Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g91 12/8 kur. 15-19
  • Sehemu ya 10: Hatimaye Serikali Kamilifu!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Sehemu ya 10: Hatimaye Serikali Kamilifu!
  • Amkeni!—1991
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Utafutaji wa Serikali Nzuri
  • Theokrasi ya Aina Gani?
  • Theokrasi za Bandia
  • Serikali Kamilifu I Karibu
  • Kaa Karibu na Theokrasi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Yehova Atawala—Kupitia Theokrasi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Wachungaji na Kondoo Katika Theokrasi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Serikali ya Mungu Inaanza Kutawala
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1991
g91 12/8 kur. 15-19

Utawala wa Kibinadamu Wapimwa Katika Mizani

Sehemu ya 10: Hatimaye Serikali Kamilifu!

Theokrasi: latokana na maneno ya Kigiriki “the·osʹ” (mungu) na “kraʹtos” (utawala); hivyo, serikali kupitia uelekezi au usimamizi wa Mungu, nyakati nyingine kupitia wawakilishi walioteuliwa.

IKIWA wewe ungeweza kununua mkufu wa lulu halisi au pete ya almasi, je! ungechukua mwigizo mbovu tu wa ile ya halisi? Labda sivyo, isipokuwa uwe ulidanganyika ukaamini kwamba kile ulichokuwa ukipata ndicho kilichokuwa bora zaidi ambacho kingeweza kupatikana.

Kwa habari ya serikali, mamia ya mamilioni ya watu wamedanganywa wakaamini kuwa wanapata ile bora iwezayo kupatikana. Kwa uhalisi hatimaye wanapata miigizo mibovu. Si ajabu kwamba wamekata tamaa, wamekosa kutosheka na wamefadhaika.

Utafutaji wa Serikali Nzuri

William Ralph Inge, aliyekuwa wakati mmoja mkuu wa makasisi wa Kanisa Anglikana la St. Paul’s Cathedral, London, aliandika hivi katika 1922: “Serikali nzuri ingali ndiyo baraka iliyo bora zaidi kwa binadamu, na hakuna taifa lolote lililopata kuifurahia wakati wowote.” Kwa nini?

Maelezo ya kadiri fulani yaweza kupatikana katika maneno ya John F. Kennedy, rais wa 35 wa United States. “Hakuna serikali iliyo nzuri kushinda wale wanaoifanyiza,” yeye akasema. Kwa kuwa hata mwanasiasa aliye hodari kushinda wote si mkamilifu, kila serikali ambayo wanadamu wanaanzisha haitafaulu.

Mtunga hadithi ya drama Mwingereza wa karne ya kumi na saba Philip Massinger alikuwa sahihi alipoandika hivi: “Yeye ambaye angeongoza wengine, lazima kwanza ajiweze mwenyewe.” Lakini ni binadamu gani asiyekamilika anayejiweza mwenyewe kweli kweli? Hakika, hakuna mwanasiasa aliye na maarifa na hekima za kutosha ili kuongoza matukio na hali na hivyo kuhakikisha furaha yake na hali njema yake, licha ya furaha na hali njema ya mamilioni ya wanadamu wenzake. Na hata ikiwa nyakati zote angeweza kufanya maamuzi yanayofaa, hangeweza kuwa na mamlaka ya kuyatekeleza.

Mtungaji wa insha Mwamerika Brooks Atkinson, akitambua tatizo hilo, kule nyuma katika 1951, alikata kauli hivi: “Twahitaji binadamu walio na uwezo unaoshinda ule wa mwanadamu kututawala—kazi ni kubwa mno na uhitaji wa uamuzi wenye hekima ni wa muhimu sana. Lakini, wapi,” yeye alisema, “hakuna watu wenye uwezo unaoshinda ule wa mwanadamu.” Leo, karne nne baadaye, bado hakuna hata mmoja.

Kwa hakika, Mungu hakukusudia kamwe wanadamu wajitawale wenyewe. Ili kufurahia serikali kamilifu, wanadamu wanahitaji zaidi ya serikali ya binadamu wenye uwezo unaoshinda ule wa mwanadamu tu. Wanahitaji theokrasi, serikali ya Mungu.

Theokrasi ya Aina Gani?

Theokrasi ndiyo aina ya serikali iliyotawala katika Edeni, ambako Mungu aliweka wanadamu wa kwanza wawili. Akiwa Mwenye Enzi Kuu aliye na haki, Mungu hapo kwanza alisimamia mambo na kumiliki.

