Yehova Atawala—Kupitia Theokrasi
“BWANA [Yehova, NW] atamiliki milele.”—ZABURI 146:10.
1, 2. (a) Kwa nini jitihada za binadamu kuhusu utawala zimeshindwa? (b) Ni nini imekuwa namna ya serikali ambayo imekuwa yenye mafanikio kwelikweli?
TANGU wakati wa Nimrodi, watu wamejaribu njia tofauti za kutawala jamii ya kibinadamu. Kumekuwa na serikali za kidikteta, za wafalme, za wachache, na namna mbalimbali za demokrasi. Yehova ameruhusu hizo zote. Kwa kweli, kwa kuwa Mungu ndiye Chanzo kikuu zaidi cha mamlaka yote, katika maana fulani aliwaweka watawala tofauti-tofauti katika vyeo vinavyowahusu. (Warumi 13:1) Hata hivyo, jitihada zote za binadamu kuhusiana na serikali zimeshindwa. Hakuna mtawala wa kibinadamu ambaye ametokeza jamii yenye kudumu muda mrefu, iliyo thabiti na ya haki. Mara nyingi sana, “mwanadamu ametawala mwanadamu kwa hasara yake.”—Mhubiri 8:9, NW.
2 Je! hilo litushangaze? Bila shaka la! Binadamu asiyekamilika hakufanywa ajitawale mwenyewe. “Njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” (Yeremia 10:23) Ndiyo sababu, muda wote wa historia ya kibinadamu, ni namna moja tu ya serikali ambayo imefanikiwa kwelikweli. Ni ipi? Theokrasi chini ya Yehova Mungu. Katika Kigiriki cha Kibiblia, “theokrasi” yamaanisha utawala [kraʹtos] wa Mungu [the·osʹ]. Kungeweza kuwa na serikali gani bora zaidi kuliko ile ya Yehova Mungu mwenyewe?—Zaburi 146:10.
3. Ni nini zilizo baadhi ya vielelezo vya mapema vya theokrasi vilivyokuwako duniani?
3 Theokrasi ilitawala kwa muda mfupi katika Edeni, mpaka Adamu na Hawa walipoasi dhidi ya Yehova. (Mwanzo 3:1-6, 23) Katika wakati wa Abrahamu, yaonekana theokrasi ilikuwako katika jiji la Salemu, Melkizedeki akiwa ndiye mfalme-kuhani. (Mwanzo 14:18-20; Waebrania 7:1-3) Hata hivyo, theokrasi ya kwanza ya kitaifa chini ya Yehova Mungu ilisimamishwa katika jangwa la Sinai katika karne ya 16 K.W.K. Hilo lilitokeaje? Na serikali hiyo ya kitheokrasi ilitendaje kazi?
Theokrasi Yazaliwa
4. Yehova alisimamishaje taifa la Israeli la kitheokrasi?
4 Katika 1513 K.W.K., Yehova aliwaokoa Waisraeli kutoka utumwani Misri akayaharibu majeshi ya Farao yaliyokuwa yakiwafuata katika Bahari Nyekundu. Kisha Yeye akawaongoza Waisraeli hadi Mlima Sinai. Walipokuwa wamepiga kambi chini ya mlima huo, Mungu aliwaambia hivi kupitia Musa: “Mmeona jinsi nilivyowatendea Wamisri, na jinsi nilivyowachukua ninyi juu ya mbawa za tai, nikawaleta ninyi kwangu mimi. Sasa basi ikiwa mtaitii sauti yangu kweli kweli, na kulishika agano langu, hapo ndipo mtakapokuwa tunu kwangu kuliko makabila yote ya watu.” Waisraeli waliitikia: “Hayo yote aliyoyasema BWANA [Yehova, NW] tutayatenda.” (Kutoka 19:4, 5, 8) Agano lilifanyizwa, na lile taifa la Israeli la kitheokrasi lilizaliwa.—Kumbukumbu la Torati 26:18, 19.
