Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g90 3/8 kur. 24-25
  • Je! Ibada ya Mababu Waliokufa Yawapasa Wakristo?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Ibada ya Mababu Waliokufa Yawapasa Wakristo?
  • Amkeni!—1990
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ibada ya Mababu Hutegemea Msingi Gani?
  • Kuna Tumaini Gani kwa Mababu Waliokufa?
  • Ibada ya Mababu
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
  • Je, Uhofu Wafu?
    Amkeni!—1996
  • Wazazi Wetu wa Kale Wako Wapi?
    Je, Umeipata Barabara Inayoongoza Kwenye Uhai wa Milele?
  • Je, Wafu Wapasa Kuheshimiwa?
    Amkeni!—1999
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1990
g90 3/8 kur. 24-25

Maoni ya Biblia

Je! Ibada ya Mababu Waliokufa Yawapasa Wakristo?

WATU walio wengi wajua kwamba ibada ya mababu waliokufa yahusika sana katika maisha za mamilioni ya watu, hasa wafuasi wa Dini ya Konfyushasi, wafuasi wa Dini ya Buddha, na wafuasi wa Dini ya Shinto. Lakini je! wewe ulijua kwamba ibada ya mababu waliokufa yafungamana na maisha ya Kiafrika pia? Kwa kweli, nyuzi za ibada ya mababu waliokufa zaweza kuonwa katika karibu dini zote, labda hata katika yako. Ni “hali ya ulimwenguni pote,” asema profesa mmoja Mnaijeria wa uchunguzi wa mambo ya kidini.

Ni nini ibada ya mababu waliokufa? Labda uelewevu wako kuihusu wakubaliana na uelezaji huu: “Desturi za ibada ya kutuliza watu wa ukoo waliokufa na kuwaomba msaada, zikitegemea imani ya kwamba roho [za wafu] huongoza ajali ya mwisho itakayowapata walio hai.”—The Concise Columbia Encyclopedia.

Hivyo, katika nyumba ya mfuasi mwenye kujitolea sana ibada ya mababu waliokufa—kwa kielelezo, mfuasi wa Buddha mwenye kuishi katika Esia ya Kusini-mashariki, huenda ukaona madhabahu ndogo ikiwa imewekelewa picha yenye kuonekana wazi sana ya mtu wa ukoo aliyekufa. Hapa pia huenda ukanusa harufu ya uvumba wenye kufukizwa au ukasikia sala zikisemwa-semwa na mikono ikipigwa-pigwa. Mara nyingi, wenye kujitoa sana huweka chakula au hupanga maua juu ya madhabahu hiyo kwa manufaa ya mfu wa ukoo wao.

Hamia kontinenti nyingine, nawe utapata kwamba Waafrika wengi “huishi pamoja na wafu wao.” Katika sehemu ya Afrika iliyo chini ya Sahara imani ya ujumla ni kwamba yawezekana kuwa na ushirika na uwasiliano kati ya wale walio hai na waliokufa. “Sisi sote Waafrika twahisi kwamba wazazi wetu waliokufa na mababu wengine wako karibu nasi,” asema mwanatheolojia Mwafrika aliye mashuhuri wa imani ya Kiprotestanti.

Katika sehemu kubwa ya Afrika, mababu waliokufa wangali wachukuliwa kuwa ndio vichwa vya jamaa au jumuiya walizokuwamo walipokuwa hai. Wao wabakia wakiwa ndio “wasimamizi wa kiroho wa mambo ya jamaa,” asema Profesa E. Bọlaji Idowu, katika kitabu chake African Traditional Religion—A Definition. Roho ya babu waliokufa yaweza kuombwa iwape watu au iwaepushe na karibu kitu chochote kile. Hivyo, mababu waliokufa huchukuliwa kuwa ndio “wasababishi wa ufungamano katika jamii ya Kiafrika,” na kulingana na The New Encyclopædia Britannica, kuwaonyesha kicho kingi huendeleza “uthabiti wa kijamaa.”

Katika mabara ya Magharibi—kama Ufaransa au Kanada—makanisa, vikanisa, au maabadi huwekwa wakfu kwa watakatifu, ambao wangeweza kuitwa mababu wafu walio mashujaa. Sala zitokazo kwenye midomo ya wenye kujitoa sana husemwa-semwa mbele ya sanamu zilizo kimya. Au wakiwa wamepiga magoti kwa kunyoosha mikono, wenye kujitoa sana huzipa zawadi aikoni zilizopakwa dhahabu. Ni kweli kwamba wafuasi wa dini za Jumuiya ya Wakristo wangeshtuka wachukizwe sana kwa kuambiwa kwamba ujitoaji ambao wao huonyesha ni ibada ya mababu waliokufa; lakini mfuasi wa Dini ya Buddha, mfuasi wa Dini ya Shinto, au Mwafrika mwenye kujitoa sana hutabasamu aambiwapo hivyo. Yeye ajua kwamba kicho chenye kuonyeshwa na “Wakristo” hawa si tofauti sana na vitendo vyake mwenyewe vya kicho cha ibada.

Ibada ya Mababu Hutegemea Msingi Gani?

