Vijana Wauliza . . .
Kwa Nini Wazazi Wangu Wananitia Aibu?
Katikati kabisa ya darasa la bayolojia, unaanza kujisikia ukiwa mgonjwa. Kwa njia yenye kukukatisha tamaa, shule inapiga simu nyumbani, na baada ya muda mfupi mama yako anakuja—amevaa viatu vya kuogea, vikunja-nywele vya rangi nyekundu-nyeupe, na ile suruali nyekundu yenye sura mbaya ambayo yeye huwa anavaa akiwa nyumbani. Kwa kusadiki kwamba wewe una shida sana, amefanya haraka kuja kando yako bila kujali sura yake. Lakini wewe huthamini sana jitihada zake za kuja kukuokoa. Jambo moja tu unalofikiria ni jinsi mama yako anavyoonekana mjinga na mzembe katika mavazi yake. Naye anapoanza kukuhangaikia sana mbele ya wanadarasa wenzako, unaona ni afadhali ungeweza kupotea kabisa. Umeaibika sana!
VISA kama hiki huenda vikaonekana kuwa vya kuchekesha watazamaji. Lakini wewe hucheki. Unajisikia ukitatizika, mkazo mkubwa sana hivi kwamba unajisikia ingeweza kuwa afadhali ufe. Kwa kweli, usemi uliungwa kutokana na jambo hilo: ‘Kuuawa na aibu.’ Na si wewe wa kwanza kujisikia hivyo. Kwa kielelezo, Wayahudi wa kale waliutambua uwezo wa aibu wenye kuvunja maono ya moyoni. Talmud ya Kiebrania ilionyesha kwamba kutia mtu aibu mbele ya watu ni kama kumwaga damu yake!
Kuna vyanzo vingi vya kuona aibu, lakini vijana wengi wanakubali kwamba hakuna kilicho kikubwa kuliko wazazi wao wenyewe. Orodha ya mambo ambayo wazazi wanaweza kufanya kukutia aibu inaonekana kuwa bila mwisho: kuonyesha shauku mbele ya watu, kujisifu juu ya matimizo yako, kutenda kama watoto mbele ya rafiki zako, kudai kwamba “ujionyeshe” mbele ya wageni. Naam, hata sura ya wazazi wako inaweza kukutia aibu! Basi, si ajabu kwamba vijana fulani wanajikunyata wanapofikiria kuonwa wakiwa pamoja na wazazi wao.
Ingawa hivyo, kwa nini huenda wazazi wako wakakutia aibu sana? ‘Je! hawawezi kufanya afadhali kuliko hivyo?’ huenda ukashangaa.
Kwa Nini Wanakutia Aibu
Acheni tuchanganue maono yako mwenyewe ya ndani katika habari hii. Ukiwa kijana, inakuwa rahisi zaidi wewe kuona aibu, kwa kuwa umezidi kujua kwamba kuna watu wengi zaidi ulimwenguni kuliko jamaa yenu tu. Wewe unataka kukubaliwa na wengine—hasa marika wako—nawe unajaribu sana kutenda “kwa usahihi.” Kiasili, hutaki ukubaliwa huu ubomolewe na mwenendo wa wazazi wako wenye kutia aibu. Kama vile kijana mmoja jina lake Linda alivyosema: ‘Wazazi wako wakifanya jambo linalokutia aibu, unaona wasiwasi: “Rafiki zangu watafikiri nini juu yangu?”’ Basi, kwa nini wazazi wako hawawezi kufikiria zaidi maono yako ya ndani?
Msaikolojia Bernice Berk anasimulia kwamba mama mmoja alimwambia hivi mwana wake mwenye kuudhika upesi sana: “Hiyo ni kazi yangu, kukutia aibu. Mama yangu alinitia aibu, na itakuwa lazima wewe uwatie aibu watoto wako.” Usemi huu wa kutojali una chembe nyingi za ukweli. Hapana, kutiwa aibu si jambo la urithi, bali ni kitu kingine: kutokamilika.