Wakati mwanahistoria wa Kiyahudi Flavio Yosefo alipotunga kwa mara ya kwanza neno la Kigiriki linalotafsiriwa “theokrasi” karibu karne 19 zilizopita, alilitumia kurejezea kwenye taifa la kale la Israeli. Huo ulikuwa utambulisho unaofaa, kwa kuwa Israeli wakati huo lilikuwa ni taifa lililochaguliwa na Mungu. Kwa kweli lilikuwa likitawalwa na yeye, ingawa utawala wake ulikuwa ukitekelezwa kupitia wawakilishi wa kidunia.—Kumbukumbu 7:6; 1 Nyakati 29:23.

Wakati neno “theokrasi” lilipoingizwa katika lugha nyingine, hapo kwanza lilihusu hasa maana ambayo Yosefu alikusudia. Lakini baadaye likachukua maana nyingine zaidi. Kulingana na The Encyclopedia of Religion, ‘limetumika kwa upana kwa mambo mbalimbali kama vile Misri ya kifarao, Israeli ya kale, Jumuiya ya Wakristo ya enzi za kati, Ukalvini, Uislamu, na Ubuddha wa Tibet.’

Mwanahistoria W. L. Warren asema kwamba kulikuwako “katika umaliki wa Uingereza sehemu ya uufalme wa kitheokrasi—mfalme akiwa ndiye chombo kikuu katika mpango wa kimungu wa kutawala ulimwengu wote, mfalme akiwa ndiye mwakilishi na mtekeleza-hukumu wa Mungu.” Katika nyakati za kisasa neno hilo hata limetumika, aeleza Dewey Wallace Jr., wa Chuo Kikuu cha George Washington, kuwa usemi wa “‘maarifa’ hafifu kwa jamii ‘zenye kutawalwa na makasisi.’”

Maana pana inayotiwa katika neno hilo inaruhusu kuwapo kwa aina nyingi za theokrasi. Sisi twahitaji ya aina gani?

Theokrasi za Bandia

Serikali ya kwanza ya kibinadamu katika rekodi ya historia ilianzishwa yapata miaka 4,000 iliyopita na Nimrodi. Kitukuu huyo wa Nuhu alijifanya mfalme akawa, kama anavyosimuliwa katika Biblia, “mwindaji mwenye nguvu katika kupingana na Yehova.” (Mwanzo 10:8, 9, NW) Kwa kujiweka kuwa mtawala katika kumpinga Yehova, Nimrodi alijifanya mwenyewe kuwa mungu wa kisiasa. Kwa hiyo alikuwa na utegemezo wa mpinzani mkuu wa Mungu, yule mungu bandia Shetani Ibilisi. (2 Wakorintho 4:4) Hivyo utawala wa Nimrodi ulikuwa ni mwigizo bandia wa theokrasi halisi.

Baadaye wakaaji wa milki ya Nimrodi walipotawanywa duniani pote, watu waliendelea kufikiri kwamba serikali zao zilikuwa za kitheokrasi, yaani, zikipata mamlaka kutoka kwa mungu au miungu waliyoabudu. (Mwanzo 11:1-9) Hivyo, “theokrasi” likaja kutumiwa “kueleza namna ya mapema ya ustaarabu wa kale wa mashariki ambao katika huo hakukuwako tofauti kati ya dini na serikali,” chasema The Encyclopedia of Religion.

Katika tamaduni fulani, kama vile Misri chini ya Mafarao, mfalme aliaminiwa kuwa mwenzi wa mungu-mke mkuu au mwana wa mungu. Utamaduni mwingine mbalimbali, ulisema machache tu kuhusu zilizodhaniwa kuwa sifa au nasaba za kimungu za mfalme, badala ya hivyo ukikazia tu wazo la kuchaguliwa kimungu. Katika Ugiriki wa wakati wa Aleksanda na baadaye, mfalme alionwa kuwa wa kimungu, chaeleza kitabu A History of Political Theory, “kwa sababu alileta upatano kwenye ufalme wake kama vile Mungu aletavyo upatano katika ulimwengu.” Kitabu hicho cha historia chaendelea kusema: “Alikuwa na uungu ambao mtu wa kawaida hakuwa nao na ambao ulileta msiba kwa mnyakuaji wa utawala asiyestahili aliyechukua cheo hicho kikubwa bila baraka ya Mbinguni.”