5. Yaweza kusemwaje kwamba Yehova alitawala katika Israeli?
5 Lakini, Israeli lilitawaliwaje na Yehova, ambaye hawezi kuonekana kwa macho ya kibinadamu? (Kutoka 33:20) Kwa kuwa sheria na ukuhani wa taifa ulitolewa na Yehova. Wale waliotii sheria na kuabudu kulingana na mipango iliyoamriwa kimungu walimtumikia yule Theokrati Mkuu, Yehova. Kwa kuongezea, kuhani mkuu alikuwa na Urimu na Thumimu, ambazo Yehova Mungu alitumia kutoa mwongozo katika nyakati za dharura. (Kutoka 28:29, 30) Zaidi ya hayo, wanaume wazee waliokuwa na sifa za kustahili walikuwa wawakilishi wa Yehova katika theokrasi hiyo na walihakikisha kwamba Sheria ya Mungu ilikuwa ikifuatwa. Tukifikiria rekodi ya baadhi ya wanaume hao, tutaelewa vema zaidi jinsi wanadamu wapaswavyo kujitiisha kwa utawala wa Mungu.
Mamlaka Chini ya Theokrasi
6. Kwa nini lilikuwa jambo gumu kwa wanadamu kuwa na mamlaka katika theokrasi, na ni watu wa aina gani waliohitajiwa kwa ajili ya daraka hilo?
6 Wale waliokuwa katika vyeo vya mamlaka katika Israeli walikuwa na pendeleo kubwa, lakini walihitaji kujitahidi sana ili kudumisha usawaziko wao. Walilazimika kuwa waangalifu wasije wakajiona kamwe kuwa wa maana zaidi ya utakasaji wa jina la Yehova. Ile taarifa iliyopuliziwa kwamba “kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu” ilikuwa kweli kwa habari ya Waisraeli kama vile ilivyokuwa kweli kwa sehemu ile nyingine ya ainabinadamu. Israeli lilisitawi tu wakati wale wanaume wazee walipokumbuka kwamba Israeli lilikuwa la theokrasi na kwamba walipaswa kufanya mapenzi ya Yehova, si yao wenyewe. Upesi baada ya kusimamishwa kwa Israeli, baba-mkwe wa Musa, Yethro, alieleza vema aina ya watu waliopaswa kuwa, yaani, “watu walio na uwezo, wenye kumcha Mungu, watu wa kweli, wenye kuchukia mapato ya udhalimu.”—Kutoka 18:21.
7. Musa alikuwa kielelezo chema katika njia zipi cha mtu aliyekuwa na mamlaka chini ya Yehova Mungu?
7 Musa alikuwa mtu wa kwanza kuwa na mamlaka ya juu katika Israeli. Alikuwa kielelezo chema cha mtu mwenye mamlaka ya kitheokrasi. Ni kweli, katika pindi moja udhaifu wa kibinadamu ulitokea. Hata hivyo, Musa alimtegemea Yehova sikuzote. Maswali yalipotokea ambayo tayari hayakuwa yamesuluhishwa, alitafuta mwongozo wa Yehova. (Linganisha Hesabu 15:32-36.) Musa alikinzaje kishawishi cha kutumia cheo chake cha juu kwa ajili ya utukufu wake mwenyewe? Ingawa aliongoza taifa la mamilioni ya watu, “alikuwa mpole sana zaidi ya wanadamu wote waliokuwa juu ya uso wa nchi.” (Hesabu 12:3) Hakuwa na tamaa za makubwa za kibinafsi lakini alihangaikia utukufu wa Mungu. (Kutoka 32:7-14) Na Musa alikuwa na imani yenye nguvu. Akisema juu yake kabla ya yeye kuwa kiongozi wa kitaifa, mtume Paulo alisema hivi: “Alistahimili kama amwonaye yeye asiyeonekana.” (Waebrania 11:27) Kwa wazi, Musa hakusahau kamwe kwamba Yehova alikuwa ndiye Mtawala halisi wa taifa. (Zaburi 90:1, 2) Hicho ni kielelezo chema kama nini kwetu sisi leo!
