Je, Wewe Utafanya Upainia Msaidizi?
1. Kwa nini majira ya Ukumbusho ni wakati mzuri wa kuongeza huduma yetu?
1 Majira ya Ukumbusho ni wakati mzuri wa kuongeza huduma yetu. Ni wakati ambao tunatafakari kuhusu upendo mkubwa wa Yehova wa kumtoa Mwana wake kuwa fidia. (Yoh. 3:16) Tunamshukuru sana Yehova kwa mambo ambayo ametufanyia na hilo huongeza tamaa yetu ya kuwaambia wengine kumhusu Yehova na mambo anayowafanyia wanadamu. (Isa. 12:4, 5; Luka 6:45) Pia, ni pindi ambayo tunafurahia kampeni ya pekee ya kuwaalika rafiki zetu na watu katika eneo wajiunge nasi kuhudhuria Ukumbusho. Kisha, tunajitahidi kusitawisha upendezi wa wale waliohudhuria. Je, utaongeza huduma yako kwa kufanya upainia msaidizi mwezi wa Machi, Aprili, au Mei?
2. Kwa nini Machi ni mwezi mzuri sana wa kufanya upainia msaidizi?
2 Fanya Utendaji wa Mwezi wa Machi Kuwa wa Pekee: Mwezi wa Machi utakuwa wakati mzuri sana wa kufanya upainia msaidizi. Wale ambao wangependa kuwa mapainia wasaidizi wanaweza kuchagua kutimiza takwa la saa 30 au 50. Ikiwa mwangalizi wa mzunguko anatembelea kutaniko katika mwezi wa Machi, mapainia wasaidizi wanaweza kuhudhuria kipindi chote cha mkutano ambao yeye hufanya pamoja na mapainia wa kawaida na wa pekee. Muda wa kampeni ya kugawanya mialiko ya Ukumbusho utakaofanywa Jumanne, Machi 26, 2013, umeongezwa ukilinganishwa na miaka iliyopita. Kampeni hiyo itaanza Machi 1. Kwa kuongezea, mwezi wa Machi una miisho juma mitano. Hivyo basi, kwa nini usifikirie kwa uzito ikiwa unaweza kushiriki katika kufanya utendaji wa mwezi wa Machi kuwa wa pekee zaidi mwaka huu?
3. Ni kwa njia gani tunaweza kufanya mipango ili kuongeza huduma yetu?
3 Fanya Mipango Sasa: Huu ndio wakati wa kupitia ratiba yako na kuona ni mabadiliko gani unayohitaji kufanya ili uwe painia. Ushirikiano katika familia ni muhimu, kwa hiyo tumia wakati mnapofanya Ibada ya Familia jioni kuzungumzia miradi ya familia yako na utengeneze ratiba. (Met. 15:22) Ikiwa huwezi kufanya upainia msaidizi, usivunjike moyo. Je, unaweza kufanya mabadiliko katika ratiba yako ili utumie muda mrefu zaidi katika siku unazohubiri? Je, unaweza kupata siku ya ziada katikati ya juma ili ushiriki katika utumishi wa shambani?
4. Ni faida gani tutakazopata kwa kuongeza utendaji wetu katika miezi ya Machi, Aprili, na Mei?
4 Kadiri tunavyoongeza utendaji wetu katika miezi ya Machi, Aprili, na Mei, ndivyo tutakavyopata shangwe na uradhi unaotokana na kumtumikia Yehova na kuwapa wengine. (Yoh. 4:34; Mdo. 20:35) Jambo muhimu zaidi ni kwamba jitihada zetu za kujitoa bila ubinafsi zitamletea Yehova shangwe.—Met. 27:11.