Kwa Nini Kuna Chuki Sana?
Kwa nini ulimwengu umejaa chuki? Ili kujua sababu, tunahitaji kuelewa chuki ni nini, kwa nini watu husitawisha chuki, na jinsi inavyosambaa.
Chuki Ni Nini?
Chuki ni uadui au hisia zenye nguvu sana za kutopendezwa na mtu au kikundi cha watu. Ni hisia ya uchungu na hasira inayodumu kwa muda mrefu.
KWA NINI WATU HUSITAWISHA CHUKI?
Watu husitawisha chuki kwa sababu mbalimbali. Mara nyingi watu huchukiwa si kwa sababu ya mambo wanayofanya, bali kwa sababu ya jamii yao. Wale wanaochukiwa wanaonekana kuwa waovu, wanaokusudia kuwadhuru wengine, au wasioweza kubadilika. Wanaweza kuonekana kuwa watu wasiofaa, tishio, au chanzo cha matatizo. Huenda wale wanaowachukia wengine wakafanya hivyo kwa sababu walitendewa kwa jeuri, isivyo haki, au jambo lingine lililofanya wasitawishe hisia hizo za uadui.
JINSI CHUKI INAVYOSAMBAA
Mtu anaweza kuwachukia wengine hata ingawa hajawahi kuonana nao. Kwa mfano, mtu anaweza kufuata maoni ya kibaguzi ya mtu wa karibu na anayemheshimu. Hivyo, mtazamo wa chuki unaweza kusambaa kwa urahisi katika kikundi fulani cha watu na kufanya kila mtu awe na maoni hayo.
Tunapoelewa jinsi chuki inavyoweza kusambaa kwa urahisi, tunaweza kuelewa kwa nini watu wengi wana chuki. Hata hivyo, ili kushinda chuki iliyojaa ulimwenguni, lazima tujue chanzo chake. Chanzo chake kimefunuliwa waziwazi kwenye Biblia.
BIBLIA INAFUNUA CHANZO CHA CHUKI
CHUKI HAIKUANZISHWA NA WANADAMU. Chuki ilianza wakati malaika mmoja mbinguni, aliyekuja kuitwa Shetani Ibilisi, alipomwasi Mungu. Ibilisi “alikuwa muuaji alipoanza” uasi. Kwa kuwa “ni mwongo na ndiye baba ya uwongo,” ameendelea kuchochea chuki na ghadhabu. (Yohana 8:44; 1 Yohana 3:11, 12) Biblia inamtaja kuwa mwovu, mwenye hasira, na ghadhabu.—Ayubu 2:7; Ufunuo 12:9, 12, 17.
NI RAHISI KWA WANADAMU WASIO WAKAMILIFU KUWA NA CHUKI. Mwanadamu wa kwanza, Adamu, alifuata mwelekeo wa dhambi wa Shetani. Hivyo, wanadamu wote wamerithi dhambi na kutokamilika. (Waroma 5:12) Kaini, mtoto wa kwanza wa Adamu, alimuua ndugu yake, Abeli, kwa sababu ya chuki. (1 Yohana 3:12) Ni kweli kwamba wanadamu wengi wana upendo na huruma. Lakini kwa sababu ya dhambi tuliyorithi, watu wengi ni wabinafsi, wana wivu, na kiburi—sifa zinazochochea chuki.—2 Timotheo 3:1-5.
WATU HUCHUKIA WALE WALIO TOFAUTI NAO. Ulimwengu hufanya watu wachukiane kwa kuchochea mitazamo na matendo yasiyo na huruma na yenye madhara. Mambo kama vile kutopendezwa na watu walio tofauti, ubaguzi, maneno machafu, unyanyasaji, na uharibifu wa mali za watu, yanaongezeka kwa sababu “ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu,” Shetani Ibilisi.—1 Yohana 5:19.
Hata hivyo, Biblia inataja mengi zaidi ya kufunua chanzo cha chuki. Pia, inataja suluhisho.