Vijana Hupendezwa na Dini Kadiri Gani?
NA MLETA-HABARI WA AMKENI! KATIKA UFARANSA
KWA vijana 750,000 waliohudhuria, hii ingekuwa jioni ya kufurahisha sana. Walipunga bendera, wakaimba na kushangilia. Miale na fataki zilirushwa hewani na wanamuziki wakachangamsha umati. Hali ilifanana na “disko kubwa sana iliyopangwa kwa haraka.” Hatimaye, kukiwa na vigelegele vya usifaji, mtu waliyekuwa wamemngoja akatokea jukwaani.
Je, huu ulikuwa mwanzo wa safari ya kuzuru ulimwengu wote ya bendi ya roki? La. Ulikuwa mkutano wa kidini uliohudhuriwa na umati mkubwa katika Paris wakati wa Siku za Vijana Wakatoliki Ulimwenguni, na mtu mwenyewe alikuwa Papa John Paul wa Pili!
Kwa watu wengine, kupendezwa kwa vijana na misherehekeo ya kidini kama hii laonekana kuwa jambo la kustaajabisha. Lakini sasa vyombo vya habari vinazungumzia hali ya vijana kupenda dini tena.
Kuonekana kwa Nje
Bila kuangalia kwa undani, dini yaweza kuonekana kuwa inasitawi. Karibu asilimia 68 ya vijana wa Ulaya wanasema kwamba wao ni wa dini fulani, na katika Ireland takwimu hii huzidi asilimia 90. Katika Armenia, ambayo zamani ilikuwa jamhuri ya muungano wa Sovieti ambapo watu wengi wakati mmoja waliiona dini kuwa kitu cha kale, kasisi mmoja alisema hivi kuhusu makanisa yaliyokuwa matupu na ambayo sasa yamejaa watu: “Ninashangazwa na jinsi dini inavyowavutia vijana.”
Katika nchi nyingi vyombo vya habari vimetangaza sana kujihusisha kwa vijana katika madhehebu na vikundi vyenye kuhubiri kwa nguvu. Misherehekeo ya kidini kama ile iliyotajwa mwanzoni mwa makala hii, inapendwa sana. Lakini, twapata nini tunapochunguza dini kwa makini?
Kuchunguza kwa Makini
Uchunguzi wa makini unafunua kwamba katika mwaka wa 1967, asilimia 81 ya vijana Wafaransa waliamini katika Mungu, lakini katika mwaka wa 1997, asilimia hiyo ilikuwa chini ya nusu. Katika Ulaya yote, ni asilimia 28 tu ya vijana ambao huamini kuwa Mungu ni mtu halisi. Basi haishangazi kwamba ni asilimia 12 tu ya vijana wa Ulaya ambao huomba mara nyingi. Jambo hili linadhihirishwaje na mtazamo wa vijana kuelekea dini?
Katika Denmark asilimia 90 ya vijana husema kwamba wao ni wa dini ya taifa. Ni asilimia 3 tu kati ya hao wanaojiona kuwa washiriki wa kawaida. Katika mwaka wa 1997 mahoji yaliyofanywa na La Croix, gazeti la Kikatoliki katika Ufaransa, yalionyesha kwamba asilimia 70 ya vijana Wafaransa hukiri kwamba dini haiathiri maisha yao kwa vyovyote. Robo tatu kati yao huongozwa na ujuzi wao kuliko kuongozwa na mafundisho ya dini. Ndivyo hali ilivyo katika nchi nyingi za Ulaya.
Kwa nini vijana wanaacha makanisa? Wengi wao hawana imani na dini kubwa-kubwa. Mathalani, katika Ufaransa, vijana wengi hufikiri kwamba dini ndiyo husababisha mgawanyiko ulimwenguni. Kwa kuongezea, ni kawaida kupata vijana ambao huhisi kama Judith mwenye umri wa miaka 15, ambaye ni Mkatoliki kutoka Hispania. Asema hivi: “Mimi sikubaliani na mafundisho ya kanisa kuhusu adili.” Vivyo hivyo, Joseph mwenye umri wa miaka 20 kutoka Taiwan, huona dini kuwa “ya kidesturi sana.” Ikiwa vijana wengi hawakubaliani na mafundisho ya dini yao, basi wao huamini nini?
Kuchagua Dini Uipendayo
Sasa kwa kawaida vijana wengi huchagua itikadi za kidini kama wachaguavyo milo kwenye menyu. Gazeti moja liliita zoea hili la kidini “practice à la carte.” Gazeti moja la Kikatoliki lililirejezea kuwa “kutazama dini kwa mbali bila kujihusisha nayo.” Mawazo yaliyoonwa kuwa ya zamani sasa ni ya kawaida. Hivyo, katika Ulaya karibu asilimia 33 ya vijana huamini hirizi za bahati nzuri asilimia 40 huamini kwamba wapiga ramli wanaweza kutabiri wakati ujao, na asilimia 27 huamini kwamba nyota huongoza maisha za watu. Mawazo kama vile kuzaliwa upya katika umbo jingine sasa huaminiwa na vijana wengi wa Ulaya.
Kuna unamna-namna wa itikadi za kidini hivi kwamba vijana wanaweza kuchagua mawazo wayapendayo. Wachache huamini kwamba dini moja ndiyo ya kweli. Wakiwa na uhuru wa kuchagua itikadi wapendazo, kuna tofauti ndogo sana katika itikadi za kidini miongoni mwa vijana. Sasa wanasosholojia wanazungumzia “kufutwa hatua kwa hatua” au “kuondolewa kwa ujumla” kwa imani rasmi. Katika hali hii ya kiroho, dini za zamani zinafanyaje?
Jitihada ya Vijana ya Kuchunguza Dini
Dini zinapata ugumu wa kuvutia vijana. Kasisi Mfaransa aliuliza umati uliokuwa ukihudhuria Siku za Vijana Wakatoliki Ulimwenguni katika Paris hivi: “Vijana hawa wametoka wapi? Hakuna vijana katika makanisa yangu. Siwaoni kamwe.” Ili kuvutia na kudumisha uangalifu wa vijana, Kanisa Katoliki linahitaji kubadili namna ya mahubiri yake na namna linavyoonekana.
“Kanisa labadili mtindo wake!” likatangaza gazeti la Kifaransa Le Figaro. Kwa msherehekeo wa 12 wa Siku za Vijana Ulimwenguni katika Paris, kanisa lilitumia mashirika ambayo yana uzoefu wa kupanga maonyesho ya muziki wa roki yasimamie maonyesho haya. Kulikuwa na maonyesho zaidi ya 300 ya kutumbuiza vijana waliozuru kutoka zaidi ya nchi 100, na hasa makasisi wakashonewa mavazi ya kimtindo.
Kwa kukosa kuwaelewa vijana wa leo na kuona uhitaji wa kubadilika, dini nyingi zinakuwa na imani zinazohusisha kila aina ya watu. Akidhihirisha sera hii, Michel Dubost, kasisi aliyepanga Siku za Vijana Ulimwenguni katika Paris, alisema hivi: “Bila shaka ningependa wote waliobatizwa wawe waaminifu kwa Kristo. Lakini hata ikiwa si waaminifu, wanakubalika kanisani.”
Vijana Watafuta Majibu
Likikazia kwamba kwa kweli vijana wanatafuta majibu, gazeti moja la habari lilifafanua hudhurio la vijana kwenye msherehekeo katika Paris kuwa “ombi la kutaka imani badala ya wonyesho wa imani.” Je, ombi hilo lilijibiwa na Kanisa Katoliki?
Unapochunguza ndani badala ya nje au kuchunguza kile kilichoitwa na gazeti moja la habari la Kikatoliki kuwa “njozi za uongo” za misherehekeo mikubwa ya kidini, unapata nini? Gazeti la habari la Kifaransa Le Monde lilieleza kwamba kwa ndani kuna “ukosefu wa uradhi wa kweli.”
Ingawa namna chakula kionekanavyo ni jambo la maana, chakula chapaswa kuwa chenye lishe. Maswali ya vijana kuhusu kusudi la maisha huhitaji majibu yenye kuimarisha kiroho. Vijana hawaridhishwi na majibu wanayopewa yenye kupendeza lakini yasiyokuwa na maana.
Je, matukio ya kidini yasiyokuwa na maana yoyote yanawaathiri vijana wa leo kwa kudumu? Mwanasosholojia Mfaransa Danièle Hervieu-Léger alisema hivi: “Matukio haya yaliyopangwa vizuri ajabu hayawezi kutokeza athari za kijamii za kudumu.” Basi ni wapi vijana wawezapo kupata majibu yenye kuridhisha kwa maswali yao?
Majibu Yenye Kuridhisha
Katika mwaka wa 1997 gazeti la Kifaransa Le Point lilichapisha makala kuhusu magumu wanayokabili vijana. Kwa kuongezea maswali kuhusu kusudi la uhai ambayo huulizwa sana na vijana, vijana pia wanahitaji kukabiliana na uhalifu na jeuri. Je, inawezekana kushinda mambo haya? Makala ya gazeti hilo ilitoa maelezo haya: “David alipokuwa na umri wa miaka 30 alianza kuwa na wasiwasi kuhusu athari alizokuwa akipata kutokana na matumizi ya vileo, dawa za kulevya na jeuri. Mashahidi wa Yehova walibisha mlango wake wakiwa na majibu kwa matumaini yake ya kuwekwa huru na mazoea hayo. Alijifunza. Aligeuka. Alilipa madeni yake ya kamari na kuwarudishia pesa wote aliowalaghai katika michezo ya karata hata ingawa hawakuwa na habari. Havuti sigareti, hanywi, wala hapigani tena.”
Kuhusu vijana wengine waliojifunza na Mashahidi wa Yehova, makala hiyo iliendelea kusema: “Wamepata majibu kwa maswali yao yote.” Shahidi mmoja mchanga alieleza hivi kwa usahili: “Biblia imekuwa ikisema kweli kwa miaka elfu mbili, basi kwa nini niende mahali pengine ili kupata mwongozo?”
Neno la Mungu lina ujumbe kwa vijana. Shauri lake lenye kutumika huwasaidia wakabiliane na matatizo ya leo na huwapa msingi thabiti wa kuamini katika wakati ujao wenye amani na udugu. Katika ulimwengu unaobadilika daima, tumaini ambalo Biblia hutoa ni “nanga ya nafsi, likiwa hakika na imara,” likitokeza utegemezo na faraja. (Waebrania 6:19) Mamia ya maelfu ya vijana wamepata kusudi halisi katika maisha zao kupitia funzo la kibinafsi la Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Wamejionea jinsi Biblia hutokeza mabadiliko halisi. Kwa kuyakubali majibu ya Biblia, vijana wanapata kwamba utafutaji wao wa imani halisi huthawabishwa.
[Picha katika ukurasa wa 12]
Msherehekeo wa kidini wavutia maelfu ya vijana katika Paris
[Picha katika ukurasa wa 13]
Siku za Vijana Ulimwenguni katika Paris—je, kweli ni kurudia kupenda dini?