingine zatia ndani “Endeleeni ‘Kama Wageni na Wakaaji wa Muda’” na “Jipe Moyo! Unaweza Kuushinda Ulimwengu.”
3. Tunaweza kupata faida gani kwa kuhudhuria kusanyiko la mzunguko?
3 Baada ya kuhudhuria kusanyiko la mzunguko la hivi karibuni, dada mmoja aliyekuwa amepunguza bidii yake katika huduma aliandika kwamba programu hiyo ilimsaidia kuchunguza hali zake na kuazimia “kwenda utumishi na kuacha kutoa visababu vya kutohubiri!” Bila shaka programu ya kusanyiko la mzunguko la mwaka mpya wa utumishi itatusaidia sote kumpenda Yehova badala ya kuupenda ulimwengu. (1 Yoh. 2:15-17) Hakikisha unahudhuria na kusikiliza kwa makini ili ufaidike kikamili kutokana na uandalizi huo wenye upendo kwa wahudumu Wakristo!