Vijana wa Leo—Matatizo Wanayokabili
“UCHUNGUZI waonyesha kwamba bila shaka miaka ya ujana ni miongoni mwa nyakati zile zenye kuvuruga na kutoa mkazo zaidi maishani.” Ndivyo alivyoandika Dakt. Bettie B. Youngs katika kitabu chake Helping Your Teenager Deal With Stress. Katika nyakati zilizopita, kule kuwa wachanga tu kuliwashughulisha mno vijana. Hata hivyo, siku hizi, ni lazima wakabiliane na magumu ya ubaleghe na msongo mkubwa mno wa maisha ya mtu mzima katika miaka ya 1990.
Dakt. Hebert Friedman aliandika hivi katika gazeti World Health: “Ule mgeuko wa kutoka kuwa mtoto na kuwa mtu mzima haujapata tena kutukia katika kipindi chenye badiliko kubwa hivyo, iwe ni ongezeko lisilo la kawaida katika idadi ya watu wa ulimwengu, mwendo wa kasi wa kufanyizwa kwa miji ambao umeambatana nalo, na mabadiliko makubwa ya kitekinolojia katika mawasiliano na usafiri ambayo ni kama kwa usiku kucha yamefanyiza hali ambazo hazijapata kuonwa tena.”
Kwa hiyo, msichana mmoja kijana aitwaye Kathy asema hivi: “Ni vigumu mno kukulia katika wakati kama wetu.” Uzoevu wa madawa ya kulevya, kujiua, matumizi mabaya ya alkoholi—hivyo ndivyo vijana fulani wanakabiliana na ile mikazo na mivuto ya hizi “nyakati za hatari ngumu kushughulika nazo.”—2 Tim. 3:1, NW.
Badiliko Katika Familia
Dakt. Youngs akumbuka hivi: “Wazazi wetu walikuwa na wakati kwa ajili yetu. Wengi wetu walikuwa na mama ambao kazi-maisha yao ya wakati wote ilikuwa ni kulea watoto.” Lakini leo, “wanawake wengi hawawezi au hawataki kukaa nyumbani na kulea watoto wao wakati wote. Wanafanya kazi na wanalazimika kuchanganya kazi-maisha na familia. Hakuna saa za kutosha katika siku; lazima kitu fulani kipotee. Mara nyingi, kinachopotea ni wakati na tegemezo ambalo mzazi aweza kumpa mtoto wake. Katika wakati wa kunyumbuka utu zaidi maishani, kijana anaachwa peke yake akabiliane na mabadiliko ya kimwili, kiakili, na kihisia-moyo.”—Helping Your Teenager Deal With Stress.
Bila shaka miaka ya 1990 itaendelea kuona miundo ya familia ikigeuzwa sana na talaka (asilimia 50 za ndoa katika United States humalizikia katika talaka), watoto haramu kuzaliwa, na mtindo wenye kuongezeka wa watu wawili kuishi pamoja ijapokuwa hawajafunga ndoa. Tayari, karibu 1 kwa kila familia 4 katika United States inaongozwa na mzazi mmoja. Hesabu yenye kuongezeka ya familia ni familia za kambo zinazoundwa kwa ndoa kufungwa upya.
Je! watoto katika miundo hiyo ya familia wamo katika hatari ya kupata hasara ya kuumizwa kihisia-moyo au kisaikolojia? Kwa kielelezo, watu fulani hudai kwamba watoto katika nyumba zenye mzazi mmoja wanaelekea sana kuwa wenye upweke, huzuni, na kukosa usalama zaidi ya vijana waliolelewa katika familia za kikawaida. Ni kweli, familia nyingi zenye mzazi mmoja na za familia ya kambo huendelea zikiwa na mzoroto mdogo unaoonekana kwa watoto. Hata hivyo, Maandiko yaonyesha wazi kwamba Mungu alikusudia watoto walelewe na wazazi wawili. (Waefeso 6:1, 2) Haikosi kuacha hali hiyo inayofaa lazima kulete mkazo na mvuto wa ziada.
Badiliko katika maisha ya familia laendelea pia katika mabara mengi yanayositawi. Huko, muundo wa kawaida ulikuwa ni familia iliyopanuliwa, ambamo katika hiyo washiriki wote wa familia walio watu wazima walishiriki katika kulea watoto. Kufanywa kwa miji na kuanzishwa kwa viwanda kunapunguza sana vifungo vya familia iliyopanuliwa—na mminiko wa tegemezo linalohitajiwa na vijana.
Aandika hivi mwanamke Mwafrika mmoja kijana: “Hakuna akina shangazi wala mtu mwingine wa ukoo wa kunishauri juu ya yanayohusika katika kukua. Wazazi hutazamia habari hiyo ishughulikiwe shuleni—nayo shule yaachia wazazi jambo hilo. Lile wazo la watoto kuwa mali ya jumuiya halipo tena.”a
Mahangaiko ya Kiuchumi
Pia vijana huhisi kuhangaishwa sana na uchumi wa ulimwengu unaoharibika. Kwa kweli, vijana 4 kati ya kila 5 huishi katika mabara yanayositawi na waelekewa na mataraja ya umaskini wa muda wote wa maisha na ukosefu wa kuajiriwa. Asema hivi Luv mwenye miaka 17, mkaaji wa India: “Miongoni mwa vijana katika nchi yetu, kwa wakati huu kuna ukosefu mkubwa wa kuajiriwa, kwa hiyo je! inashangaza kwamba vijana wanakuwa wagonjwa na kukosa furaha, kunaswa na maovu, kutoroka nyumbani au hata kujiua?”
Vijana katika Magharibi yenye utajiri wana wasiwasi wao wenyewe wa pesa. Kwa kielelezo, fikiria uchunguzi mmoja wa U.S. wa vijana ulioripotiwa katika gazeti Children Today: “Walipoulizwa juu ya habari hususa zilizowahangaisha, vijana walielekea kutambulisha masuala yaliyohusu pesa na wakati ujao.” Miongoni mwa mahangaiko kumi ya kwanza ya vijana yalikuwa ni “kugharimia chuo,” “nchi kuelekea kwenye anguko [la kiuchumi],” na “kutochuma za kutosha.”
Hata hivyo, kinyume cha hilo wataalamu fulani huamini kwamba hata vijana wenye hali bora ya kifedha wataumia baada ya muda mrefu. Gazeti Newsweek lilionelea hivi: “Kufikia [miaka ya] 80, watatu kati ya wanadarasa wanne [wa U.S.] wa shule ya upili walikuwa wakifanya kazi wastani wa saa 18 kwa juma moja na mara nyingi wakienda nyumbani na zaidi ya $200 kwa mwezi”—yawezekana ni pesa zaidi za matumizi kushinda walizokuwa nazo wazazi wao! Kama ambavyo ingeweza kujuliwa kimbele, “mapato hayo yalitumiwa mara moja kwenye motokaa, mavazi, vinanda na vyombo vingine vya maisha ya starehe ya ubaleghe.”
Mwandishi Bruce Baldwin aonyesha kwamba vijana hao “hukua wakiwa na matazamio . . . ya kwamba maisha ya starehe yatakuwapo daima wayatakapo wawe watasitawisha kujiona wana daraka na mchocheo wa kutimiza jambo au la.” Lakini wao “hushtuka sana wanapoondoka nyumbani. Mazingira ya nyumbani yasiyo halisi huenda kwa kweli yakatofautiana sana na matazamio halisi ya kazi ya kuajiriwa na matakwa ya utendaji wa utu mzima uliokomaa hivi kwamba waweza kupatwa na jambo linalokaribia kuwa mgutuo wa kitamaduni.”
Orodha za Adili na Thamani Zenye Kubadilika
Mabadiliko makubwa katika adili na thamani nyinginezo pia ni vyanzo vya mvurugo miongoni mwa vijana. “Ngono . . . katika siku za nyanya yangu ni jambo ambalo halikusikika,” asema Ramani, mwanamke mmoja kijana kutoka Sri Lanka. “Ngono katika ndoa haikuzungumzwa, hata katika familia au pamoja na daktari, na ngono nje ya ndoa haikuwapo.” Hata hivyo, miiko ya kale imetokomea kabisa. “Ngono ya vijana ni kama imekuwa njia ya maisha,” aripoti.
Haishangazi kwamba wakati uchunguzi mmoja ulipofanywa wa wanafunzi 510 wa shule ya upili katika United States, hangaiko lao la pili lilikuwa “kwamba huenda wakaambukizwa UKIMWI”! Lakini sasa kwa kuwa mlango wa “adili mpya” umefunguliwa, ni vijana wachache wanaoonekana wana nia ya kuchukua kwa uzito maongezi yoyote ya kuufunga kwa kuwa na zoea la kuwa na mwenzi mmoja—achia mbali kusubiri hadi kufunga ndoa. Ni kama alivyouliza kijana mmoja Mfaransa: “Wakati wa umri wetu, je! twaweza kuahidi kuwa waaminifu maisha yetu yote?” Kwa hiyo UKIMWI na maradhi mengine ya kuambukizana yataendelea kutishia uhai na afya ya vijana wengi.
Wakati Ujao wa Aina Gani?
Vijana wana tatizo jingine lenye kuwasumbua. Taraja la kurithi dunia iliyoharibiwa—anga layo likiwa limemalizwa ozone (ile sehemu ya anga inayozuia miale yenye kudhuru ya jua), hali-joto zayo zikipanda juu kwa sababu ya kiwango kile kile cha joto kotekote, misitu yayo ya kijani-kibichi ikiwa imefyekwa, hewa na maji yayo vikiwa havifai kupumuliwa na kunywewa—hutia wasiwasi vijana wengi. Ijapokuwa linapungua, tishio la vita ya nyukilia hufanya wengine waulize ikiwa ainabinadamu watakuwa na wakati ujao achilia mbali mengine!
Basi, ni wazi kwamba vijana leo wanakabili matatizo makubwa sana. Bila msaada, mwelekezo, na uongozi, furaha yao ya wakati huu na wakati ujao inahatarishwa sana. Na bila ya tumaini la wakati ujao, hakuna hisia yoyote ya usalama inayoweza kupatikana. Kwa kupendeza, msaada unapatikana kwa utayari kwa vijana wa leo.
[Maelezo ya Chini]
a Hili pamoja na manukuu mengineyo kutoka kwa vijana katika mabara yanayositawi yametolewa katika toleo la Machi 1989 la gazeti World Health.
[Picha katika ukurasa wa 6]
Kuvunjika kwa familia nyingi kupitia talaka na mtengano kumenyima vijana wengi tegemezo linalohitajiwa la mzazi