Marejeo ya Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha
© 2024 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
SEPTEMBA 2-8
HAZINA ZA NENO LA MUNGU ZABURI 79-81
Hazina za Kiroho
it-2 111
Yosefu
Jina Yosefu Linatukuzwa. Kwa sababu ya cheo kikubwa ambacho Yosefu alikuwa nacho miongoni mwa wana wa Yakobo, inafaa sana kwamba nyakati fulani jina lake lilitumiwa kuwakilisha makabila ya Israeli (Zb 80:1) au makabila yaliyokuja kuwa sehemu ya ufalme wa kaskazini. (Zb 78:67; Amo 5:6, 15; 6:6) Pia, jina lake linapatikana katika unabii wa Biblia. Katika maono ya kinabii ya Ezekieli, urithi wa Yosefu ni wa sehemu mbili (Eze 47:13), moja ya malango ya jiji linaloitwa “Yehova Yupo Hapo” lina jina la Yosefu (Eze 48:32, 35), na kuhusu kuunganishwa kwa watu wa Yehova, Yosefu anasemwa kuwa mkuu wa sehemu moja na Yuda kuwa mkuu wa sehemu nyingine. (Eze 37:15-26) Unabii wa Obadia ulionyesha kwamba “nyumba ya Yosefu” ingeshiriki katika kuangamizwa kwa “nyumba ya Esau” (Ob 18), na unabii wa Zekaria ulionyesha kwamba Yehova angeiokoa “nyumba ya Yosefu.” (Zek 10:6) Jina la Yosefu linatokea kwenye orodha ya makabila ya Israeli la kiroho, badala ya Efraimu.—Ufu 7:8.
Kwa Yosefu kutiwa katika orodha ya Ufunuo 7:8 kunaonyesha kwamba unabii ambao Yakobo alitoa kabla ya kufa ungekuwa na utimizo katika Israeli la kiroho. Hivyo, inafaa kuzingatia kwamba Mwenye Nguvu wa Yakobo, Yehova Mungu, alimtoa Kristo Yesu kuwa Mchungaji Mwema aliyekufa kwa ajili ya “kondoo.” (Yoh 10:11-16) Pia, Kristo Yesu ndiye jiwe la msingi la pembeni ambalo juu yake hekalu la Mungu lililofanyizwa na Waisraeli wa kiroho limejengwa. (Efe 2:20-22; 1Pe 2:4-6) Jiwe hilo na Mchungaji huyo yupo pamoja na Mungu Mweza-Yote.—Yoh 1:1-3; Mdo 7:56; Ebr 10:12; linganisha Mwa 49:24, 25.
SEPTEMBA 9-15
HAZINA ZA NENO LA MUNGU ZABURI 82-84
Hazina za Kiroho
it-1 816
Yatima
Kwa kuwa ilikuwa rahisi kuacha kuwafikiria watoto hao waliofiwa na wasio na ulinzi, Yehova alituma neno “yatima” kufafanua kiwango ambacho taifa la Israeli lilikuwa limeacha kufuatia uadilifu. Taifa hilo lilipokuwa na afya nzuri kiroho, mayatima walitunzwa. Haki ilipopotoshwa nchini humo, mayatima walipuuzwa, na hiyo ilikuwa dalili ya kuzorota kwa taifa lote. (Zb 82:3; 94:6; Isa 1:17, 23; Yer 7:5-7; 22:3; Eze 22:7; Zek 7:9-11; Mal 3:5) Yehova aliwalaani wale waliowakandamiza mayatima. (Kum 27:19; Isa 10:1, 2) Yehova anajifafanua kuwa Mtetezi (Met 23:10, 11), Msaidizi (Zb 10:14), na Baba (Zb 68:5) wa mayatima. Yeye ndiye anayetekeleza hukumu kwa niaba yao (Kum 10:17, 18), anawaonyesha huruma (Ho 14:3), anawapa kitulizo (Zb 146:9), na kuwahifadhi hai.—Yer 49:11.
Mojawapo ya mambo yanayoutambulisha Ukristo wa kweli ni kuwaonyesha ufikirio wajane au mayatima. Mwanafunzi Yakobo aliwaandikia Wakristo hivi: “Namna ya ibada iliyo safi na isiyo na unajisi kwa maoni ya Mungu wetu na Baba ni hii: kuwatunza mayatima na wajane katika dhiki yao, na kuendelea kujitunza bila doa kutokana na ulimwengu.”—Yak 1:27.