Wazo la kwamba mfalme ni wa kimungu lilifuatwa hadi kwenye inayoitwa eti enzi ya Ukristo. Baada ya makabila ya Teutoni kuongolewa kwenye Ukatoliki, fahari ya mfalme iliongezeka. Kuvishwa taji na kanisa kulionyesha kwamba Mungu mwenyewe alikuwa amechagua mfalme huyo kutawala. Kutokana na msingi huo, fundisho linalojulikana kama haki ya kimungu ya wafalme lilisitawi polepole.

Hata kabla ya enzi ya “Ukristo,” Makaisari wa Rumi walikuwa wamegeuza serikali yao kuwa ya theokrasi kwa kudai uungu. Machoni pa Warumi, utawala wa kibinadamu ulikuwa sawa na utawala wa mungu, ikifanya serikali yao, kama ile ya Nimrodi, iwe theokrasi ya bandia. Hivyo wakati viongozi wa kidini Wayahudi wa karne ya kwanza walipomkataa Yesu kuwa Mfalme mkusudiwa wakisema, “Sisi hatuna mfalme ila Kaisari,” kwa hakika walikuwa wakionyesha kupendelea mwigizo bandia wa theokrasi kuliko ile ambayo Yesu alikuwa akitangaza.—Yohana 19:15.

Kwa kuwa utawala wa kitheokrasi kupitia Yehova ni bora zaidi ya utawala wowote mwingine, haishangazi, kwamba Shetani amejaribu kuingiza baadhi ya sehemu zao katika miigizo yake bandia iliyofanyizwa na binadamu—lakini bila mafanikio. Theokrasi hizi zote zenye kuitwa hivyo isivyostahili hazikaribii hata kidogo ile inayofaa. Kwa uhalisi, hakuna yoyote ambayo imekuwa utawala kupitia Mungu au kupitia wawakilishi wake. Imekuwa miigizo mibovu ya ile halisi, maonyesho ya utawala wa kibinadamu usiokamilika ulio chini ya uongozi wa mungu bandia.

Kwa kufaa, Biblia inamwita mungu huyo “mkuu wa ulimwengu huu” na “mungu wa dunia hii.” (Yohana 12:31; 14:30; 2 Wakorintho 4:4) Hiyo ndiyo sababu aliweza kumtolea Yesu “milki zote za ulimwengu, na fahari yake,” kishawishi ambacho Yesu alikataa katakata. (Mathayo 4:8-10) Yesu akijua kwamba theokrasi halisi ni utawala wa Mungu mmoja wa kweli, Yehova, hakudanganywa akubali vibadala vilivyofanyizwa na binadamu visivyoweza kuonyesha usawaziko kamili wa sifa za kimungu zinazopatikana katika ile iliyo halisi.

Serikali Kamilifu I Karibu

Miaka kadhaa iliyopita, Hugh Brogan wa Chuo Kikuu cha Essex alikata kauli hivi: “Ikiwa binadamu, aliye mnyama wa kisiasa, atajiokoa mwenyewe na staarabu zake, bado hawezi kujistarehesha asitafute aina mpya za serikali ili kutosheleza mahitaji ya nyakati zake ambayo ni mapya daima.” Tangu siku ya Nimrodi, wanadamu wamekuwa wakifanya hivyo hasa, wakirudia-rudia kubuni aina mpya za serikali ili kutosheleza mahitaji ya nyakati. Lakini ni wakati mwingi kadiri gani hasa unaohitajika ili kuthibitisha ya kwamba utawala wa kibinadamu hauwezi kufaulu hata kidogo?

Kwa furaha, katika 1914 wakati ulifika wa jaribio la kijinga la serikali ya kibinadamu likabiliwe na usimamisho wa ufalme wa Yehova wa Kimesiya mbinguni!a Tangu 1914, ingawa serikali za kibinadamu, zaendelea kung’ang’ania kuwako, zimekuwa zikiendelea kuwako kwa wakati ulioazimwa. (Danieli 7:12) Tunaishi katika kipindi ambacho Biblia yakitambulisha kuwa “siku za mwisho.” (2 Timotheo 3:1-5) Ishara inayoonyesha uharibifu ulio karibu sana wa utawala wa kibinadamu iko wazi sana hivi kwamba hakuna anayeweza kuipuuza kihaki. Inaweza kupuuzwa, lakini haiwezi kufutwa.