Wazazi ni wasiokamilika. (Warumi 3:23) Hawawezi kutazamiwa wavalie kwa unadhifu kama violezo waonyeshao mitindo ya mavazi, wala si sikuzote wanathibiti kila jambo wasemalo au kutenda, hali moja na wewe. Pia wao wana haki ya kustarehe mara kwa mara na kucheza-cheza. Pindi kwa pindi kutenda kwa njia ya ujana kuliko umri wao—au hata kwa ujinga kabisa—huenda kukawa ni njia yao ya kukabiliana na ongezeko la umri. Bila kujua jambo hili lina tokeo gani juu yako, huenda mama yako akakuaibisha kwa kujaribu hatua za dansi ya karibuni zaidi pamoja na rafiki zako; huenda baba akajaribu kuthibitisha kwamba anaweza kushindana na vijana-matineja katika uwanja wa mpira wa vikapu. Je! hiyo inatia aibu? Labda. Lakini, kwa uhakika, wao hawakuwa na wazo la kukuumiza.
Pia wazazi wako wanafikiria moyoni faida zako zilizo bora, na kwa sababu ya kutokamilika, huenda wakachukua hatua ya kupita kiasi wakati hali njema yako inapoonekana ikitishwa. Kwa kielelezo, Luka mwandikaji wa Biblia anasema juu ya wakati ambapo Yesu mwenye umri wa miaka 12 alipohudhuria Kupitwa katika Yerusalemu pamoja na jamaa yake. Wazazi wake walipokuwa wakirudi nyumbani, waliona kwamba yeye hakuwapo. Walimtafuta kwa bidii ya uendelevu, na “baada ya siku tatu wakamwona hekaluni, ameketi katikati ya waalimu, akiwasikiliza na kuwauliza maswali.” Bila shaka, Yesu alikuwa akionea shangwe maongezi pamoja na wanaume wenye umri mkubwa kuliko yeye. Hata hivyo, mama yake alipokuja hapo, labda kwa kuonekana kabisa na wanaume hao wakuu wa taifa, alisema hivi: “Mwanangu [mtoto, NW] mbona umetutenda hivi? Tazama, baba yako na mimi tulikuwa tukikutafuta kwa huzuni.”—Luka 2:41-48.
Jambo jingine la kufikiria ni kwamba wazazi wako wana matatizo yao wenyewe, mengine yakiwa ni ambayo huenda hata usiyajue. Labda wasiwasi wa kifedha, ugonjwa, au mikazo mingine ndiyo inayofanya wajiendeshe vile.
Mwisho, wazazi walio wengi wanajivunia wazao wao. Wanaona shangwe kuwafanya wajionyeshe. Hata hivyo, hii inaweza kuongoza kwenye aina zote za hali zenye kuudhi, kama vile kuombwa upige piano mbele ya rafiki za mama yako au kulazimika kuvumilia kumsikia baba yako akiambia mtu yeyote atakayesikiliza kwamba wewe ni mtu “mwenye akili” sana!
Kujifunza Kukabiliana
Wazazi wake wanapomtia aibu, kijana mmoja jina lake Tonia anasema, “Uso wangu uliiva kwa haya nyingi.” Ingawa huenda hili likawa itikio la kiasili, kuna njia zenye matokeo zaidi za kukabiliana. Kukumbuka tu mengine ya mambo yaliyotokezwa kufikia hapa huenda kukasaidia kutuliza fadhaiko lako la kwanza. (Mithali 19:11) Pia fikiria madokezo yanayofuata:
Acha Wasiwasi: Hata uwe na wasiwasi wa kadiri gani, labda hiyo haitabadili mambo sana. (Linganisha Mathayo 6:27.) Ingawaje, si wewe mwenye daraka kwa wazazi wako; wewe ni mtu wa kando. ‘Kila mtu atalichukua furushi lake mwenyewe,” inasema Wagalatia 6:5. Zaidi ya hilo, labda tatizo lako si baya kadiri unavyowazia. Dakt. Joyce L. Vedral anaonelea kwamba ‘kila kijana-tineja mwenye kutiwa aibu anawazia kwamba kuna wasikilizaji wanaomtazama.’ Hata hivyo, watu walio wengi hawapendezwi kwa kadiri hiyo. Vedral anaongezea hivi: “Watu walio wengi wanahangaikia zaidi kipele kilicho juu ya pua yao kuliko vile wanavyohangaikia historia ya jamaa yenu nzima.” Kumbuka, pia, kwamba marika wako pia wana mambo ya kuwatia wasiwasi juu ya maoni ambayo wazazi wao wanafanya watu wawe nayo!
