Marejeo ya Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha
JULAI 1-7
Kutafuta Hazina za Kiroho
it-2 169 ¶3-5
Ufalme wa Mungu
“Ufalme wa Mwana Wake Mpendwa.” Siku kumi baada ya Yesu kwenda mbinguni, Pentekoste ya 33 W.K., wanafunzi wake walipata uthibitisho kwamba alikuwa “[ameinuliwa] kwenye mkono wa kuume wa Mungu” wakati ambapo Yesu alimimina roho takatifu juu yao. (Mdo 1:8, 9; 2:1-4, 29-33) Hivyo, “agano jipya” likaanza kufanya kazi kuwaelekea, nao wakawa sehemu ya kwanza ya ‘taifa jipya takatifu,’ Israeli la kiroho.—Ebr 12:22-24; 1Pe 2:9, 10; Gal 6:16.
Wakati huo Kristo alikuwa ameketi kwenye mkono wa kuume wa Baba yake na alikuwa Kichwa cha kutaniko hilo. (Efe 5:23; Ebr 1:3; Flp 2:9-11) Maandiko yanaonyesha kwamba kuanzia Pentekoste 33 W.K. na kuendelea, ufalme wa kiroho ulianzishwa juu ya wanafunzi wake. Alipowaandikia Wakristo katika jiji la Kolosai, mtume Paulo alisema kwamba Yesu Kristo tayari alikuwa na ufalme: “[Mungu] alituokoa kutoka kwenye mamlaka ya giza na kutuingiza katika ufalme wa Mwana wake mpendwa.”—Kol 1:13; linganisha Mdo 17:6, 7.
Ufalme wa Kristo kuanzia Pentekoste 33 W.K. na kuendelea umekuwa utawala wa kiroho juu ya Israeli la kiroho, Wakristo ambao wamezaliwa na roho ya Mungu na kuwa watoto wa kiroho wa Mungu. (Yoh 3:3, 5, 6) Wakristo hao waliozaliwa kwa roho wanapopata thawabu yao ya mbinguni, hawaendelei kuwa raia wa kidunia wa ufalme wa Kristo, bali wanakuwa wafalme pamoja na Kristo mbinguni.—Ufu 5:9, 10.
JULAI 8-14
Kutafuta Hazina za Kiroho
it-1 863-864 ¶9
Uasherati
Uasherati ni kosa ambalo linaweza kufanya mtu afukuzwe (atengwe na ushirika wa) kutaniko la Kikristo. (1Ko 5:9-13; Ebr 12:15, 16) Mtume huyo anaeleza kwamba Mkristo anayefanya uasherati anautendea dhambi mwili wake mwenyewe, akitumia viungo vya uzazi kinyume cha kusudi lake. Anaathiriwa vibaya sana kiroho na analichafua kutaniko la Mungu, na anaweza kupata magonjwa hatari ya zinaa. (1Ko 6:18, 19) Anaingilia haki za ndugu zake Wakristo (1Th 4:3-7) kwa (1) kuleta uchafu na kufanya upumbavu wenye kufedhehesha na shutuma kutanikoni (Ebr 12:15, 16), (2) kumnyima yule anayefanya naye uasherati msimamo safi wa kiadili na, ikiwa mtu huyo ni mseja, anamnyima haki ya kuwa safi anapooa au kuolewa, (3) kuinyang’anya familia yake rekodi ya kuwa na msimamo safi wa maadili, na vilevile (4) kuwakosea wazazi, mume, au mchumba wa yule anayefanya naye uasherati. Hampuuzi mwanadamu ambaye sheria zake huenda ziruhusu au zikataze uasherati, bali anampuuza Mungu ambaye atamhukumu kwa dhambi yake.—1Th 4:8.
