Vijana wa Leo— Ufanani Duniani Pote
MIFANANISHO maarufu huonyesha vijana kuwa waasi wenye kichaa cha madawa ya kulevya, wapumbavu, wenye kujifikiria na wavivu, wasiofikiria kingine isipokuwa mavazi, TV, na ngono. Hata hivyo, kwa walio wengi maoni hayo mabaya kuelekea vijana huonekana kuwa yaliyo mbali sana na uhalisi.
Uchunguzi mmoja ulioripotiwa katika Psychology Today ulipata kwamba ‘karibu robo tatu za wale waliochunguzwa walionekana wamerekebishwa vizuri. Kwa ujumla walikuwa wenye furaha, wenye kujiweza, wenye kuwajali wengine, wenye kuhangaishwa na matokeo ya vitendo vyao.’ Tofauti sana na kuwa wametenganishwa sana na wazazi wao, vijana walio wengi walipatikana kuwa ‘wameshikilia nia nzuri sana kuelekea familia zao.’
Uchunguzi mwingine mwingi wafunua kwamba mengi ya matumaini, matazamio, na hofu za vijana wa leo huonyesha pia kufikiri kwa akili nzuri, kwenye utimamu. Katika 1985 Unesco Courier liliuliza vijana katika mabara 41 hivi: “Ni nini tatizo lenye kuhangaisha vijana wote leo?” Walipata majibu yaliyofikiriwa vizuri kama “matatizo ya vita na amani” (asilimia 50), “ukosefu wa kuajiriwa na kazi” (asilimia 30), na “wakati ujao” (asilimia 10).
Hata fikira zinapoelekezwa kwenye matamanio ya kibinafsi, kwa mara nyingine vijana wanakuwa na maoni ya kiakili. Baada ya kutafuta maoni ya “kikundi cha vijana wanaume na wanawake [wa U.S.] wa umri wa miaka kumi na minne hadi ishirini na mmoja wenye kuwakilisha taifa lote,” gazeti Seventeen liliambia wasomaji walo wachanga hivi: “Zaidi ya jambo jinginelo lote, nyinyi mwataka kuoa na kuwa na familia. Jambo la pili mnalotaka ni kazi au kazi-maisha. Mna lengo la kuchuma pesa. Mna wasiwasi juu ya pesa, pia, na elimu. Lakini asilimia zaidi ya 60 yenu hamwamini matatizo ya ulimwengu ni makubwa mno kwa kizazi chenu kutoweza kufanya mambo yawe afadhali.”
Basi, kwa ujumla vijana ulimwenguni pote wanataka mambo yale yale ambayo wazee wao hutafuta: furaha, usalama, familia zenye ukaribu-karibu. Wanahangaikia ulimwengu wanaoishi ndani yao na kwa moyo mweupe wataka kuufanya uwe bora zaidi. Hata hivyo, kuna upande usio na tumaini zuri wa ufananisho huo.
Vijana Wenye Huzuni na Wenye Kujiangamiza
Uchunguzi huo uliotangulia kutajwa ulifanya ugunduzi huu wenye kusikitisha: “Robo moja ya wabaleghe waliotahiniwa walisema huwa na huzuni na wenye upweke mara nyingi na huhisi wakiwa tupu kihisia-moyo, na pia kuzongwa na matatizo ya maisha. Wachache hata walikubali kuwa na mawazo na mielekeo ya kujiua.” Katika mabara fulani vijana huchukua hatua zaidi ya kufikiri tu. Kiwango cha kujiua miongoni mwa vijana wenye umri mkubwa zaidi katika United States karibu kilikuwa maradufu katika miaka 20 iliyopita!a
Sababu nyingine yenye kuhangaisha sana ni ongezeko la ulimwenguni pote la matumizi ya madawa ya kulevya, kama vile marijuana, heroin, kokeni, na kasumba, namna fulani ya kokeni. Msichana mmoja wa miaka 14 katika United States alisema hivi juu ya kuvuta marijuana: “Sasa hata si ndio ‘mtindo wa kisasa’ tena. Hilo lakaribia kuwa sehemu ya maisha ya kila mtu.”
Wala nchi zinazositawi hazikuepuka tatizo hilo. Ni jambo la kawaida katika mabara hayo kuona vijana wakivuta sigareti za nta ya coca na vitu kama hivyo. Kwa hiyo Katibu-Mkuu wa UM Javier Pérez de Cuéllar alisema kwamba tatizo la ulanguzi haramu na matumizi mabaya ya madawa ya kulevya “latokeza tishio lenye kuangamiza kwa vizazi vya sasa na vijavyo kama vile zile tauni zilizoenea sehemu nyingi za ulimwengu katika mihula ya mapema.”
Pia matumizi ya madawa ya kulevya yaliyo halali, kama vile alkoholi (kileo) na tumbako, miongoni mwa vijana yanatia wataalamu wengi—na wazazi—wasiwasi. Laripoti hivi UN Chronicle: “Kwa miaka 30 hadi 40 iliyopita, kulingana na WHO [Shirika la Afya Ulimwenguni], asilimia zenye kuongezeka za watoto na wabaleghe wameanza kunywa alkoholi; viwango na ukawaida wa unywaji umeongezeka; na umri ule ambao unywaji huanza umeshuka.”
Kama ilivyo, ni vijana wachache walioshuka moyo au wanaoshiriki katika tabia ya kujiangamiza. Hata hivyo, ulimwenguni pote, jumla yake inakuwa ni mamilioni mengi walio na matatizo makubwa. Kama tutakavyoona kufuatia, vijana leo wanaelekewa na mikazo na misongo iliyo ya kipekee kwa nyakati hizi tunamoishi.
[Maelezo ya Chini]
a Kulingana na kitabu Helping Your Teenager Deal With Stress, wengine huamini kwamba “migongano ya motokaa ni njia inayotumiwa mara nyingi sana na vijana wenye umri mkubwa zaidi wanaojiua.” Kwa kuwa misiba ya magari huwa kwa ujumla haihesabiwi kuwa kujiua, tarakimu za vijana kujiua huenda zikawa zinapunguzwa mno.