Utawala wa Kibinadamu Wapimwa Katika Mizani
Utawala wa Kibinadamu Wapimwa Katika Mizani kwa Nini?
“Amkeni!” lapendezwa kutangaza mfululizo wa makala juu ya “Utawala wa Kibinadamu Wapimwa Katika Mizani”
HAKUNA mtu yeyote anayeweza kukanusha uvutano ambao serikali—kwa habari ya kisiasa—zimekuwa nao kwenye historia ya ulimwengu na juu ya kila mmoja wetu. Lugha unayonena, daraja unalofuatia maishani, aina ya kazi unayofanya, mfumo wa kijamii unaofurahia, yawezekana hata dini unayodai, zimeamuliwa kwako angalau kwa sehemu na mapendezi ya badiliko la kisiasa.
Kwa kuwa serikali ni ya lazima, ni nani miongoni mwetu asiyetamani kuishi chini ya umbo la serikali ambayo itatosheleza mahitaji yetu katika njia bora zaidi iwezekanayo? Lakini ni serikali ya aina gani inayofaa zaidi? Na je! hata tuna uchaguzi wowote juu ya habari hii ya utawala?
Amkeni! lafurahi kutangaza mfululizo wa makala juu ya “Utawala wa Kibinadamu Wapimwa Katika Mizani.” Hizo zitaendelea katika matoleo ya wakati ujao ya gazeti hili. Wakati wa sehemu fulani ya 1991, litashughulika na mandhari-nyuma ya kihistoria ya tawala za kifalme, za kikabaila, za wachache, na za wenye mali. Litashughulika na eneo kubwa la demokrasi, pamoja na aina nyingi tofauti-tofauti za jamhuri. Litaelekeza fikira kwenye tawala za mamlaka kamili ya mtu mmoja, za udikteta, na serikali zenye mamlaka kamili kama vile Ufashisti na Unazi wa enzi za Vita ya Ulimwengu ya 2. Usoshalisti na Ukomunisti utafikiriwa pia.
Mafumbo ya utawala wa kibinadamu ni mengi na yaliyotatanika, kwa hiyo si habari zote za serikali zitakazotolewa. Makala hizi hazikukusudiwa kuwa kitabu cha marejezeo chenye habari zote juu ya siasa. Hazitapendekeza wala kukazia faida za serikali za kibinadamu kwa ujumla wala umbo lolote hasa. Ulinganishi wowote kati ya maumbo mbalimbali hautakuwa kwa kusudi la kutetea moja kuliko lile jingine. Amkeni! litashikilia sana miongozo yalo iliyoonyeshwa kwenye ukurasa 5, ambapo twasoma hivi: “Linachunguza sana matukio ya sasa na kutoa maana ya kweli ya matukio hayo, hata hivyo linabaki sikuzote bila kuingilia siasa.”
Makala “Utawala wa Kibinadamu Wapimwa Katika Mizani” zimekusudiwa kuwa sehemu ya hatua hiyo ya kuchungulia “sana.” Zitaonyesha “maana ya kweli ya matukio hayo,” matukio yanaoonyesha kwamba utawala wa kibinadamu unakabiliana na msiba.
Kitabu The Columbia History of the World chaeleza msiba huo hivi: “Hali ambayo katika hiyo twaona ndani yake serikali, dini, adili, uhusiano wa kijamii, lugha, ufundi, na ule msingi wa upeo wa maisha yaliyostaarabika, tumaini la umma, huturuhusu angalau tukate kauli isiyothibitishwa juu ya ukubwa wa muhula wa sasa. Serikali ndiyo ya kwanza katika orodha na ndiyo ya kwanza katika umaana. . . . [Kuna] kudharau sheria, Taifa linaloitekeleza, na kwa watawala ambao wangali wanaamini mambo hayo mawili. . . . Mtazamo wa sasa unatofautiana sana na ule wa karne moja iliyopita . . . Katika sehemu nyingi za ulimwengu nguvu mbalimbali ziko tayari kwa amri ya neno moja kuvamia jumba la jiji, kuvunja baraza, kuharibu chuo kikuu, au kulipua makao ya ubalozi. . . . Hasira ya uhuru kamili imefoka. . . . Kwa ufupi, ulio wema mmoja wa kisiasa na kijamii, lililo lengo moja la uwezo wa wakati huu ni Ujitegemeo, bila kujali mawazo mengine ya kale ya falsafa yajionyesha kwa njia gani. Endapo bado hilo halijawa Uharibifu, bila shaka hilo ni Mvunjiko.”
Je! karibuni “Mvunjiko” utaongoza kwenye “Uharibifu,” na ikiwa ndivyo, hilo liwe na matokeo gani kwa ulimwengu tunamoishi? Ukweli ni kwamba utawala wa kibinadamu umo katika hukumu lakini si ya wanadamu tu, ambao wamekuwa wakipima serikali zao kwa maelfu ya miaka na kuzikuta zina kasoro tena na tena. Wakati huu Muumba wa ulimwengu wote mzima mwenyewe anataka hesabu itolewe. Je! rekodi ya utawala wa kibinadamu wakati wa karne zilizopita inautetea uruhusiwe uendelee? Au je! kupimwa kwao kwenye mizani ya hukumu ya kimungu kutaonyesha lazima uondolewe? Na ikiwa ndivyo, mahali pao paweza kuchukuliwa na nini?
Mfululizo wa makala “Utawala wa Kibinadamu Wapimwa Katika Mizani” utazidisha maarifa yako juu ya serikali. Nao utakujaza na tumaini kwa sababu wewe una kila ya sababu ya kuwa na maoni ya kutazamia mema. Serikali bora zaidi iko njiani. Na lililo bora zaidi ya yote, wewe waweza kuishi uifurahie!
[Picha katika ukurasa wa 9]
Wakati rekodi ya utawala wa kibinadamu inapopimwa katika mizani ya haki ya kimungu, je! hukumu ya Mungu itakuwa ya wema?
[Hisani]
WHO photo/PAHO by J. Vizcarra