Wachukueni Manabii Kuwa Kielelezo—Yona
1. Yona alikuwa na sifa gani nzuri?
1 Ni jambo gani huja akilini unapomfikiria nabii Yona? Watu fulani humwona kuwa mwoga au asiye na huruma. Hata hivyo, ni wazi kwamba alionyesha unyenyekevu, ujasiri, na roho ya kujidhabihu. Tunawezaje ‘kuchukua kuwa kielelezo’ sifa zenye kutamanika za nabii Yona?—Yak. 5:10.
2. Tunawezaje kuiga unyenyekevu wa Yona?
2 Unyenyekevu: Mwanzoni, Yona alikimbia mgawo wake na kuelekea upande tofauti. Jambo hilo halishangazi kwa sababu Waashuru walikuwa wakatili sana, na Ninawi lilikuja kuitwa “jiji la umwagaji wa damu.” (Nah. 3:1-3) Hata hivyo, Yehova alimtia nidhamu Yona, ambaye alionyesha unyenyekevu kwa kukubali mgawo wake alipopewa nafasi nyingine. (Met. 24:32; Yona 3:1-3) Licha ya kwamba mwanzoni alikimbia mgawo wake, alifanya mapenzi ya Yehova. (Mt. 21:28-31) Je, tumeazimia kama Yona kuhubiri habari njema, hata ikiwa tumetiwa nidhamu au tunahubiri katika eneo gumu?
3. Ni sehemu gani za utumishi wako zinazohitaji uwe na ujasiri na mwenye kujidhabihu?
3 Ujasiri na Kujidhabihu: Yona alipotambua kuwa uamuzi wake mbaya ulihatarisha maisha ya mabaharia, alikuwa tayari kudhabihu uhai wake. (Yona 1:3, 4, 12) Baadaye, alipokuwa akitimiza utume wake katika jiji la Ninawi, alienda hadi katikati kabisa ya jiji, labda akitafuta mahali panapofaa ili kutangaza hukumu ya Yehova. Hayo yalikuwa matendo, si ya mtu mwoga, bali ya nabii wa Mungu mwenye ujasiri! (Yona 3:3, 4) Namna gani sisi leo? Tunahitaji ujasiri kutoka kwa Mungu ili kutoa ushahidi kwa ujasiri tunapokabiliana na upinzani. (Mdo. 4:29, 31) Tunahitaji kuwa na roho ya kujidhabihu ili kutumia wakati na mali katika huduma.—Mdo. 20:24.
4. Kwa nini tunapaswa kutumia wakati ili kutafakari kielelezo kizuri kilichowekwa na manabii wa Yehova?
4 Kila wakati unaposoma simulizi fulani kuhusu nabii wa Yehova, utafaidika iwapo utajiwazia mwenyewe ukiwa katika hali hizo. Jiulize hivi: ‘Mimi ningetendaje? Ninawezaje kuiga sifa zake nzuri katika maisha yangu?’ (Ebr. 6:11, 12) Makala zijazo katika Huduma Yetu ya Ufalme zitazungumzia mambo mengine muhimu tunayoweza kujifunza kutoka kwa manabii wengine waaminifu wa Yehova.