8. Yehova alimpa Yoshua amri gani, na kwa nini hiyo yastahili kufikiriwa?
8 Uangalizi wa Israeli ulipothibitika kuwa wenye kulemea sana kwa Musa akiwa peke yake, Yehova aliweka roho yake juu ya wanaume wazee 70 ambao wangemwunga mkono katika kuhukumu taifa. (Hesabu 11:16-25) Katika miaka ya baadaye kila jiji lingekuwa na wanaume wazee walo. (Linganisha Kumbukumbu la Torati 19:12; 22:15-18; 25:7-9.) Baada ya Musa kufa, Yehova alimfanya Yoshua awe kiongozi wa taifa. Twaweza kuwazia kwamba akiwa na pendeleo hilo, Yoshua alikuwa na mengi ya kufanya. Hata hivyo, Yehova alimwambia kwamba kulikuwa na jambo moja ambalo hakupaswa aliache kamwe: “Kitabu hiki cha torati kisiondoke kinywani mwako, bali yatafakari maneno yake mchana na usiku, upate kuangalia kutenda sawasawa na maneno yote yaliyoandikwa humo.” (Yoshua 1:8) Ona kwamba ingawa Yoshua alikuwa ametumikia kwa zaidi ya miaka 40, alihitaji kuendelea kuisoma Sheria. Sisi pia twahitaji kujifunza Biblia na kuburudisha akili zetu kuhusiana na sheria na kanuni za Yehova—iwe rekodi yetu ya utumishi ni ndefu kadiri gani au tuna mapendeleo mengi kadiri gani.—Zaburi 119:111, 112.
9. Ni nini kilichotokea katika Israeli katika wakati wa waamuzi?
9 Yoshua alifuatwa na mfululizo wa waamuzi. Kwa kusikitisha, mara nyingi katika wakati wao Waisraeli “walifanya yaliyokuwa ni maovu mbele za macho ya BWANA [Yehova, NW].” (Waamuzi 2:11) Kuhusu kipindi cha waamuzi, rekodi husema hivi: “Siku hizo hapakuwa na mfalme katika Israeli; kila mtu alifanya yaliyokuwa ni mema machoni pake mwenyewe.” (Waamuzi 21:25) Kila mtu alifanya maamuzi yake mwenyewe juu ya mwenendo na ibada, na historia yaonyesha kwamba Waisraeli wengi walifanya maamuzi mabaya. Waliangukia ibada ya sanamu na nyakati nyingine walifanya uhalifu mbalimbali wenye kuchukiza. (Waamuzi 19:25-30) Lakini, baadhi yao walionyesha imani iliyokuwa kielelezo chema.—Waebrania 11:32-38.
10. Serikali katika Israeli ilibadilikaje sana katika wakati wa Samweli, na ni nini kilichoongoza kwenye hilo?
10 Katika maisha ya mwamuzi wa mwisho, Samweli, Israeli lilipitia wakati mgumu kwa habari ya serikali. Wakivutwa na mataifa ya maadui yaliyowazunguka, yote yakitawalwa na wafalme, Waisraeli walisababu kwamba wao pia walihitaji mfalme. Walisahau kwamba tayari walikuwa na Mfalme, kwamba serikali yao ilikuwa ya theokrasi. Yehova alimwambia Samweli hivi: “Hawakukukataa wewe, bali wamenikataa mimi, ili nisiwe mfalme juu yao.” (1 Samweli 8:7) Kielelezo chao chatukumbusha jinsi ilivyo rahisi kupoteza maoni yetu ya kiroho na kuvutwa na ulimwengu unaotuzunguka.—Linganisha 1 Wakorintho 2:14-16.
11. (a) Lijapokuwa badiliko katika serikali, yaweza kusemwaje kwamba Israeli liliendelea kuwa theokrasi chini ya wafalme? (b) Yehova aliwapa wafalme wa Israeli amri gani, na kwa kusudi gani?
11 Hata hivyo, Yehova alikubali ombi la Waisraeli akachagua wafalme wao wawili wa kwanza, Sauli na Daudi. Israeli liliendelea kuwa la theokrasi, likitawalwa na Yehova. Ili wafalme walo wakumbuke jambo hilo, kila mmoja wao alikuwa na wajibu wa kufanya nakala yake mwenyewe ya Sheria na kuisoma kila siku, “ili apate kujifunza kumcha BWANA [Yehova, NW], Mungu wake, ayashike maneno yote ya torati hii na amri hizi, kwa kuyafanya; moyo wake usije ukainuliwa juu ya ndugu zake.” (Kumbukumbu la Torati 17:19, 20) Ndiyo, Yehova alitamani kwamba wale wenye mamlaka katika theokrasi yake wasingejitukuza na kwamba matendo yao yangeonyesha Sheria yake.