JULAI 15-21
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | 2 WATHESALONIKE 1-3
it-1 972-973
Ujitoaji-Kimungu
Kuna fumbo lingine, ambalo linapingana na “siri takatifu” ya Yehova. Ni “fumbo la uasi sheria huu.” Hilo lilikuwa fumbo kwa Wakristo wa kweli kwa sababu katika siku za mtume Paulo, utambulisho wa “mtu wa uasi sheria” haukuwa umeonekana wazi na kuwa jamii inayotambuliwa kwa urahisi. Hata baada ya “mtu” huyo kuonekana, utambulisho wake ungeendelea kuwa fumbo kwa watu wengi kwa sababu uovu wake ungefichwa kwa njia ya kwamba watu wangefikiri ni ujitoaji-kimungu. Kwa kweli, uasi huo ungekuwa uasi-imani, tofauti na ujitoaji-kimungu wa kweli. Paulo alisema kwamba “fumbo la uasi sheria huu” lilikuwa tayari likifanya kazi katika siku zake, kwa sababu kulikuwa na uvutano wa uasi sheria katika kutaniko la Kikristo ambao mwishowe ungetokeza kikundi cha waasi-imani. Mwishowe, huyo mtu angeangamizwa na Yesu Kristo wakati wa kuwapo kwake. “Mtu” huyo mwasi anayeongozwa na Shetani angejiinua “juu ya wale wanaoitwa mungu au vitu vinavyoabudiwa” (Kigiriki, seʹba·sma). Hivyo mpinzani huyu mkuu wa Mungu akitumiwa na Shetani angedanganya sana na kuwasababishia uharibifu wale wanaofuata mazoea yake. Kwa sababu ya kuficha uovu wake kwa ujitoaji-kimungu wa kinafiki “mtu wa uasi sheria” angefanikiwa sana.—2Th 2:3-12; linganisha Mt 7:15, 21-23.
it-2 245 ¶7
Uwongo
Yehova Mungu anaruhusu watu wanaopendelea uwongo “wapotoshwe kupitia udanganyifu, na hivyo waamini uwongo” badala ya habari njema kumhusu Yesu Kristo. (2Th 2:9-12) Kanuni hii inaonyeshwa wazi na mambo yaliyotukia karne nyingi mapema katika kisa cha Mfalme Ahabu wa Israeli. Manabii wa uwongo walimhakikishia Ahabu kwamba angeshinda vita dhidi ya Ramothi-gileadi, ingawa Mikaya, nabii wa Yehova, alitabiri msiba. Mikaya aliona katika maono, Yehova akimruhusu kiumbe wa roho kuwa “roho ya udanganyifu” katika vinywa vya manabii wote wa Ahabu. Kwa maneno mengine, kiumbe huyo wa roho alitumia mamlaka yake juu yao hivi kwamba wakasema kile ambacho wao wenyewe walitaka kusema na kile ambacho Ahabu alitaka kusikia kutoka kwao, badala ya kumwambia ukweli. Ingawa alionywa mapema, Ahabu alichagua kudanganywa na uwongo waliomwambia na akafa kwa sababu hiyo.—1Fa 22:1-38; 2Nya 18.
Kutafuta Hazina za Kiroho
it-1 834 ¶5
Moto
Petro aliandika kwamba “mbingu na dunia zilizopo sasa zimewekwa akiba kwa ajili ya moto.” Kutokana na muktadha, na kulingana na maandiko mengine, ni wazi kwamba huo si moto halisi bali unawakilisha uharibifu wa milele. Kama vile Gharika ya siku za Noa haikuharibu mbingu na dunia halisi, bali watu wasiomwogopa Mungu, hivyo ndivyo ufunuo wa Yesu Kristo akiwa pamoja na malaika wake wenye nguvu utakavyoleta uharibifu wa kudumu kwa wale wasiomwogopa Mungu na juu ya mfumo mwovu wa mambo ambao wao ni sehemu yake.—2Pe 3:5-7, 10-13; 2Th 1:6-10; linganisha Isa 66:15, 16, 22, 24.