Usifanye Hali Mbaya Iwe Mbaya Zaidi: Inasema hivi Mithali 27:12: “Mwenye busara anaona matata yanakuja na kulala chini.” (The New English Bible) Kuvuta uangalifu kwako mwenyewe kwa kupaaza sauti, ‘Ah, ewe Mama!’ kunaongezea tu hali ile. “Kulala chini” kwa kutosema lolote huenda kukawa jambo la hekima.—Mhubiri 3:7.
Kubali Nidhamu Inayohitajiwa: Sahihisho mbele ya watu huenda likakuaibisha. Lakini mara nyingi nidhamu ile inastahiliwa, na ile aibu ni sehemu yake tu. (Waebrania 12:11) Namna gani ikiwa nidhamu hiyo inaonekana kuwa isiyohitajiwa? Kumbuka jinsi Yesu alivyoshughulika na katizo la mama yake. Alibaki mtulivu na kueleza hali yake. Kwa kweli, Biblia inasema ‘aliendelea kujitiisha’ kwa wazazi wake. (Luka 2:49, 51, NW) Kwa nini wewe usijaribu kufanya ivyo hivyo?
Ongea na Wazazi Wako: Waambie kwa fadhili na kwa heshima ni jambo gani hasa linalokuhangaisha. Kufanya hivyo kunafanya kazi! Rosalee aliona katika kisa chake kwamba “ukiwaambia vile unavyojisikia, na wakiona kwamba ni jambo linalofaa, basi kwa kawaida watajaribu kujisahihisha.” Njia moja ya kusaidia wazazi wako waone upande wako wa suala hilo ni kuwauliza ni mambo gani ya kuaibisha yaliyowapata walipokuwa vijana zaidi. Huenda hiyo ikawafanya wafikirie hali yako.
Onyesha Maono ya Kujisikia Kama Wengine: Ebu fikiria nyakati zote ambapo wewe umewatia aibu wazazi wako! Je! ulifanya hivyo kwa nia ya kuumiza? Bila shaka sivyo! Hivyo basi kwa nini ujisikie kwamba wazazi wako wanapanga makusudi njama ya kukutia wewe aibu?
Usipoteze Kamwe Ucheshi Wako: Kama vile kijana-tineja mmoja alivyokubali wazi: “Mambo fulani ni lazima ujaribu kuyachekelea tu; baada ya hapo yanakuwa kama kichekesho tu.” Ndiyo, kwa nini uchukue tukio baya kwa uzito sana? Kumbuka, kuna “wakati wa kucheka,” na nyakati fulani kuonyesha ucheshi kunaondoa lile umivu la kutiwa aibu.—Mhubiri 3:4.
Lakini, hata ujaribu namna gani, huwezi kuepuka kabisa kutiwa aibu. Lakini kwa kutumia yaliyotangulia, huenda hata ukaweza kubadili maoni yako juu ya zile zinazoitwa hali zenye kutia aibu.
Kwa kielelezo, mtungaji Jami Bernard anasimulia hivi: “Sikuzote mama yangu alinifanya nimshike mkono tulipovuka barabara, hata nilipokuwa na umri mkubwa zaidi. Siku moja, nilivuta mkono wake nikauondoa, nikiminya sauti kwa kunung’unika, ‘Mama, mimi sihitaji mambo haya tena.’ Yeye alinigeukia akasema, ‘Mimi nayahitaji.’ Sijui kama alimaanisha kwamba alihitaji mtu fulani wa kuegemea au kwamba aliutamani sana wakati ambapo nilikuwa ‘kitoto’ chake au kwamba alitaka kugusana na mimi lakini asijue hasa jinsi ya kufanya hivyo. Lakini sasa ninaposhika mkono wake ili kuvuka barabara, ninapata msisimuko wenye ujoto—si wa kutiwa aibu bali wa upendo.”—Gazeti Seventeen, Desemba 1985.