12. Mfalme Daudi alikuwa na rekodi gani ya uaminifu?
12 Mfalme Daudi alikuwa na imani yenye kutokeza katika Yehova, na Mungu alifanya agano kwamba angekuwa baba wa mstari wa wafalme ambao ungedumu milele. (2 Samweli 7:16; 1 Wafalme 9:5; Zaburi 89:29) Ujitiisho mnyenyekevu wa Daudi kwa Yehova ulistahili kuigwa. Alisema hivi: “Ee BWANA [Yehova, NW], mfalme atazifurahia nguvu zako, na wokovu wako ataufanyia shangwe nyingi sana.” (Zaburi 21:1) Ingawa nyakati nyingine Daudi alishindwa kwa sababu ya udhaifu wa kimwili, kwa desturi yeye alitegemea nguvu za Yehova, si zake mwenyewe.
Matendo na Mitazamo Isiyo ya Kitheokrasi
13, 14. Ni nini baadhi ya hatua zisizo za kitheokrasi zilizochukuliwa na waandamizi wa Daudi?
13 Si viongozi wote Waisraeli waliokuwa kama Musa na Daudi. Wengi walionyesha ukosefu mkubwa wa staha kuelekea mpango wa kitheokrasi, wakiruhusu ibada bandia katika Israeli. Pindi nyingine hata baadhi ya watawala waaminifu walitenda kwa njia isiyo ya kitheokrasi. Hali ya Sulemani, aliyepewa hekima na ufanisi mwingi, ilikuwa yenye kuhuzunisha sana. (1 Wafalme 4:25, 29) Lakini, kwa kupuuza sheria ya Yehova, yeye alioa wake wengi na kuruhusu ibada ya sanamu katika Israeli. Yaonekana, utawala wa Sulemani ulikuwa mwonevu katika miaka yake ya baadaye.—Kumbukumbu la Torati 17:14-17; 1 Wafalme 11:1-8; 12:4.
14 Rehoboamu mwana wa Sulemani alikabili dai la kwamba arahisishe mzigo wa raia wake. Badala ya kushughulikia hali hiyo kwa upole, alijidaia mamlaka yake kwa ugomvi—akapoteza makabila 10 kati ya yale 12. (2 Mambo ya Nyakati 10:4-17) Mfalme wa kwanza wa yale makabila kumi yaliyojitenga alikuwa Yeroboamu. Ili ahakikishe kwamba ufalme wake usingejiunga tena kamwe na taifa jenzilo, alisimamisha ibada ya ndama. Huenda ikawa hiyo ilionekana kuwa hatua yenye werevu kisiasa, lakini ilionyesha kupuuza kwa theokrasi kwa njia ya majivuno. (1 Wafalme 12:26-30) Baadaye, mwishoni mwa maisha marefu ya utumishi mwaminifu, Mfalme Asa aliruhusu kiburi kitie waa rekodi yake. Alimtenda vibaya nabii aliyemjia akiwa na shauri kutoka kwa Yehova. (2 Mambo ya Nyakati 16:7-11) Ndiyo, nyakati nyingine hata wale ambao wamekuwa waaminifu kwa miaka mingi huhitaji shauri.
Mwisho wa Theokrasi
15. Yesu alipokuwa duniani, viongozi wa Kiyahudi walishindwaje wakiwa watu wenye mamlaka katika theokrasi?
15 Yesu Kristo alipokuwa duniani, Israeli lilikuwa la theokrasi bado. Lakini, kwa kusikitisha, wengi wa wanaume walo wazee wenye daraka hawakuwa na akili za kiroho. Kwa hakika walishindwa kusitawisha ule usikivu ambao Musa alionyesha. Yesu alionyesha ufisadi wao wa kiroho aliposema hivi: “Waandishi na Mafarisayo wameketi katika kiti cha Musa; basi, yo yote watakayowaambia, myashike na kuyatenda; lakini kwa mfano wa matendo yao, msitende; maana wao hunena lakini hawatendi.”—Mathayo 23:2, 3.