it-1 1206 ¶4-6
Kuongozwa na Roho
“Maneno Yaliyoongozwa na Roho”—Ya Kweli na ya Uwongo. Neno la Kigiriki pneuʹma (roho) linatumiwa kwa njia ya pekee katika maandishi fulani ya mitume. Kwa mfano, katika 2 Wathesalonike 2:2, mtume Paulo aliwaonya akina ndugu Wathesalonike wasisisimke au kutikiswa upesi kutoka kwenye kufikiri kwao iwe ni kwa “maneno yaliyoongozwa na roho au ujumbe uliosemwa au barua inayodhaniwa kutoka kwetu, kwamba siku ya Yehova imefika.” Ni wazi kwamba Paulo anatumia neno pneuʹma (roho) kuhusiana na njia ya mawasiliano, kama vile “ujumbe unaopitishwa kwa mdomo” au “barua.” Kwa sababu hiyo, kitabu kimoja (Lange’s Commentary on the Holy Scriptures uku. 126) kinasema hivi kuhusu andiko hilo: “Kwa hili Mtume anamaanisha mwonekano wa kiroho, utabiri wa kujifanya, maneno ya nabii.” (Imetafsiriwa na kuhaririwa na P. Schaff, 1976) Kitabu Word Studies in the New Testament cha Vincent kinasema: “Kupitia roho. Kupitia maneno ya kinabii kutoka kwa watu katika makusanyiko ya Kikristo, wakidai kwamba wana mamlaka ya kutoa ufunuo kutoka kwa Mungu.” (1957, Buku la 4, uku. 63) Hivyo, ingawa tafsiri fulani zinatafsiri neno pneuʹma katika kisa hiki na visa vingine vinavyofanana na hiki kuwa “roho,” tafsiri nyingine zinasema “ujumbe wa Roho” (AT), “utabiri” (JB), “ulioongozwa na roho” (D’Ostervald; Segond [Kifaransa]), “maneno yaliyoongozwa na roho” (NW).
Maneno ya Paulo yanaonyesha kwamba kuna ‘maneno ya kweli yaliyoongozwa na roho’ na ya uwongo. Alitaja aina zote mbili kwenye 1 Timotheo 4:1 aliposema kwamba “neno lililoongozwa na roho [kutoka kwa roho takatifu ya Yehova] linasema wazi kwamba wakati ujao watu fulani wataiacha imani, wakisikiliza maneno ya uwongo yaliyoongozwa na roho waovu na mafundisho ya roho waovu.” Hilo linatambulisha chanzo cha ‘maneno ya uwongo yaliyoongozwa na roho’ kuwa ni roho waovu. Hilo linaungwa mkono na maono ambayo mtume Yohana alipewa alipoona “maneno matatu machafu yaliyoongozwa na roho,” ambayo yalionekana kama vyura, yakitoka katika kinywa cha yule joka, mnyama wa mwituni, na yule nabii wa uwongo, na alisema wazi kwamba maneno hayo “yanaongozwa na roho waovu,” kusudi yawakusanye wafalme wa dunia kwenye vita vya Har-Magedoni.—Ufu 16:13-16.
Hivyo, ni kwa sababu nzuri kwamba Yohana aliwasihi Wakristo ‘wayajaribu maneno yaliyoongozwa na roho ili kuona kama yanatoka kwa Mungu.’ (1Yo 4:1-3; linganisha Ufu 22:6.) Alionyesha pia kwamba maneno ya kweli ya Mungu yaliyoongozwa na roho yalipitishwa kupitia kutaniko la Kikristo la kweli, si kupitia vyanzo vya ulimwengu visivyo vya Kikristo. Bila shaka, maneno ya Yohana yaliongozwa na roho ya Yehova Mungu, lakini mbali tu na hilo, barua ya Yohana ilikuwa imeweka msingi imara wa kusema maneno haya ya wazi: “Yeyote anayemjua Mungu hutusikiliza; yeyote ambaye hatokani na Mungu hatusikilizi. Hivi ndivyo tunavyolitofautisha neno la kweli lililoongozwa na roho na neno lenye kosa lililoongozwa na roho.” (1Yo 4:6) Mbali na kuwa mshupavu, Yohana alionyesha kwamba yeye na Wakristo wengine wa kweli, walikuwa wakionyesha tunda la roho ya Mungu, hasa upendo, na walikuwa wakithibitisha kwa mwenendo wao mzuri na maneno ya kweli kwamba walikuwa ‘wakitembea katika kweli’ kwa muungano na Mungu.—1Yo 1:5-7; 2:3-6, 9-11, 15-17, 29; 3:1, 2, 6, 9-18, 23, 24; tofautisha na Tit 1:16.
