Maana ya Habari za Leo
TAZAMA gazeti au fungua televisheni. Unasoma, kusikia, au kuona nini? Habari za mauaji, wanawake kulalwa kinguvu, madawa ya kulevya, kuvunjika kwa familia, mapinduzi ya serikali, maasi, kashifa, udanganyifu, maradhi kama vile UKIMWI, matetemko ya dunia, njaa, kukosa chakula. Hizo ndizo habari za kila siku zisizobadilika. Hata hivyo, upande wenye muhimu wa habari hizo hupuuzwa kwa ujumla, na hata ukitajwa, unasahauliwa upesi.
Kwa kielelezo, wakati wa kipindi chake cha kwanza akiwa rais wa U.S., Ronald Reagan alinena juu ya “Har-magedoni,” akisema: “Najikuta nikijiuliza—kama sisi ndicho kizazi kitakachoona hilo likitukia.” Hata hivyo, baadaye, alipunguza uzito wa jambo hilo, akisisitiza kwamba yeye hakusema kamwe kwamba “ni lazima tupange kulingana na Har-magedoni.”
Hata hivyo, kitabu cha Biblia cha Ufunuo hutuambia juu ya kuja kwa Har–Magedoni, kikieleza kwamba “wafalme wa dunia na wa ulimwengu wote” watakusanywa “kwenye pigano la ile siku kuu ya Mungu Mweza Yote.” Ikiendelea, Biblia yasema kwamba mataifa yatakusanywa “pamoja kwenye mahali paitwapo katika lugha ya Kiebrania Har–Magedoni.”—Ufunuo 16:14, 16, King James Version.
Pigano hilo lenye kutikisa dunia la ile siku kuu ya Mungu Mweza Yote litatukia lini? Je! yaweza kuwa ni katika wakati wetu? Hata Ronald Reagan alichochewa kueleza hivi: “Sijui kama nyinyi mmeona wowote wa unabii huo mbalimbali karibuni, lakini, hakika yangu, unaeleza nyakati tunazozipitia bila shaka.”
Habari Zenye Umaana Mkubwa
Jiangalilie unabii wa Biblia ufuatao: “Jua hili, kwamba katika siku za mwisho [za huu mfumo wa mambo] nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo zitakuwa hapa. Kwa maana watu watakuwa wajipenda wenyewe, wapenda fedha, wenye kimbelembele, wenye kujigamba, wakufuru, wasiotii wazazi, wasio na shukrani, wasio washikamanifu, wasio na shauku ya asili, wasiotaka kufanya mwafaka wowote, wachongezi, bila kujiweza, wakali, bila upendo wa wema, wasaliti, wenye kichwa kigumu, wenye kuvimbishwa kwa kiburi, wapenda raha kuliko kuwa wapenda Mungu, wenye ujitoaji kimungu lakini wakithibitika kuwa mabandia kwa nguvu zao; na kutoka hao geukia mbali.” (2 Timotheo 3:1-5, NW) Je! wewe ungeweza kusema unabii huo unatimizwa sasa?
Na zaidi, alipokuwa akieleza juu ya kuwapo kwake kwa wakati ujao na umalizio wa mfumo wa mambo, Yesu alitabiri hivi: “Mtasikia juu ya vita na ripoti za vita . . . Kwa maana taifa litainuka dhidi ya taifa na ufalme dhidi ya ufalme, na kutakuwako upungufu wa chakula na matetemeko ya dunia mahali hapa na mahali hapa. . . . Na kwa sababu ya ongezeko la uhalifu wa sheria upendo wa walio wengi utapoa.” (Mathayo 24:3-12, NW) Je! wewe hukubali pia kwamba unabii huo unatimizwa?
Kusudi wafuasi wake ambao wangekuwa wakiishi wakati wa utimizo wa unabii huo mbalimbali wathamini maana yao halisi, Yesu alitoa kielezi hiki: “Utazameni mtini na miti mingine yote. Wakati iishapo kuchipuka, mwaona na kutambua wenyewe ya kwamba majira ya mavuno yamekwisha kuwa karibu. Nanyi kadhalika, mwonapo mambo hayo yanaanza kutokea [kwa kweli, matukio yale yale tunayoona yakitukia leo], tambueni ya kwamba ufalme wa Mungu u karibu.”—Luka 21:29-31.
Hakika, ushuhuda ni tele kwamba tunaishi wakati ambao kuja kwa Ufalme wa Mungu na vita yake ya Har–Magedoni ni karibu sana! ingawa habari hiyo ya muhimu imepuuzwa kabisa na vyanzo vya habari vya ulimwengu, Mashahidi wa Yehova wanashiriki katika kuieneza ulimwenguni pote. Habari njema hizo wanazoeleza si kwamba tu Mungu atasafisha upotovu wote duniani bali pia kwamba, chini ya utawala wa serikali ya Ufalme, dunia yote itafanywa kuwa paradiso ya kupendeza iliyo mfano wa bustani.
Kuhusu mambo hayo, Biblia yaahidi hivi: “Maana wanyofu watakaa katika nchi, na wakamilifu watadumu ndani yake. Bali waovu watatengwa na nchi, nao wafanyao hila watang’olewa.” Na tena: “Wenye upole watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani. Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.”—Mithali 2:21, 22; Zaburi 37:11, 29.
Je! wewe ungependa kujua vizuri zaidi kuhusu ushuhuda wa kwamba utimizo wa huo unabii mbalimbali mtukufu umekaribia sana? Ikiwa ndivyo, wajulishe Mashahidi wa Yehova. Wao watafurahi kukusaidia utambue kwamba habari za leo zamaanishia kikweli kwamba Ufalme wa Mungu u karibu, ndiyo, kwamba ulimwengu mpya wa uadilifu umekaribia.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 9]
Nordhausen/kambi ya watumwa: USAF Official Photo; Mtoto anayekufa njaa: WHO photo by W. Cutting; Kiwanda: WHO photo by P. Almasy