SEPTEMBA 16-22
HAZINA ZA NENO LA MUNGU ZABURI 85-87
Hazina za Kiroho
it-1 1058 ¶5
Moyo
Kutumikia kwa “Moyo Kamili.” Moyo halisi unapaswa kuwa kamili ili utende kwa njia ya kawaida, lakini moyo wa mfano unaweza kugawanyika. Daudi alisali hivi: “Unganisha moyo wangu ili niliogope jina lako,” akidokeza kwamba moyo wa mtu unaweza kugawanyika kwa kutegemea mambo yanayompendeza au anayoogopa. (Zb 86:11) Mtu kama huyo anaweza kuwa na “moyo nusunusu,” yaani, kumwabudu Mungu akiwa vuguvugu. (Zb 119:113; Ufu 3:16) Pia, mtu anaweza kuwa na “mioyo miwili” (kihalisi, kwa moyo na moyo), kwa kujaribu kuwatumikia mabwana wawili, au kwa kusema jambo moja kwa udanganyifu huku akifikiria jambo lingine. (1Nya 12:33; Zb 12:2, maelezo ya chini) Yesu alishutumu vikali unafiki huo wa kuwa na mioyo miwili.—Mt 15:7, 8.
OKTOBA 14-20
HAZINA ZA NENO LA MUNGU ZABURI 96-99
Hazina za Kiroho
it-2 994
Wimbo
Maneno “wimbo mpya” hayapatikani tu kwenye Zaburi bali yanapatikana pia katika maandishi ya Isaya na ya mtume Yohana. (Zb 33:3; 40:3; 96:1; 98:1; 144:9; 149:1; Isa 42:10; Ufu 5:9; 14:3) Muktadha wa sehemu nyingi ambapo maneno “wimbo mpya” yanapatikana unaonyesha kwamba wimbo huo uliimbwa kwa sababu ya matukio mapya yanayohusu njia ambayo Yehova anatumia mamlaka yake akiwa mwenye enzi kuu ya ulimwengu wote. Kwenye Zaburi 96:10 tangazo hili linatolewa kwa shangwe: “Yehova amekuwa Mfalme!” Inaonekana kwamba matukio mapya katika upanuzi wa ufalme wa Yehova, kutia ndani jinsi matukio hayo yanavyoathiri mbingu na dunia, ndiyo mada kuu ya huo “wimbo mpya.”—Zb 96:11-13; 98:9; Isa 42:10, 13.
OKTOBA 21-27
HAZINA ZA NENO LA MUNGU ZABURI 100-102
Hazina za Kiroho
it-2 596
Mwari
Mwari anaposhiba chakula, mara nyingi anaruka hadi mahali ambapo atakuwa peke yake, kisha anasimama kana kwamba ana huzuni kwa kuzamisha kichwa chake ndani ya mabega yake na kusimama bila kusonga, hivi kwamba kwa mbali anaonekana kama jiwe jeupe. Ndege huyo anaweza kusimama hivyo kwa saa nyingi, na kwa sababu hiyo inafaa kwamba mtunga-zaburi alirejelea huzuni yake iliyomfanya asiwe mtendaji alipoandika hivi: “Mimi ni kama mwari wa nyikani.” (Zb 102:6) Katika mstari huu huenda neno “nyikani” halirejelei jangwani, bali eneo ambalo liko mbali na mahali ambapo wanadamu wanaishi, labda kwenye kinamasi. Katika misimu fulani, mwari waliishi katika vinamasi vilivyokuwa kaskazini mwa Bonde la Yordani. Kuna aina tatu za mwari wanaopatikana katika Israeli. Anayepatikana kwa wingi ni mwari mweupe wa mashariki (Pelecanus onocrotalus). Mwari aina ya Dalmatian (Pelecanus crispus) na mwari aliye na mgongo wa waridi (Pelecanus rufescens) huonekana mara chache zaidi.
Mwari hupenda zaidi kukaa katika maeneo ambako hakuna mashamba, na ambako hawezi kusumbuliwa na wanadamu. Anajenga kiota huko, kutaga mayai, kuangua makinda yake, na kupeleka samaki wake huko baada ya kuvua. Kwa kuwa ndege huyo anapenda sana kuwa katika mahali penye upweke na ukiwa, Biblia humtumia kuwakilisha uharibifu kamili. Ili kuonyesha kwamba Edomu lingeharibiwa, Isaya alitabiri kwamba mwari angemiliki nchi hiyo. (Isa 34:11) Sefania alitabiri kwamba mwari wangeishi kwenye nguzo za Ninawi, kuonyesha kwamba jiji hilo lingeangamizwa kabisa na hakuna wanadamu ambao wangeishi humo.—Sef 2:13, 14.