Katika Biblia kwenye Danieli sura ya 2 utawala wa kitheokrasi kupitia Ufalme wa Kimesiya wa Yehova unawakilishwa na jiwe ‘lililochongwa bila kazi ya mkono’ ambalo ‘lilipiga sanamu [ufananisho wa utawala wa kibinadamu] kwenye miguu yake, iliyokuwa ya chuma na udongo, likaivunja vipande vipande.’ Hilo linamaanisha kwamba Ufalme wa Mungu uliosimamishwa utaharibu kila namna ya utawala mbovu wa kibinadamu hivi karibuni, uuvunje vipande vipande. Kwa ukamili jinsi gani? Biblia inajibu: “Ndipo kile chuma, na ule udongo, na ile shaba, na ile fedha, na ile dhahabu, vilivunjwa vipande vipande pamoja, vikawa kama makapi ya viwanja vya kupepetea wakati wa hari; upepo ukavipeperusha, hata pasionekane mahali pake.”—Danieli 2:34, 35.

Ikiwa serikali mbovu za kibinadamu zitafagiliwa mbali kwa ukamili hivi kwamba mahali pazo hapataonekana kamwe, basi ni wazi kwamba watetezi wa utawala wa kibinadamu watapatwa na nyakati ngumu. Wakitambua uhakika huo, mamilioni ya watu wanaona hekima ya kuondoa tegemeo lao kutoka utawala wa kibinadamu uliopotoka hadi kwenye mwingine ulio bora zaidi. Utawala wa Yehova Mungu tu, Muumba wa ulimwengu wote mzima, ndio uwezao kusuluhisha matatizo yaliyoletwa na maelfu ya miaka ya utawala mbaya na usimamizi mbaya wa kibinadamu. Theokrasi ya kweli tu ndiyo inayoweza kutosheleza mahitaji ya nyakati zetu.

Amkeni! linatumaini kwamba mfululizo huu wenye sehemu kumi “Utawala wa Kibinadamu Wapimwa Katika Mizani” umekukazia umaana wa kufanya uamuzi wa kibinafsi juu ya jambo hili la serikali. Na juu ya yote inatumainiwa kwamba utakusaidia kufanya uamuzi wa hekima. Utawala wa kibinadamu umekwisha pimwa katika mizani na kupatikana umepungukiwa. Je! utachagua nini? Mwigizo bandia ulio duni au kile kilicho halisi? Utawala wa kibinadamu au utawala wa Mungu wa kweli, Yehova?—Danieli 2:44; Mathayo 6:9, 10.

[Maelezo ya Chini]

a Kwa uthibitisho wa kwamba Ufalme wa Mungu ulisimamishwa 1914 na ya kuwa ulimwengu huu umekuwa katika siku zake za mwisho tangu wakati huo, ona sura 16 na 18 za kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani, kilichotangazwa katika 1982 na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

[Sanduku katika ukurasa wa 17]

Mambo Ambayo Utawala wa Kitheokrasi wa Yehova Utafanya

◆ Utarudisha wazee wanyonge kwenye nguvu za ujana.—Ayubu 33:25.

◆ Utafanya vita kuwa jambo la kale.—Zaburi 46:9; Isaya 9:7.

◆ Utaipa kila familia makao bora kabisa.—Isaya 65:21.

◆ Utaponya wagonjwa na wasiojiweza.—Isaya 33:24; 35:5, 6.

◆ Utafufua wafu.—Isaya 25:8; Matendo 24:15; Ufunuo 20:13.

◆ Utaondoa ufisadi, ukosefu wa adili, na uhalifu.—Mithali 2:21, 22.

◆ Utatoa chakula cha kutosha kwa wote.—Zaburi 72:16; Isaya 25:6.

◆ Utarudisha uhusiano wa amani kati ya wanadamu na wanyama.—Isaya 11:6-9; Ezekieli 34:25.

◆ Utagawia kila mtu kazi yenye kujaa maana na yenye kuthawabisha.—Isaya 65:22, 23.

◆ Utageuza dunia kuwa paradiso ya tufe lote.—Isaya 35:1, 6, 7; Luka 23:43,“ZSB.”

Hizi si ahadi za kisiasa za bure zenye kufanywa na wanadamu; ni ahadi zilizofanywa na Mungu, na “Mungu hawezi kusema uongo.”—Waebrania 6:18.

[Picha katika ukurasa wa 18]

Baraka za milele za serikali kamilifu zaweza kuwa zako!

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki