Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w98 9/1 kur. 13-18
  • Kaa Karibu na Theokrasi

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kaa Karibu na Theokrasi
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Theokrasi ya Kweli Ni Nini?
  • Tengenezo la Kitheokrasi
  • Maoni ya Kitheokrasi Kuhusu Utawala wa Kilimwengu
  • Tanguliza Utukufu wa Mungu
  • “Iweni Waigaji wa Mungu”
  • Yehova Atawala—Kupitia Theokrasi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Wachungaji na Kondoo Katika Theokrasi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Sehemu ya 10: Hatimaye Serikali Kamilifu!
    Amkeni!—1991
  • Kuchunga Pamoja na Muumba Wetu Mtukufu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
w98 9/1 kur. 13-18

Kaa Karibu na Theokrasi

“BWANA ndiye mwamuzi wetu; BWANA ndiye mfanya sheria wetu; BWANA ndiye mfalme wetu.”—ISAYA 33:22.

1. Kwa nini serikali ni jambo linalohangaisha watu walio wengi?

HABARI inayohusu serikali ni yenye kuhangaisha watu sana kwa ujumla. Serikali nzuri huleta amani na ufanisi. Biblia husema: “Mfalme huithibitisha nchi kwa hukumu.” (Mithali 29:4) Kwa upande mwingine, serikali mbaya huongoza kwenye ukosefu wa haki, ufisadi, na ukandamizaji. “Mwovu atawalapo, watu huugua.” (Mithali 29:2) Katika historia yote, wanadamu wamejaribu aina nyingi za serikali, na kwa kusikitisha mara nyingi ‘wemeugua’ kwa sababu ya kukandamizwa na watawala wao. (Mhubiri 8:9) Je, kuna serikali yoyote itakayofanikiwa kuletea raia zake uradhi wenye kudumu?

2. Kwa nini “theokrasi” ni ufafanuzi ufaao wa serikali ya Israeli la kale?

2 Mwanahistoria Josephus alitaja aina ya pekee ya serikali alipoandika: “Vikundi fulani vya watu vimewakabidhi wafalme mamlaka ya juu zaidi ya kisiasa, vingine vikazikabidhi serikali za wachache, ilhali vingine vimeukabidhi umma. Hata hivyo, mpaji-sheria wetu [Musa] hakuvutiwa na aina zozote za serikali hizo, lakini aliipa katiba yake muundo ambao—ikiwa mtu aweza kutumia usemi usio wa kawaida—waweza kuitwa ‘theokrasi,’ akiweka mikononi mwa Mungu enzi kuu na mamlaka yote.” (kichapo Against Apion, II, 164-165) Kulingana na kamusi ya Concise Oxford Dictionary, theokrasi humaanisha “aina fulani ya serikali yenye kuongozwa na Mungu.” Neno hilo halionekani katika Biblia, lakini lafafanua vema serikali ya Israeli la kale. Ingawa Waisraeli walipata kuwa na mfalme mwenye kuonekana, mfalme wao halisi alikuwa Yehova. Nabii Isaya wa Israeli alisema hivi: “BWANA ndiye mwamuzi wetu; BWANA ndiye mfanya sheria wetu; BWANA ndiye mfalme wetu.”—Isaya 33:22.

Theokrasi ya Kweli Ni Nini?

3, 4. (a) Theokrasi ya kweli ni nini? (b) Ni baraka zipi ambazo theokrasi italetea wanadamu wote hivi karibuni?

3 Tangu Josephus abuni neno hilo, mashirika mengi yamefafanuliwa kuwa theokrasi. Baadhi ya hayo yalionekana kuwa yenye kukosa uvumilivu, yenye ushupavu, na yenye kukandamiza kikatili. Je, yalikuwa theokrasi za kweli? Si katika maana ambayo Josephus alitumia neno hilo. Tatizo ni kwamba maana ya “theokrasi” imepanuliwa. Kichapo World Book Encyclopedia hulifasili kuwa “aina ya serikali ambamo taifa linatawalwa na kuhani au makuhani, na ambamo washiriki wa huo ukuhani wana mamlaka katika mambo ya kiraia na ya kidini.” Hata hivyo, theokrasi ya kweli si serikali yenye kuongozwa na makuhani. Kwa kweli huo ni utawala wa Mungu, serikali yenye kuongozwa na Muumba wa ulimwengu, Yehova Mungu.

