Kulalwa Kinguvu— Alilindwa na Aliyosoma
WEWE ufanye nini ukikabiliwa na mlala-wanawake-kinguvu? Kuna ushauri wenye kugongana. Watu fulani hudai kwamba ukinzani humchochea zaidi tu mshambulizi, na bado Biblia yaonyesha mwanamke apaswa kukinza. (Kumbukumbu 22:23-27) Ushauri bora zaidi ni nini?
Uchunguzi mpya uliotangazwa katika toleo la Januari la The American Journal of Public Health wadokeza ukinzani. Makala yasema hivi: “Utafiti wa mambo yaliyoonwa wajumlika kuunga mkono kukata shauri moja la maana: kukinza hupunguza uyamkini wa kukamilishwa kwa ushambulizi.” Lililopata mwanamke mmoja Septemba uliopita katika Japani latoa kielezi cha jambo hilo. Alikuwa ametoka tu kurudi nyumbani kwake usiku sana, ambapo yeye huishi peke yake. Yeye afafanua hivi:
“Mlala-wanawake-kinguvu aliingia ndani ya nyumba yangu akafunga mlango. Kwa sababu ya kughafilikiwa na kutetemeka sana, niliduwaa kabisa. Mwanamume huyo alijaribu kunivuta chumbani, lakini mimi nikashika sana nguzo na kumkinza.
“Hapo ndipo nilikumbuka andiko katika Kumbukumbu sura ya 22. Lasema kwamba ikiwa mwanamke hapaazi kilio ashambuliwapo, yaonyesha anamruhusu mwanamume na anatenda dhambi dhidi ya Yehova. Pia, nilikumbuka niliyosoma katika makala ya Amkeni! ‘Kuingilia Wanawake Kinguvu—Wewe Waweza Kujilindaje?’—Oktoba 8, 1980, chapa ya Kijapani; Machi 1981, chapa ya Kiswahili.
“Haya basi, mimi niliwaza hivi: ‘Ni lazima nipige ukelele na kumkinza kwa ustahiki wangu wote.’ Kwa hiyo nikapaaza sauti: ‘Yehova, nisaidie!’ tena na tena na kuendelea kuinua sauti. Mlala-wanawake-kinguvu alipovuta mikono yangu kuelekea kulia, mimi niliivuta kuelekea kushoto. Aliponivuta mbele, mimi nilijivuta nyuma, na aliponifunika kinywa ili ajaribu kunikomesha kupiga kelele, nilimwuma. Vyovyote vile, niliendelea kumkinza.
“Naamini kwamba niliweza kuepuka kulalwa kinguvu kwa sababu ya msaada wa Yehova na kwa sababu ya kutumia niliyokuwa nimesoma katika Amkeni! Kama nisingalikuwa nimesoma makala hiyo ya Amkeni!, nafikiri kwamba kwa sababu ya hofu ningalinyamaza na yaelekea ningalifanya vile hasa mhalifu huyo alivyosema. Asanteni sana sana.”