Tumia Utangulizi Wenye Matokeo
1. Tunaweza kujifunza nini kutokana na tangulizi mbalimbali ambazo Wakristo wa mapema walitumia?
1 Wakristo wa mapema waliwahubiria habari njema watu wa tamaduni na dini mbalimbali. (Kol. 1:23) Ingawa walihubiri ujumbe uleule, yaani, Ufalme wa Mungu, walitumia tangulizi mbalimbali ikitegemea wasikilizaji. Kwa mfano, alipozungumza na Wayahudi ambao waliheshimu sana Maandiko, Petro alianza kwa kumnukuu nabii Yoeli. (Mdo. 2:14-17) Kwa upande mwingine, ona jinsi Paulo alivyosababu na Wagiriki katika kitabu cha Matendo 17:22-31. Leo, watu katika maeneo fulani wanaheshimu Maandiko, nasi tunaweza kuirejelea Biblia kwa uhuru tunapohubiri nyumba kwa nyumba. Hata hivyo, huenda tukahitaji kuwa wenye busara zaidi tunapozungumza na wale ambao hawapendezwi na Biblia au dini au wale ambao si wa dini za Kikristo.
2. Tunaweza kutumiaje matoleo ya machapisho kuwasaidia wale wanaopendezwa na wale wasiopendezwa na Biblia?
2 Tumia Matoleo ya Machapisho kwa Njia Bora Zaidi: Matoleo ya machapisho ya mwaka huu wa utumishi yatabadilika kila baada ya miezi miwili nayo yatatia ndani magazeti, trakti, na broshua. Hata kama watu katika eneo letu hawapendezwi na Biblia kwa ujumla, bado tutaweza kuzungumza nao kuhusu jambo litakalowavutia kutoka katika mojawapo ya machapisho hayo. Huenda tusisome andiko katika ziara ya kwanza au kurejelea Biblia moja kwa moja, lakini ikiwa mwenye nyumba ameonyesha upendezi tunaweza kurudi tukiwa na lengo la kumsaidia ajenge imani katika Muumba na Neno lake lililoongozwa kwa roho. Kwa upande mwingine, ikiwa tunawahubiria watu ambao wanaiheshimu Biblia tunaweza kutumia chapisho na utangulizi unaoonyesha jambo hilo. Isitoshe, tunaweza kutoa kitabu Biblia Inafundisha au broshua Msikilize Mungu au Msikilize Mungu Uishi Milele wakati wowote ule, bila kuzingatia toleo la mwezi huo. Jambo kuu ni kutumia utangulizi utakaomchochea mtu apendezwe na Yehova.
3. Ni katika njia gani mioyo ya watu katika eneo letu ni kama udongo?
3 Tayarisha Udongo: Moyo wa mtu ni kama udongo. (Luka 8:15) Udongo mwingine huhitaji matayarisho zaidi kabla mbegu za kweli ya Biblia hazijaanza kutia mizizi na kuanza kukua. Waeneza-injili wa karne ya kwanza walipanda kwa mafanikio katika aina zote za udongo na jambo hilo liliwaletea uradhi na shangwe. (Mdo. 13:48, 52) Tunaweza kupata mafanikio kama hayo kwa kutilia maanani utangulizi wetu.