4 Hivi karibuni, dunia nzima itakuwa chini ya theokrasi, na itakuwa baraka iliyoje! “Mungu mwenyewe atakuwa pamoja na [wanadamu]. Naye atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.” (Ufunuo 21:3, 4) Hakuna utawala wowote wenye kuongozwa na wanadamu wasio wakamilifu uwezao kuleta furaha kama hiyo. Utawala wa Mungu pekee ndio uwezao kufanya hivyo. Kwa sababu hiyo, Wakristo wa kweli hawajaribu kuanzisha theokrasi kwa kuchukua hatua za kisiasa. Wao humngoja Mungu kwa subira aanzishe theokrasi ya ulimwenguni pote katika wakati wake na njia yake mwenyewe.—Danieli 2:44.

5. Ni wapi ambapo theokrasi ya kweli inatenda kazi leo, na ni maswali gani huzushwa kuihusu?

5 Hata hivyo, wakati huuhuu, theokrasi ya kweli inafanya kazi. Wapi? Miongoni mwa wale ambao kwa hiari hujitiisha chini ya utawala wa Mungu na ambao hushirikiana pamoja kufanya mapenzi yake. Waaminifu hao wamekusanywa kuwa “taifa” la kiroho la ulimwenguni pote kwenye “nchi” yake ya kiroho. Wao ni mabaki ya “Israeli wa Mungu” na waandamani wao Wakristo ambao ni zaidi ya milioni tano u nusu. (Isaya 66:8; Wagalatia 6:16) Hao wako chini ya Mfalme wa kimbingu Yesu Kristo, aliyetawazwa na Yehova Mungu, “Mfalme wa umilele.” (1 Timotheo 1:17; Ufunuo 11:15) Tengenezo hilo ni la kitheokrasi katika njia gani? Washiriki wake huionaje mamlaka ya serikali za kilimwengu? Nao wanadamu wenye mamlaka hudumishaje kanuni za kitheokrasi ndani ya jumuiya yao ya kiroho?

Tengenezo la Kitheokrasi

6. Mungu anaweza kutawalaje tengenezo la kibinadamu lenye kuonekana?

6 Yehova ambaye hukaa katika mbingu zisizoonekana anaweza kutawalaje tengenezo la kibinadamu? (Zaburi 103:19) Inawezekana kwa sababu washiriki wake hufuata shauri hili lililopuliziwa: “Mtumaini BWANA kwa moyo wako wote, wala usizitegemee akili zako mwenyewe.” (Mithali 2:6; 3:5) Wao humruhusu Mungu awatawale huku wakishika “sheria ya Kristo” na kutumia kanuni za Biblia zilizopuliziwa katika maisha yao ya kila siku. (Wagalatia 6:2; 1 Wakorintho 9:21; 2 Timotheo 3:16; ona Mathayo 5:22, 28, 39; 6:24, 33; 7:12, 21.) Ili kufanya hivyo, ni lazima wawe wanafunzi wa Biblia. (Zaburi 1:1-3) Kama Waberoya wa zamani “wenye akili ya uelekevu,” wao hawafuati wanadamu bali huthibitisha daima kwamba mambo wanayojifunza yamo katika Biblia. (Matendo 17:10, 11; Zaburi 119:33-36) Kama mtunga-zaburi, wao husali hivi: “Unifundishe akili na maarifa, maana nimeyaamini maagizo yako.”—Zaburi 119:66.

7. Ni upi ulio utaratibu wa usimamizi katika theokrasi?

7 Katika kila tengenezo, ni lazima kuwepo watu fulani wenye mamlaka au wenye kutoa mwelekezo. Ndivyo ilivyo na Mashahidi wa Yehova, nao hufuata muundo wa mamlaka ulioelezwa na mtume Paulo: “Kichwa cha kila mwanamume ni Kristo; nacho kichwa cha mwanamke ni mwanamume; nacho kichwa cha Kristo ni Mungu.” (1 Wakorintho 11:3) Kwa kupatana na hilo, wanaume wanaostahili pekee ndio hutumikia wakiwa wazee makutanikoni. Na ingawa Yesu—“kichwa cha kila mwanamume”—yuko mbinguni, duniani bado kuna “waliobaki” wa ndugu zake watiwa-mafuta, ambao wana tumaini la kutawala pamoja naye mbinguni. (Ufunuo 12:17; 20:6) Wote pamoja hufanyiza “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” Wakristo huonyesha ujitiisho wao kwa Yesu, na hivyo kwa Yehova aliye kichwa cha Yesu, kwa kukubali usimamizi wa “mtumwa” huyo. (Mathayo 24:45-47; 25:40) Katika njia hiyo, theokrasi ina utaratibu. “Mungu ni Mungu, si wa kukosa utaratibu, bali wa amani.”—1 Wakorintho 14:33.

8. Wazee Wakristo hutegemezaje kanuni ya theokrasi?

8 Wazee Wakristo hutegemeza kanuni ya theokrasi kwa sababu wao hutambua kwamba wanawajibika kwa Yehova kuhusiana na jinsi watumiavyo mamlaka yao iliyo ya kiwango kidogo. (Waebrania 13:17) Na wanapofanya maamuzi, wao hutegemea hekima ya Mungu, bali si hekima yao wenyewe. Katika hilo, wao hufuata kielelezo cha Yesu. Yeye alikuwa mtu mwenye hekima zaidi aliyepata kuishi. (Mathayo 12:42) Hata hivyo, aliwaambia Wayahudi hivi: “Mwana hawezi kufanya hata kitu kimoja kwa uanzisho wake mwenyewe, ila tu kile atazamacho Baba akifanya.” (Yohana 5:19) Wazee pia wana mtazamo uleule aliokuwa nao Mfalme Daudi. Alikuwa na mamlaka nzito katika theokrasi. Hata hivyo, alitaka kufuata njia ya Yehova bali si njia yake mwenyewe. Alisali hivi: “Ee BWANA, unifundishe njia yako, na kuniongoza katika njia iliyonyoka.”—Zaburi 27:11.

9. Wakristo walio wakfu wana maoni gani yenye usawaziko kuhusiana na matumaini na mapendeleo tofauti-tofauti ya utumishi katika theokrasi?

9 Watu fulani wametia shaka kama ni jambo la haki kwamba wanaume wanaostahili pekee wawe ndio wenye mamlaka kutanikoni, au kama ni jambo la haki kwamba wengine wawe na tumaini la kimbingu ilhali wengine wana tumaini la kidunia. (Zaburi 37:29; Wafilipi 3:20) Hata hivyo, Wakristo walio wakfu, hutambua kwamba mipango hiyo imeelezwa katika Neno la Mungu. Hiyo ni ya kitheokrasi. Ikiwa mipango hiyo hutiliwa shaka, kwa kawaida wale ambao hawatambui kanuni za Biblia ndio hufanya hivyo. Isitoshe, kuhusiana na wokovu, Wakristo wanajua kwamba wanaume na wanawake ni sawa mbele ya macho ya Yehova. (Wagalatia 3:28) Kwa Wakristo wa kweli, pendeleo lililo kubwa zaidi wawezalo kupata ni kuwa waabudu wa Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu, nao hufurahi kutimiza fungu lolote ambalo Yehova huwaonyesha. (Zaburi 31:23; 84:10; 1 Wakorintho 12:12, 13, 18) Isitoshe, uhai udumuo milele, hata uwe mbinguni au uwe duniani, kwa kweli ni tumaini la ajabu.

10. (a) Yonathani alionyesha mtazamo gani mwema? (b) Wakristo leo huonyeshaje mtazamo sawa na ule wa Yonathani?

10 Hivyo, Mashahidi wa Yehova wako kama Yonathani, mwana mwenye kumhofu Mungu wa Mfalme Sauli. Yaelekea kwamba Yonathani angekuwa mfalme bora kabisa. Hata hivyo, kwa sababu Sauli alikosa kuwa mwaminifu, Yehova alimchagua Daudi awe mfalme wa pili wa Israeli. Je, Yonathani alitiwa uchungu na hilo? La. Alikuwa rafiki mzuri wa Daudi na hata akamlinda na Sauli. (1 Samweli 18:1; 20:1-42) Vivyo hivyo, wale wenye tumaini la kidunia hawawaonei wivu wale wenye tumaini la kimbingu. Nao Wakristo wa kweli hawawaonei wivu wale wenye mamlaka ya kitheokrasi kutanikoni. Badala yake, wao “[huwapa] ufikirio ambao ni zaidi kuliko ule wa kawaida katika upendo,” wakitambua kazi yao ngumu kwa niaba ya ndugu na dada zao wa kiroho.—1 Wathesalonike 5:12, 13.

Maoni ya Kitheokrasi Kuhusu Utawala wa Kilimwengu

11. Wakristo wanaojitiisha chini ya utawala wa kitheokrasi wana maoni gani kuhusu mamlaka za kilimwengu?

11 Ikiwa Mashahidi wa Yehova wako chini ya theokrasi, utawala wa Mungu, wao wana maoni gani kuhusu watawala wa kitaifa? Yesu alisema kwamba wafuasi wake wangekuwa “si sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 17:16) Hata hivyo, Wakristo hutambua deni lao kwa “Kaisari,” serikali za kilimwengu. Yesu alisema kwamba wapaswa “[kulipa] Kaisari vitu vya Kaisari, lakini [kulipa] Mungu vitu vya Mungu.” (Mathayo 22:21) Kulingana na Biblia, serikali za kibinadamu “zimesimama zikiwa zimewekwa na Mungu katika mahali pa vyeo vyazo vyenye kuhusu.” Yehova, yule Chanzo cha mamlaka yote, huruhusu serikali ziweko, naye huzitarajia ziwafanyie mema walio chini ya mamlaka yake. Wafanyapo hivyo, wanakuwa “mhudumu wa Mungu.” Wakristo hujitiisha chini ya serikali ya nchi wanamoishi “kwa sababu ya dhamiri [yao].” (Waroma 13:1-7) Bila shaka, ikiwa nchi ingedai jambo fulani lililo kinyume cha sheria ya Mungu, Mkristo “angem[tii] Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.”—Matendo 5:29.

12. Wakristo wanaponyanyaswa na wenye mamlaka, wao hufuata kielelezo cha nani?

12 Namna gani Wakristo wa kweli wanyanyaswapo na mamlaka za kiserikali? Basi wao hufuata kielelezo cha Wakristo wa mapema, waliovumilia vipindi vya mnyanyaso mkali. (Matendo 8:1; 13:50) Majaribu hayo ya imani yalitarajiwa, kwa kuwa Yesu alikuwa ameonya kwamba yangekuja. (Mathayo 5:10-12; Marko 4:17) Hata hivyo, Wakristo hao wa mapema hawakulipiza kisasi dhidi ya waliowanyanyasa; wala imani yao haikudhoofika chini ya mkazo. Badala yake, walifuata kielelezo cha Yesu: “Alipokuwa akitukanwa, hakuwa akitukana kwa kurudisha. Alipokuwa akiteseka, hakutisha, lakini alifuliza kujikabidhi mwenyewe kwa yeye ambaye huhukumu kwa uadilifu.” (1 Petro 2:21-23) Ndiyo, kanuni za Kikristo zilishinda uchokozi wa Shetani.—Waroma 12:21.

13. Mashahidi wa Yehova wameitikiaje mnyanyaso na kampeni yenye uchongezi dhidi yao?

13 Hali iko hivyohivyo leo. Katika karne hii, Mashahidi wa Yehova wamenyanyaswa sana na watawala wa kidikteta kama vile Yesu alivyotabiri. (Mathayo 24:9, 13) Katika nchi fulani uwongo na masingizio huenezwa na wale wanaojaribu kuwalazimisha wenye mamlaka wachukue hatua dhidi ya Wakristo hao wanyofu. Hata hivyo, licha ya “ripoti mbaya” kama hiyo, Mashahidi hujipendekeza wenyewe kuwa wahudumu wa Mungu kupitia mwenendo mwema. (2 Wakorintho 6:4, 8) Inapowezekana, wao huwasilisha kesi yao kwa maofisa na mbele ya mahakama za nchi, ili wadhihirishe kutokuwa kwao na hatia ya kufanya kosa. Wao hutumia njia zozote zile ziwezazo kupatikana ili kutetea hadharani habari njema. (Wafilipi 1:7) Lakini baada ya kufanya yote wawezayo kupatana na sheria, wao huacha mambo mikononi mwa Yehova. (Zaburi 5:8-12; Mithali 20:22) Kama Wakristo wa mapema, wao hawaogopi kuteseka kwa ajili ya uadilifu ikihitajika.—1 Petro 3:14-17; 4:12-14, 16.

Tanguliza Utukufu wa Mungu

14, 15. (a) Wale wanaotegemeza kanuni ya theokrasi hutanguliza nini? (b) Ni wakati gani ambapo Solomoni aliweka kielelezo chema cha unyenyekevu akiwa katika cheo chake cha usimamizi?

14 Yesu alipowafunza wafuasi wake kusali, alitaja kwanza juu ya kutakaswa kwa jina la Yehova. (Mathayo 6:9) Kwa kupatana na hilo, wanaoishi chini ya theokrasi hutafuta utukufu wa Mungu, bali si utukufu wao wenyewe. (Zaburi 29:1, 2) Biblia yaripoti kwamba katika karne ya kwanza, jambo hilo lilikuwa kikwazo kwa wale waliokataa kumfuata Yesu kwa sababu “walipenda utukufu wa wanadamu,” walipenda kutukuzwa na wanadamu. (Yohana 12:42, 43) Kwa kweli, inahitaji unyenyekevu ili kumtanguliza Yehova badala ya umashuhuri wa mtu binafsi.

15 Solomoni alionyesha mtazamo mzuri kuhusiana na hilo. Linganisha maneno yake wakati wa kuwekwa wakfu kwa hekalu lenye utukufu alilokuwa amejenga, na maneno ya Nebukadneza kuhusu uhodari wake wa kujenga. Kwa majivuno makubwa, Nebukadneza alijisifu: “Mji huu sio Babeli mkubwa nilioujenga mimi, uwe kao langu la kifalme, kwa uwezo wa nguvu zangu, ili uwe utukufu wa enzi yangu?” (Danieli 4:30) Kinyume cha hilo, kwa kiasi Solomoni alidunisha lile alilokuwa ametimiza kwa kusema hivi: “Inawezekana hata Mungu atakaa na watu duniani? Tazama, mbingu na mbingu za mbingu hazikutoshi; si zaidi nyumba hii niliyoijenga!” (2 Mambo ya Nyakati 6:14, 15, 18, Zaire Swahili Bible; Zaburi 127:1) Solomoni hakujikweza. Alijua kwamba yeye alikuwa tu mwakilishi wa Yehova naye akaandika hivi: “Kijapo kiburi ndipo ijapo aibu; bali hekima hukaa na wanyenyekevu.”—Mithali 11:2.

16. Kwa kutojitukuza, wazee wamethibitikaje kuwa baraka ya kweli?

16 Vivyo hivyo, wazee Wakristo humkweza Yehova, bali si wao wenyewe. Wao hufuata shauri hili la Petro: “Ikiwa yeyote ahudumu, acheni ahudumu kama ategemeaye nguvu ambazo Mungu hutoa; ili katika mambo yote Mungu apate kutukuzwa kupitia Yesu Kristo.” (1 Petro 4:11) Mtume Paulo alifafanua “cheo cha mwangalizi” kuwa “kazi bora,” bali si cheo chenye umashuhuri. (1 Timotheo 3:1) Wazee huwekwa rasmi ili kutumikia, bali si kutawala. Wao ni walimu na wachungaji wa kundi la Mungu. (Matendo 20:28; Yakobo 3:1) Wazee wanyenyekevu na wenye kujidhabihu ni baraka ya kweli kwa kutaniko. (1 Petro 5:2, 3) “Fulizeni kuwachukua watu wa namna hiyo kuwa wenye thamani kubwa,” na kumshukuru Yehova kwa kuwa ameandaa wazee wengi wanaostahili ili wategemeze theokrasi katika “siku [hizi] za mwisho.”—Wafilipi 2:29; 2 Timotheo 3:1.

“Iweni Waigaji wa Mungu”

17. Walio chini ya theokrasi humwiga Mungu katika njia zipi?

17 Mtume Paulo alihimiza: “Iweni waigaji wa Mungu, mkiwa watoto wapendwa.” (Waefeso 5:1) Wale wanaojitiisha chini ya theokrasi hujaribu kuwa kama Mungu kwa kadiri iwezekanavyo kwa wanadamu wasio wakamilifu. Kwa mfano, Biblia husema hivi kumhusu Yehova: “Yeye Mwamba, kazi yake ni kamilifu; maana njia zake zote ni haki. Mungu wa uaminifu, asiye na uovu, yeye ndiye mwenye haki na adili.” (Kumbukumbu la Torati 32:3, 4) Ili kumwiga Mungu katika hilo, Wakristo hutafuta kuwa waaminifu, waadilifu, na wenye usawaziko katika haki. (Mika 6:8; 1 Wathesalonike 3:6; 1 Yohana 3:7) Wao huepuka mambo mengi ambayo yamekubaliwa katika ulimwengu, kama vile ukosefu wa adili, kutamani na pupa. (Waefeso 5:5) Kwa kuwa watumishi wa Yehova hufuata viwango vya Mungu bali si vya wanadamu, tengenezo lake ni la kitheokrasi, safi, na lenye kujenga.

18. Ni ipi iliyo sifa yenye kutokeza zaidi ya Mungu, na Wakristo huionyeshaje sifa hiyo?

18 Upendo ndiyo sifa yenye kutokeza zaidi ya Yehova Mungu. “Mungu ni upendo,” mtume Yohana asema. (1 Yohana 4:8) Kwa kuwa theokrasi humaanisha utawala wa Mungu, basi neno hilo humaanisha utawala wa upendo. Yesu alisema: “Kwa hilo wote watajua kwamba nyinyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo miongoni mwenu wenyewe.” (Yohana 13:35) Tengenezo la kitheokrasi limeonyesha upendo wenye kutokeza katika siku hizi ngumu za mwisho. Wakati wa zogo la uangamizaji wa jamii katika Afrika, Mashahidi wa Yehova walionyesha upendo kwa wote, haidhuru walikuwa wa kikundi gani cha kikabila. Wakati wa vita katika Yugoslavia ya zamani, Mashahidi wa Yehova kutoka maeneo yote walisaidiana, huku vikundi vinginevyo vya kidini vikishiriki katika ule uitwao utakaso wa kikabila. Katika maisha yao ya kibinafsi, Mashahidi wa Yehova hujitahidi kushika shauri hili la Paulo: “Acheni uchungu wote wenye nia ya kudhuru na hasira na hasira ya kisasi na kupiga kelele na usemi wenye kuudhi viondolewe mbali kutoka kwenu pamoja na ubaya wote. Bali iweni wenye fadhili nyinyi kwa nyinyi, wenye huruma kwa njia nyororo, mkisameheana kwa hiari mtu na mwenzake kama vile Mungu pia kupitia Kristo alivyowasamehe nyinyi kwa hiari.”—Waefeso 4:31, 32.

19. Wale wanaojitiisha chini ya theokrasi wanapata baraka zipi leo na vilevile wakati ujao?

19 Wale ambao hujitiisha chini ya theokrasi hufurahia baraka nyingi. Wana amani pamoja na Mungu na Wakristo wenzao. (Waebrania 12:14; Yakobo 3:17) Wana kusudi maishani. (Mhubiri 12:13) Wana usalama wa kiroho na tumaini hakika la wakati ujao. (Zaburi 59:9) Kwa kweli, wao hufurahia mwonjo wa kimbele wa vile itakavyokuwa wakati ambapo wanadamu wote watakuwa chini ya utawala wa kitheokrasi. Hivyo basi, Biblia husema, “hawatadhuru wala hawataharibu katika mlima wangu wote mtakatifu; maana dunia itajawa na kumjua BWANA, kama vile maji yanavyoifunika bahari.” (Isaya 11:9) Huo utakuwa wakati mtukufu kama nini! Sote na tuhakikishe kwamba tutakuwa katika Paradiso hiyo ya wakati ujao kwa kukaa karibu na theokrasi sasa.

Je, Waweza Kueleza?

◻ Theokrasi ya kweli ni nini nayo hupatikana wapi leo?

◻ Wanadamu hujitiishaje chini ya utawala wa kitheokrasi maishani mwao?

◻ Wale walio chini ya theokrasi hutafuta kutanguliza utukufu wa Mungu badala ya utukufu wao wenyewe katika njia zipi?

◻ Wale wanaotegemeza theokrasi huiga sifa zipi za kimungu?

[Picha katika ukurasa wa 17]

Solomoni alitanguliza utukufu wa Mungu badala ya utukufu wake mwenyewe

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki