Je! Wewe Ni Dereva wa Hatari Sana?
Na mleta habari za Amkeni! katika Japan
“SISI tunajua watu wa namna ambayo wataelekea kufanya aksidenti,” akasema Hiroyasu Ohtsuka, Mkuu wa Usalama Barabarani kwenye Taasisi ya Kitaifa ya Sayansi ya Polisi ya Japani. “Hata hivyo, sisi hatukatai kuwapa leseni ya dereva, lakini tunataka watu watambue kasoro zao za utu na wazirekebishe.”
Kwa kawaida madereva walio wa hatari sana hawajifahamu kuwa hivyo. Lakini wastadi wanatambua namna sita za kasoro za utu ambazo zinaweza kwa urahisi kujionyesha wazi wakati mtu anapoenda kwenye usukani. Unapofikiria kila namna, jaribu kujifikiria mwenyewe, na uone wewe ni dereva salama kadiri gani.
Wale Wasiofaa Kijamii
Miongoni mwa wale walio aina za hatari sana kuna wale ambao tabia zao si za kawaida, wale walio na matatizo katika kuhusiana na wengine. Wao ni:
Anayejifikiria Mwenyewe Huyu ndiye mtu anayesisitiza kufanya kila jambo kwa njia yake mwenyewe. Akiwa ameketi kwenye usukani, anafikiri kwamba yeye ni ‘mfalme wa barabarani.’ Anajisikia huru kuweka mwendo wake mwenyewe, anapuuza sheria zozote anazofikiria kuwa si za maana sana, na kujionyesha wakati wowote anapopenda. Anasahau kwamba ni lazima ashirikiane barabara pamoja na madereva wengine wote. Akitenda kwa uamuzi wake mwenyewe na kuchezea hatari, anasababisha aksidenti kwa sababu anashindwa kuzijali hali zinazobadilika daima barabarani na kujirekebisha kupatana nazo.
Asiye na Ushirikiano Dereva asiye na ushirikiano hajali sana jinsi wengine wanavyojisikia, wala haelewi fikira na maoni yao ya ndani. Kwa sababu ya ugumu wake katika kuchukuana na watu, ana mwelekeo wa kuwaepuka. Hii inaonyeshwa katika kukosa adabu barabarani na kukosa uungwana kuelekea madereva wengine—yote hayo mawili yakiwa ni mambo ya hatari sana. Kwa wengine, kujifunza jinsi ya kutendeana vizuri na watu kunaweza kuchukua miaka mingi, na hii ni sababu moja ya kuwako kwa aksidenti nyingi miongoni mwa vijana.
Mtaka Mapambano Ishara moja ya dereva mtaka mapambano, kulingana na kitabu Driving Instruction According to Aptitude (Agizo la Kuendesha Kulingana na Ustadi), ni “kukataa kabisa kuwaachia wengine nafasi wakati dereva huyo anapoamini yeye ndiye mwenye haki ya kutangulia. Yeye hatasamehe makosa madogo ya madereva wengine au watembea-miguu, na hii inaongoza kwenye kupiga kelele, kukatiza vitendo vya wengine, . . . na kupiga-piga honi . . . kwa kulinda haki zake mwenyewe kwa ukali kabisa.” Hata makosa ya kuwaziwa yanaweza kumfanya achokozeke. Ikiwa pia ni mwenye kukasirika haraka, mara nyingi uendeshaji wake utaruka mipaka iliyo ya kiakili.
Wale Wasiofaa Katika Maono ya Moyoni
Halafu kuna wale walio na matatizo ya maono ya moyoni. Hawa ni kutia ndani:
Asiye Imara Hali za kupita kiasi katika maono ya moyoni zinaonyesha tabia ya mtu asiye imara. Yeye ana vipindi vya kufurahi-furahi, kusisimuka, na kushuka moyo. Akiendesha gari akiwa ameshuka moyo, atakosa kuona hatari, na huenda miitikio yake ikawa ya kuchelewa mno kwa uendeshaji salama. Akiendesha akiwa na misisimuko ya maono ya moyoni, huenda akawa mzembe sana. Maonyo anayopewa akiwa katika tabia-moyo hii yanaweza kuamsha wonyesho wa uasi. Jambo lile tu ambalo huenda akatambua kuwa lisilo la kawaida ni mshuko wake wa moyo.
Mwenye Wasiwasi Kupita Kiasi Mara nyingi huyu ni wa ile namna yenye utulivu ambaye anahusika sana kufikiria mawazo yake mwenyewe, akifanya wasiwasi juu ya kila jambo. Anapoendesha, akili yake inavurugana kwa habari zisizo za uendeshaji,” hivi kwamba “ataelekea zaidi kukosa habari za maana au kuzifasiri vibaya,” wakaonelea hivyo wachunguzi Richard E. Mayer na John R. Treat katika uchunguzi mmoja wa madereva walio hatari sana. Dereva mwenye wasiwasi anaweza kubabaika kabisa hata katika hali ambazo si za hatari, kama wakati ambapo lori linakaribia kando yake. Anatazamia mabaya kabisa.
Mwenye Kushtukia Mambo Wa namna hii anatenda kwa haraka. Badala ya kuchukua wakati wa kuhakikisha mambo ya uhakika na kufanya uamuzi sahihi, anaelekea kutegemea silika. Wakati unaotumiwa kungojea taa za barabarani na watembea-miguu unaonekana kuwa mrefu kwake kuliko vile ulivyo kwa mtu wa kawaida. Hivyo basi yeye anavurugika fikira na kupoteza subira yake haraka. Kushindwa kwake kufanya uamuzi timamu kabla ya kutenda kunamfanya awe dereva hatari.
Je! wewe unajiona katika yoyote ya namna hizi? Ni nini itikio lako wakati dereva fulani asiye mwenye ufikirio anapoijaribu subira yako? Ikiwa wewe ni wa namna hiyo, kubali. Kwa usalama wako mwenyewe, tii onyo, na ujitahidi kutengeneza udhaifu huo. Unahitaji kudhibiti maono ya moyoni na maelekeo yako ili uwe dereva mzuri.
Dereva Mwenye Kurekebika Vizuri
Lakini ni nini kinachofanya mtu kuwa dereva mzuri? Katika mahoji ya Amkeni!, wachunguzi mashuhuri kutoka polisi ya Japani walikazia ufikirio kwa wengine, kufikiri kabla ya kutenda, uwezo wa kuielewa hali nzima, hekima ya kuamua kwa usahihi, utambuzi, upole, kujidhibiti, na kutenda kwa njia inayolinda watumiaji wengine wa barabara.
Vivyo hivyo, ripoti moja kutoka Chuo Kikuu cha Wilaya ya Osaka inasimulia madereva wazuri kuwa “wenye kipimo cha juu cha imara ya maono ya moyoni; utendaji wa akili ya uamuzi wenye ufahamu unaofanya kazi haraka kuliko miitikio yao ya kimwili; uamuzi wao ni sahihi; wanaweza kudhibiti maono yao ya moyoni.” Je! usimulizi huu unapatana na wewe?
Kwa maelfu ya miaka, Biblia imekuwa ikifundisha watu jinsi ya kusitawisha hekima, uelewevu, na utambuzi. (Mithali 2:1-6) Inaonyesha jinsi wanadamu wasiokamilika wanavyoweza kubadili “hasira, na ghadhabu, na uovu, na matukano, na matusi” kwa “upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujidhibiti.” Ndiyo, Biblia hata inaweza kukusaidia uwe dereva mzuri zaidi!—Wakolosai 3:8-10, UV; Wagalatia 5:22, 23, NW.