16. Viongozi wa Kiyahudi wa karne ya kwanza walionyeshaje kwamba hawakuwa na staha kuelekea theokrasi?
16 Baada ya kumkabidhi Yesu kwa Pontio Pilato, viongozi wa Kiyahudi walionyesha jinsi walivyokuwa wamepotelea mbali kutoka kwenye ujitiisho wa kitheokrasi. Pilato alimhoji Yesu akakata maneno kwamba alikuwa mtu asiye na hatia. Akimtoa Yesu nje mbele ya Wayahudi, Pilato alisema hivi: “Tazama, Mfalme wenu!” Wayahudi walipofanya ghasia kuomba Yesu auawe, Pilato aliuliza hivi: “Je! nimsulibishe [nimtundike, NW] mfalme wenu!” Makuhani wakuu walijibu: “Sisi hatuna mfalme ila Kaisari.” (Yohana 19:14, 15) Walimkiri Kaisari kuwa mfalme, si Yesu, ‘aliyekuja kwa jina la Yehova’!—Mathayo 21:9.
17. Kwa nini Israeli la kimwili lilikoma kuwa taifa la kitheokrasi?
17 Katika kumkatalia mbali Yesu, Wayahudi walikatalia mbali theokrasi, kwani yeye angekuwa ndiye mtu mkuu katika mipango ya kitheokrasi ya wakati ujao. Yesu alikuwa mwana wa kifalme wa Daudi ambaye angetawala milele. (Isaya 9:6, 7; Luka 1:33; 3:23, 31) Hivyo, Israeli la kimwili lilikoma kuwa taifa teule la Mungu.—Warumi 9:31-33.
Theokrasi Mpya
18. Ni theokrasi mpya gani iliyozaliwa katika karne ya kwanza? Eleza.
18 Hata hivyo, tendo la Mungu la kukatalia mbali Israeli la kimwili halikuwa mwisho wa theokrasi duniani. Kupitia Yesu Kristo, Yehova alisimamisha theokrasi mpya. Hilo lilikuwa kutaniko la Kikristo la wapakwa, ambalo kwa kweli lilikuwa taifa jipya. (1 Petro 2:9) Mtume Paulo aliliita “Israeli wa Mungu,” na hatimaye washiriki walo walitoka “kila kabila na lugha na jamaa na taifa.” (Wagalatia 6:16; Ufunuo 5:9, 10) Ingawa walijitiisha kwa serikali za kibinadamu ambazo waliishi chini yazo, washiriki wa theokrasi hiyo mpya kwa kweli walikuwa wakitawalwa na Mungu. (1 Petro 2:13, 14, 17) Upesi baada ya kuzaliwa kwa theokrasi hiyo mpya, watawala wa Israeli la kimwili walijaribu kuwalazimisha baadhi ya wanafunzi waache kutii amri ambayo Yesu alikuwa amewapa. Itikio lilikuwa nini? “Imetupasa kumtii Mungu [kuwa mtawala, NW] kuliko wanadamu.” (Matendo 5:29) Maoni ya kitheokrasi kwelikweli!
19. Kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza lingeweza kuitwaje theokrasi?
19 Lakini, theokrasi hiyo mpya ilitendaje kazi? Kulikuwa na Mfalme, Yesu Kristo, akimwakilisha yule Theokrati Mkuu, Yehova Mungu. (Wakolosai 1:13) Ingawa Mfalme hakuonekana akiwa mbinguni, utawala wake ulikuwa halisi kwa raia wake, na maneno yake yaliongoza maisha zao. Kwa habari ya uangalizi wenye kuonekana, wanaume wazee wenye sifa za kustahili kiroho waliwekwa rasmi. Katika Yerusalemu kikundi cha wanaume hao kilitenda kazi kikiwa baraza lililoongoza. Waliowakilisha baraza hilo ni wazee wasafirio, kama vile Paulo, Timotheo, na Tito. Na kila kutaniko lilitunzwa na baraza la wanaume wazee, au wazee. (Tito 1:5) Tatizo gumu lilipotokea, wazee walishauriana na baraza lililoongoza au na mmoja wa wawakilishi walo, kama vile Paulo. (Linganisha Matendo 15:2; 1 Wakorintho 7:1; 8:1; 12:1.) Zaidi ya hayo, kila mshiriki wa kutaniko alishiriki sehemu katika kuunga mkono theokrasi. Kila mmoja alikuwa na daraka mbele ya Yehova la kutumia kanuni za Kimaandiko maishani mwake.—Warumi 14:4, 12.