Kiini cha ibada ya mababu ni ile imani ya kwamba kupitia kitu fulani kisichokufa cha utu wa kibinadamu, wafu huendelea kuwako. Hiyo ni “imani katika kutokufa kwa nafsi,” kulingana na Damian Lwasa aliye mwandikaji Mkatoliki wa Uganda. Msingi wa imani hiyo ni imara kadiri gani? Harry Sawyerr aliye mwanatheolojia Msierra Leone akiri kwamba Waafrika wenye kudai “kwamba mababu wao waliokufa wako hai katika roho hufanya hivyo bila ushuhuda wowote thabiti.”

Kwa kweli, kulingana na Biblia, hakuna sehemu yoyote ya kiroho ya mtu ambayo huendelea kuwa hai baada ya kufa kwa mwili. Muumba mwenyewe asema hivi: “Tazama! Nafsi zote—ni zangu mimi. Kama vile nafsi ya baba kadhalika na nafsi ya mwana—ni zangu mimi. Ile nafsi inayofanya dhambi—hiyo yenyewe ndiyo itakayokufa.” (Ezekieli 18:4, NW) Wanasayansi na wanatiba hawajapata ushuhuda wowote wa sehemu yoyote ya wanadamu ambayo huendelea kuwa hai ikiwa na fahamu baada ya kufa kwa mwili.

Muda mrefu kabla ya Confucius au Buddha, mwanamume mwenye hekima wa nyakati zilizotangulia Ukristo aliandika hivi: “Walio hai wanajua ya kwamba watakufa; lakini wafu hawajui neno lo lote.” (Mhubiri 9:5) Mapema kidogo, Ayubu alisema hivi: “Mwanadamu wa duniani hutokwa na pumzi, naye yuko wapi? Wanaye hupata kuheshimiwa, lakini yeye hajui hilo.” (Ayubu 14:10, 21, NW) Hivyo, wafu hawawezi kutumikia wakiwa ‘wasimamizi wa kiroho wa mambo ya jamaa.’ Wakati wa kufa mtu ‘hawezi kuchukua chochote hata kidogo ili aende nacho.’—Zaburi 49:10, 17-19, NW.

Fikiria hili: Je! mababu waliokufa hula chakula kizuri watolewacho? Je! ule uhakika wa kwamba chakula kile hubaki bila kuguswa hauonyeshi kwamba wafu wako hoi? Zaidi ya hilo, mababu waliokufa hawawezi kuwa na habari juu ya kicho kingi au dhabihu ambazo zatolewa na wajukuu walio hai. Kwa kuwa hawako, wao hawawezi kupendezwa na jamaa yao ya hapo kwanza wala kujiingiza katika mambo yayo. Biblia yasema hivi: “Hawana sehemu tena katika jambo lo lote lililofanyika chini ya jua.”—Mhubiri 9:6.

Kuna Tumaini Gani kwa Mababu Waliokufa?

Basi, je! hii yamaanisha kwamba hakuna tumaini la kuunganishwa tena na wapendwa waliokufa? Sivyo hata kidogo! Watu waliotenganishwa na kifo muda mrefu uliopita wataungamanishwa tena waletwapo kwenye uhai katika ufufuo. “Saa inakuja,” Yesu aahidi katika Biblia, “ambamo wote wale walio katika makaburi ya ukumbusho watasikia sauti yake na watoke.”—Yohana 5:28, 29, NW.

Tumaini hili la ufufuo lilisaidia kufanyiza upya maisha ya mwanamke mmoja wa Okinawa aliyeabudu mababu wake waliokufa. Yeye aeleza hivi: ‘Maoni yangu juu ya maisha yalibadilika. Kuwa mfuasi wa Yesu Kristo kumenisaidia niwe mwenye upendo zaidi kwa watu wa ukoo wangu walio hai na kwa wengine.’ Je! kupenda wazazi walio hai silo jambo la kiakili kuliko kicho kingi kwa mababu waliokufa? (Waefeso 6:2, 3) Yeye aendelea kusema: ‘Nionapo upweke wa wazazi na mababu na manyanya wenye kuzeeka leo, mimi nashukuru sana kwamba nilijifunza kuwaonyesha wazazi wangu upendo na staha halisi walipokuwa wangali hai.’

Kwa kuongezea, jambo zito zaidi lenye kufanya Wakristo wakatae ibada ya mababu waliokufa ni kwamba hiyo yawakilisha mwendo wa kuasi dhidi ya amri ya Mungu iliyo wazi: “Usiwe na miungu mingine ila mimi . . . kwa kuwa mimi, BWANA [Yehova, NW], Mungu wako, ni Mungu mwenye wivu [mwenye kutoza ujitoaji wa pekee, NW].” (Kutoka 20:3, 5) Kwa hiyo badala ya kuabudu watu wa ukoo waliokufa, tii shauri la Biblia la kuabudu Yehova, yule Mmoja tu mwenye uwezo wa kuwezesha kuwe na kuunganika upya kwenye shangwe pamoja na watu wa ukoo waliokufa.—Ufunuo 20:12, 13.

[Blabu katika ukurasa wa 24]

“Lakini wafu hawajui neno lo lote.”—Mhubiri 9:5

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki