Vijana wa Leo—Kukabiliana na Matatizo ya Miaka ya 1990
NOVEMBA 1985. Waheshimiwa kutoka mabara 103 walikusanyika kwenye makao makuu ya Umoja wa Mataifa ili watokeze “mbinu ya duniani pote ya kusuluhisha matatizo ya vijana wa ulimwengu.”—UN Chronicle.
Miaka mitano imekwisha, na matatizo ya ujana yanakuwa makubwa zaidi ya wakati mwingineo wote. Migongano ya falsafa ya kisiasa, ukosefu mkubwa wa fedha, na kubadilika-badilika kwa mambo yanayoonwa kuwa ya muhimu kumevuruga majaribio yenye nia nzuri ya serikali ya kufanya kazi pamoja kwa niaba ya vijana.
Vilevile dini imeshindwa kuwa nguvu ya kutokeza wema. Uchunguzi wa karibuni wa Gallup katika United States wafunua kwamba ingawa hesabu kubwa ya vijana (karibu asilimia 90) huamini Mungu (au roho ya ulimwenguni pote), ni wachache sana wanaofikiria dini kuwa yenye maana maishani mwao. Kuongezea hayo, dini imefanya machache au haikufanya chochote ili kuzuia tabia ya ngono ya ovyo-ovyo.
Kisha wapo wale waitwao ati wataalamu—wasaikolojia, wasosholojia, washauri, na watu wa namna hiyo—wanaotoa ushauri kwa vijana. Mwingine wao ni timamu na wenye kusaidia. Hata hivyo, ushauri wao, huelekea kukazia mahangaiko ya kimwili: magumu ya kiuchumi ya mimba ya ujana, kuepuka UKIMWI, hatari za kimwili za matumizi mabaya ya madawa ya kulevya. Ni mara chache, zikiwapo, wakabilianapo na masuala ya adili yanayohusika ambayo ni ya maana zaidi. “Wataalamu” hao kwa ujumla huridhika na kufuata maoni yanayopendwa na wengi ya miendo ya wakati huu au kurudia misemo yenye kuvutia, kama vile “Ngono salama” au “Sema la tu!”
Vipi wazazi? Walio wengi mno wanashughulishwa na shughuli yao ya kuishi. Wakiwa hawajioni salama au bila kustareheka kuzungumza mambo yenye kutaka uangalifu, wazazi wengi huelekea kusita wakati masuala yenye kutokeza haya yanapozuka. Basi, haishangazi sana kwamba vijana wengi hugeukia marika wao wasio na ujuzi wapate msaada.
Chanzo Bora Zaidi cha Msaada kwa Vijana
Basi, vijana wanawezaje kupata majibu yanayotumika kwa maswali yanayowasumbua? Maswali kama vile: ‘Je! nijaribu madawa ya kulevya na alkoholi?’ ‘Vipi juu ya ngono kabla ya ndoa?’ ‘Nijueje kama ni upendo halisi?’ ‘Wakati ujao umeniwekea nini?’
Huenda ikashangaza wengine kusikia kwamba chanzo bora zaidi cha ushauri kwa ajili ya vijana ni Neno la Mungu, Biblia. Ati Biblia? Ndiyo, ina mengi ya kuwaambia vijana. (Ona Mithali, sura 1-7; Waefeso 6:1-3.) Kuongezea hayo, ilipuliziwa na Muumba wetu, ambaye anajua sana “tamaa zenye msukosuko za ujana.” (2 Timotheo 2:20-22, Phillips; 3:16) Kabla ya kulitupilia mbali wazo la kwamba kitabu hiki cha kale kingeweza kuwa chafaa maisha ya miaka ya 1990, fikiria hili: Je! yaelekea kwamba ushauri ulio mwingi unaotolewa na “wataalamu” wa leo utasomwa na kustahiwa miaka 50 kutoka sasa? Hata hivyo, Biblia yaendelea kuchukuliwa kwa uzito maelfu ya miaka baada ya kuandikwa!
Ni kweli, jumuiya ya kibinadamu imebadilika sana tangu nyakati za Biblia, lakini asili ya kibinadamu haikubadilika. Kwa msingi tamaa za ujana ni zile zile. Kwa hiyo Biblia ni ya wakati huu kama katika wakati mwingineo wote. Nayo hushughulika na msingi wa matatizo yaliyo mengi yanayohusu vijana leo. Wakati uo huo, hiyo hutolea vijana tumaini kwa ajili ya wakati ujao.
Kwa kuwa Biblia yatoka kwa Muumba wetu, tungetazamia shauri layo liwe lenye kufanya kazi, lenye kutumika. Mambo ya kweli ya maisha waliyojionea maelfu ya vijana Wakristo leo, wanaofuata ushauri wa Biblia, huthibitisha ndivyo ilivyo! Ili kuwasaidia vijana, Watch Tower Society imetangaza kitabu kiitwacho Questions Young People Ask—Answers That Work. Kinatia mambo mengi yanayohusu vijana, na shauri lacho lategemea Biblia daima! Itikio lenye idili la wasomaji vijana wa kitabu hiki lathibitisha si tokeo lenye mafaa la maagizo ya Biblia tu bali pia uhakika wa kwamba vijana wataka na hufaidiwa na mwelekezo wa Biblia. Makala ifuatayo yatoa baadhi ya semi za kutoka moyoni zilizosemwa na vijana kutoka ulimwenguni pote.
Uwe wewe ni mchanga au mzee, unajiwia kuzoeleana na Biblia. Mashahidi wa Yehova wamesaidia mamilioni wafanye hivyo kupitia mpango wa funzo la Biblia nyumbani, nao wangefurahi sana kukusaidia. Kwa kuzoeleana na shauri la Biblia na kulitumia, vijana wanaweza kujifunza si masuluhisho tu yenye kutumika ya matatizo ya leo bali pia njia ya kupata kibali cha Mungu, ambaye hualika vijana wamtumikie.—Mhubiri 12:1.