Wakaaji wa Nje ya Dunia Hii—Ndoto ya Tangu Kale
WAANDIKAJI wa ki-siku-hizi wa hadithi-ubuni za kisayansi sio waliovumbua lile wazo la kuwako kwa wakaaji wa nje ya dunia hii. Karne kama 23 zilizopita, mwanafalsafa Mgiriki jina lake Metrodorus alifundisha kwamba haielekei kuwa kuna ulimwengu mzima wenye dunia moja tu inayokaliwa kama vile shamba kubwa lisivyokuwa na suke moja tu la mhindi. Lucretius, mshairi Mroma wa karne ya kwanza K.W.K., aliandika kwamba “katika sehemu nyingi za anga kuna madunia mengine na jamii mbalimbali za wanadamu.”
Fundisho hili, liitwalo wingi wa malimwengu, halikupendelewa katika Jumuiya ya Wakristo kwa karne nyingi. Lakini kuanzia karibu 1700 hadi sehemu ya mapema ya karne yetu wenyewe, wanaelimu walio wengi, kutia na baadhi ya wanasayansi walio mashuhuri zaidi katika historia, waliamini kwa uthabiti kwamba kuna uhai katika malimwengu mengine. Kwa uhakika, mwelimishaji mmoja wa miaka ya katikati ya 1800 alishambuliwa kotekote alipothubutu kuandika gazeti lenye kukana fundisho hilo.
Watu walionekana kuwa wenye hamu ya kuamini kuna wakaaji wa nje ya dunia hii, hata kwa kutegemea uthibitisho dhaifu kabisa. Katika 1835 mwandishi wa habari za gazeti moja aliandika kwamba wanaanga walikuwa wamevumbua uhai mwezini. Aliandika kwamba wanyama wa ajabu, mimea ya kigeni, na hata watu wadogo wenye mabawa, wenye kupuruka-puruka na kutoa ishara zenye kuonekana, wote hao walionwa kupitia darubini! Gazeti lake liliongezeka mweneo. Wengi waliendelea kuamini hekaya hiyo hata ilipofichuliwa kuwa udanganyifu.
Wanasayansi pia walikuwa na matazamio mazuri. Katika miaka ya mwishoni mwa 1800, mwanaanga Percival Lowell alisadiki kwamba angeweza kuona mfumo tata wa mifereji ikiwa juu ya uso wa sayari Mars. Alichora vizuri ramani yenye habari zote kuihusu na akaandika vitabu juu ya utamaduni uliokuwa umeijenga. Katika Ufaransa, Chuo cha Sayansi Mbalimbali kilikuwa na uhakika sana kwamba kuna uhai katika Mars hivi kwamba kikafanya toleo la kumpa zawadi mtu yeyote ambaye angekuwa wa kwanza kuwasiliana na wowote wa wakaaji wengine wa nje ya dunia hii zaidi ya wakaaji wa Mars.
Watu fulani walipendekeza mipango ya kiajabu-ajabu ya kuwasiliana na wahai walio katika malimwengu ya karibu, kuanzia kuwasha mioto mikubwa katika Jangwa la Sahara hadi kupanda misitu ya maumbo yaliyopangwa kwa vipimo sahihi sana kutoka upande mmoja hadi mwingine wa Siberia. Katika 1899 mvumbuzi Mwamerika alisimamisha mlingoti wenye tufe la shaba juu na kupitisha ndani yao midundo ya kiumeme yenye nguvu ili kuwapa ishara wakaaji wa Mars. Damu iliwachemka watu sana, na mianga ikawaka sehemu zote zenye kuzunguka kwa mwendo wa kilometa 48, lakini hakuna jibu lililotoka Mars.
Kujawa na Tumaini
Ingawa tekinolojia yenye kuzunguka utafutaji wa leo wa uhai katika malimwengu mengine huenda ikawa mpya, jambo moja labakia bila kubadilika: Wanasayansi wangali wana uhakika kwamba ainabinadamu haiko pekee katika kosmosi (ulimwengu wote mzima). Kama vile mwanaanga Otto Wöhrbach alivyoandika katika gazeti la Kijeremani Nürnberger Nachrichten: “Ni vigumu kupata mwanasayansi wa asili ambaye hangesema ndiyo akiulizwa kama kuna uhai nje ya dunia hii.” Gene Bylinsky, mtungaji wa Life in Darwin’s Universe, aliweka wazo hilo hivi: “Siku yoyote sasa, ikiwa wanaanga wa uchunguzi wa kiredio waweza kuaminiwa, ishara fulani kutoka kwenye nyota itamweka ivuke ile nafasi kubwa mno ya anga ili imalize upweke wetu wa kikosmosi.”
Kwa nini wanasayansi wana uhakika sana kwamba kuna uhai katika malimwengu mengine? Tazamio lao huanza na nyota. Ni nyingi sana—maelfu ya mamilioni katika galaksi yetu. Na hapo ndipo kudhania mambo huanza. Haikosi nyingi za nyota hizo zina sayari zenye kuzizunguka, na ni lazima uhai uwe ulisitawi katika baadhi ya malimwengu hayo. Kwa kusababu mambo hivyo, wanaanga wamekisia-kisia kwamba kuna tamaduni nyingi kuanzia maelfu hadi mamilioni mumu humu katika galaksi yetu wenyewe!
Je! Kuna Tofauti Yoyote?
Kuna tofauti gani kama uhai uko au hauko ng’ambo ya Dunia? Ni kwamba, wanayasansi huhishi kwamba lolote la majibu hayo lingekuwa na matokeo makubwa sana juu ya familia ya kibinadamu. Wao husema kwamba kupata habari kwamba ni sisi peke yetu tulio katika ulimwengu wote mzima kungefundisha ainabinadamu kukadiria thamani ya uhai hapa kwa sababu hauna kifani. Kwa upande mwingine, mwanasayansi mmoja aliye mstahiwa asababu kwamba tamaduni za kigeni zingeelekea kuwa zina maendeleo kuliko ule wetu wenyewe kwa mamilioni mengi ya miaka na zingeweza kushirikiana nasi hekima yazo iliyo kubwa sana. Zingeweza kutufundisha sisi kuponya magonjwa yetu, kumaliza uchafuzi, vita, na kufa njaa. Zingeweza hata kutuonyesha jinsi ya kushinda kifo chenyewe!
Kutokuwako magonjwa, vita, kifo—tumaini la aina hiyo ni la maana sana kwa watu katika nyakati zetu zenye msukosuko. Bila shaka ni la maana sana kwako pia. Ingawa hivyo, labda wewe utakubali kwamba ni afadhali kutokuwa na tumaini lolote kuliko kuegemea la bandia. Basi, ni jambo la maana tupate kujua kama wanasayansi wana msingi thabiti wakazaniapo kwamba ulimwengu wote mzima una malimwengu mengi ya wakaaji.
[Blabu katika ukurasa wa 5]
Je! wanasayansi wana msingi thabiti wakazaniapo kwamba ulimwengu wote mzima una malimwengu mengi ya wakaaji?