JULAI 22-28
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | 1 TIMOTHEO 1-3
“Jitahidi Kufikia Kazi Njema”
km 9/78 4 ¶7
Wale ‘Wanaojipatia Sifa Nzuri’
7 Ni rahisi kuona kwa nini Paulo alisema kwamba wanaume kama hao “wanajipatia sifa nzuri.” Hilo halimaanishi wanapandishwa cheo kanisani, kama wengine wanavyodai. Badala yake, watumishi wa huduma “wanaohudumu vizuri” wanahakikishiwa watapata baraka kutoka kwa Yehova na Yesu, na wanaheshimiwa na kuungwa mkono na kutaniko lote. Kwa sababu hiyo wanapata “uhuru mwingi wa kusema katika imani iliyo katika Kristo Yesu.” Kwa kuwa wanatimiza mgawo wao vizuri, wanathaminiwa kwa sababu ya utumishi wao mzuri; wao ni imara katika imani na wanaweza kutangaza imani yao bila hofu au kuogopa kuaibishwa.
Kutafuta Hazina za Kiroho
it-1 914-915
Ukoo
Hakukuwa na faida kuchunguza na kuzungumzia mambo hayo, na hilo lilikuwa kweli hasa wakati ambapo Paulo alimwandikia Timotheo. Haikuwa muhimu kudumisha rekodi za ukoo ili kuthibitisha mtu alizaliwa katika familia gani, kwa kuwa sasa katika kutaniko la Kikristo Mungu hakuona ikiwa kuna tofauti yoyote kati ya Myahudi na Mtu wa Mataifa. (Gal 3:28) Na tayari rekodi za ukoo zilikuwa zimethibitisha kwamba Kristo alikuja kutokana na ukoo wa Daudi. Pia, muda mfupi baada ya Paulo kuandika himizo hilo Yerusalemu liliharibiwa, pamoja na rekodi za Wayahudi. Mungu hakuzihifadhi. Hivyo, Paulo alihangaikia sana kwamba Timotheo na makutaniko yasikengeushwe yatumie muda mwingi yakifanya utafiti na kubishana kuhusu mambo yasiyo na maana kama kuchunguza mtu alizaliwa katika familia gani, na mambo hayo hayakuchangia chochote katika imani ya Kikristo. Ukoo unaotajwa katika Biblia unatosha kuthibitisha kwamba Kristo alikuwa Masihi, na huo ndio ukoo muhimu zaidi kwa Wakristo. Orodha nyingine za ukoo zilizo katika Biblia zinathibitisha kwamba rekodi ya Maandiko ni sahihi kabisa, na hivyo kuthibitisha kwamba ni simulizi halisi la kihistoria.
JULAI 29–AGOSTI 4
Kutafuta Hazina za Kiroho
it-2 714 ¶1-2
Kusoma Mbele ya Watu
Katika Kutaniko la Kikristo. Katika karne ya kwanza, ni watu wachache sana waliokuwa na nakala ya vitabu vingi vya kukunjwa vilivyofanyiza Biblia, kwa hiyo, kusoma mbele ya watu kulikuwa muhimu sana. Mtume Paulo aliamuru kwamba barua zake zisomwe mbele ya watu katika makutaniko ya Kikristo na akaagiza kwamba makutaniko yabadilishane barua hizo ili zisomwe katika makutaniko hayo pia. (Kol 4:16; 1Th 5:27) Paulo alimshauri kijana Timotheo aliyekuwa mwangalizi kijana atie jitihada katika “kusoma mbele ya watu, kuhimiza, na kufundisha.”—1Ti 4:13.
Mtu anayesoma mbele ya watu anapaswa kusoma kwa ufasaha. (Hab 2:2) Kwa kuwa kusudi la kusoma mbele ya watu ni kuwaelimisha, msomaji anapaswa kufahamu kabisa kile anachosoma na aelewe waziwazi kusudi la mwandikaji, akiwa mwangalifu kwamba anaposoma asiwape wasikilizaji maoni au mawazo yasiyofaa. Kulingana na Ufunuo 1:3, wale wanaosoma unabii huo kwa sauti, na wale wanaosikia maneno yake na kuyashika, watakuwa wenye furaha.