20. Ni nini chaweza kusemwa juu ya theokrasi katika nyakati za baada ya mitume?
20 Paulo alionya kwamba baada ya kifo cha mitume, uasi-imani ungesitawi, ambalo ndilo jambo lililotokea hasa. (2 Wathesalonike 2:3) Wakati ulipopita, idadi ya wale waliodai kuwa Wakristo iliongezeka hadi mamilioni kisha hadi mamia ya mamilioni. Walisitawisha aina tofauti-tofauti za serikali za kikanisa, kama vile utawala wa viongozi wa kidini, wa makasisi, na wa kikutaniko. Hata hivyo, wala mwenendo wala itikadi za makanisa hayo hazikuonyesha utawala wa Yehova. Hizo hazikuwa za theokrasi!
21, 22. (a) Yehova amerudishaje theokrasi katika wakati wa mwisho? (b) Ni maswali gani juu ya theokrasi yatakayojibiwa baadaye?
21 Katika wakati wa mwisho wa mfumo huu wa mambo, kungekuwa na kutenganishwa kwa Wakristo wa kweli kutoka Wakristo bandia. (Mathayo 13:37-43) Hilo lilitokea katika 1919, mwaka wa msingi katika historia ya theokrasi. Wakati huo ule unabii mtukufu wa Isaya 66:8 ulitimizwa: “Ni nani aliyeona mambo kama haya? Je! nchi yaweza kuzaliwa siku moja? Taifa laweza kuzaliwa mara?” Jibu la maswali hayo lilikuwa ndiyo yenye mvumo! Katika 1919 kutaniko la Kikristo lilikuwako mara nyingine tena likiwa “taifa” lililotengwa. Kwa kweli “nchi” ya kitheokrasi ilizaliwa kana kwamba katika siku moja! Wakati wa mwisho ulipoendelea, tengenezo la taifa hilo jipya lilirekebishwa ili kulipatanisha kwa ukaribu zaidi na lile lililokuwako katika karne ya kwanza. (Isaya 60:17) Lakini lilikuwa la theokrasi sikuzote. Katika mwenendo na itikadi, sikuzote liliangaza sheria na kanuni zilizopuliziwa kimungu katika Maandiko. Na sikuzote lilijitiisha kwa Mfalme aliyetawazwa, Yesu Kristo.—Zaburi 45:17; 72:1, 2.
22 Je! wewe hushirikiana na theokrasi hiyo? Je! una cheo cha mamlaka ndani yayo? Ikiwa ndivyo, je, wajua kinachomaanishwa na kutenda kwa njia ya kitheokrasi? Je! wajua ni mitego ipi ya kuepuka? Maswali hayo mawili ya mwisho yatazungumziwa katika makala inayofuata.
Je! Waweza Kueleza?
◻ Theokrasi ni nini?
◻ Israeli lilikuwa la theokrasi katika njia gani?
◻ Yehova alifanya mpango upi ili kuwakumbusha wafalme kwamba Israeli lilikuwa la theokrasi?
◻ Kutaniko la Kikristo lilikuwa la theokrasi katika njia gani, nalo lilipangwaje kitengenezo?
◻ Ni tengenezo jipi la kitheokrasi ambalo limesimamishwa katika wakati wetu?
[Picha katika ukurasa wa 12]
Mbele ya Pontio Pilato, watawala Wayahudi walimkiri Kaisari kuwa mfalme badala ya Mfalme wa Yehova aliyewekwa rasmi kitheokrasi