Utawala wa Kibinadamu Wapimwa Katika Mizani
Sehemu 3: Je! Kweli ‘Serikali ya Walio Bora Zaidi’ Ndiyo Bora Zaidi?
Aristocracy: serikali ya makabaila, wachache waliopendelewa, au tabaka ya wachache bora inayodhaniwa ndiyo inastahili zaidi kutawala; oligarchy: serikali ya wachache, ama ya watu fulani au familia fulani, mara nyingi kwa ajili ya makusudi yaliyopotoka na ya kichoyo.
YAONEKANA ni jambo la akili kwamba aina bora zaidi ya serikali ingekuwapo kama ingeundwa na watu walio bora zaidi. Watu bora zaidi wameelimishwa vizuri zaidi, wastahili zaidi, na wana uwezo zaidi—ndivyo ilivyo hoja hiyo—na kwa hiyo wafaa zaidi kuongoza wengine. Serikali ya aristocracy yenye kuongozwa na tabaka ya wachache walio bora yaweza kuwa ya mojawapo aina kadhaa; kwa kielelezo, utawala wa matajiri, plutokrasi; utawala wa makasisi, theokrasi; au utawala wa maofisa, biurokrasi.
Jumuiya nyingi zisizostaarabika, zikiwa chini ya utawala wa wazee au majumbe wa kikabila, zilikuwa aristocracy. Wakati mmoja au mwingine, Rumi, Uingereza, na Japani, tukitaja tatu tu, zote zilikuwa na serikali za aristocracy. Katika Ugiriki ya kale, neno “aristocracy” lilitumiwa kurejezea serikali za majiji, au poleis, ambapo kikundi kidogo kilitawala. Mara nyingi hesabu fulani ya familia maarufu ziligawana mamlaka. Hata hivyo, katika visa fulani, familia moja moja zilinyakua mamlaka kiharamu na kusimamisha utawala wa namna ya kikatili.
Kama vile serikali za majiji mengine, Athene lilikuwa aristocracy hapo awali. Baadaye, kwa kadiri mabadiliko ya kitamaduni yalivyodhoofisha tofauti za kitabaka na kuvunja-vunja umoja, jiji hilo lilitwaa namna za kidemokrasi. Kwa upande mwingine, Sparta, ambalo husemekana lilianzishwa katika karne ya tisa K.W.K., lilitawalwa na oligarchy ya kijeshi. Upesi jiji hilo likalingana na Athene la kale zaidi, na majiji yote mawili yalipigania ukuu wa ulimwengu wa Kigiriki wa wakati huo. Kwa hiyo, utawala wa wengi, kama katika Athene, ukaja kushindana na utawala wa wachache, kama katika Sparta. Bila shaka, ushindani wayo ulihusisha mengi, ukitia ndani zaidi ya kutoafikiana juu ya serikali.
Wazo Bora Lapotoshwa
Mara nyingi tofauti za kisiasa zilikuwa habari ya hoja za kifalsafa miongoni mwa wanafalsafa Wagiriki. Aristotle, aliyekuwa hapo kwanza mwanafunzi wa Plato alitofautisha kati ya aristocracy na oligarchy. Alibainisha aristocracy kamili kuwa namna nzuri ya serikali, wazo bora lililowezesha watu wenye uwezo wa pekee na maadili ya juu wajitumikishe katika utumishi wa umma kwa faida ya wengine. Lakini aristocracy kamili inapoongozwa na wachache walio bora wenye uonevu na ubinafsi, inazorota kuwa oligarchy isiyofanya haki. Aliona hiyo kuwa namna iliyopotoka ya serikali.
Ijapokuwa alitetea utawala wa ‘walio bora zaidi,’ Aristotle alikubali kwamba kuunganisha aristocracy na demokrasi yaelekea kungetokeza matokeo yaliyotamaniwa, wazo ambalo bado huvutia wafikiriaji wengine wa kisiasa. Kwa kweli, Warumi wa kale waliunganisha namna hizo mbili za serikali na kufanikiwa kwa kadiri fulani. “Siasa [katika Rumi] zilikuwa shughuli ya kila mtu,” chasema The Collins Atlas of World History. Hata hivyo, wakati uo huo, ‘raia walio tajiri zaidi na wale waliopendelewa vya kutosha kuzaliwa katika daraja la juu waliunda oligarchy iliyogawana miongoni mwayo vyeo vya hakimu, jemadari wa jeshi na kuhani.’
Hata katika nyakati za katikati za baadaye na nyakati za mapema za ki-siku-hizi, vitovu vya miji vya Ulaya viliunganisha viasili vya kidemokrasi na aristocracy katika serikali yao. Chasema Collier’s Encyclopedia: ‘Jamhuri ya Venice isiyotaka mabadiliko kamwe, ambayo Napoleon aliipindua hatimaye, ni kielelezo kizuri cha oligarchy ya namna hiyo; lakini Majiji Huru ya Milki ya Rumi Takatifu, majiji ya Shirika la Hansea, na miji ya mkataba ya Uingereza na Ulaya ya magharibi yaonyesha mielekeo ile ile ya ujumla kuelekea uongozi thabiti wa oligarchy kupitia aristocracy ya wachache lakini wenye kiburi na wa daraja la juu.’
Imebishaniwa, na kukiwa na ukweli fulani, kwamba serikali zote ni za asili ya aristocracy, kwa kuwa zote hujitahidi kuwa na watu wanaostahili zaidi mamlakani. Wazo la tabaka yenye kutawala limetumika kutia nguvu maoni hayo. Kwa hiyo kitabu fulani cha marejezo chamalizia hivi: “Tabaka yenye kutawala na wachache walio bora zinakuwa semi zenye kumaanisha jambo moja la kueleza kuwa ni ya kweli yale waliyotolea hoja Plato na Aristotle kuwa yaliyo bora.”
Utafutaji-tafutaji wa ‘Walio Bora Zaidi’
Karne nyingi kabla ya wanafalsafa hao Wagiriki kutokea, jumuiya ya feudal (iliyotegemea mabwana na vibaraka) ilikuwa ikileta kadiri fulani ya uthabiti na amani kwenye China ya kale chini ya nyumba ya kifalme ya Chou. Lakini baada ya 722 K.W.K., wakati wa kile kinachoitwa kipindi cha Ch’un Ch’iu, mfumo wa feudal ulidhoofika polepole. Katika sehemu ya mwisho wa kipindi hicho, wengine wachache walio bora walitokea, wakifanyizwa na wale ambao hapo awali walikuwa “waungwana,” waliotumika katika nyumba za feudal, na wazao wa wakuu wa kale. Washiriki wa walio bora wachache hao waliotokea waliingia katika vyeo vikubwa vya serikali. Confucius, yule Mchina mwenye hekima nyingi aliyejulikana sana, kama ambavyo The New Encyclopædia Britannica hutaja, alikazia kwamba “uwezo na ubora wa adili, wala si uzawa, ndiyo yaliyomfanya mwanamume afae kwa uongozi.”
Lakini katika Ulaya miaka zaidi ya elfu mbili baadaye, utaratibu wa kuchagua wachache walio bora, wale waliokuwa bora zaidi kutawala, haukuhusiana sana na “uwezo na ubora wa adili.” Profesa wa Harvard Carl J. Friedrich asema kwamba ‘wachache walio bora katika Uingereza ya aristocracy ya karne ya kumi na nane walikuwa wachache walio bora waliotegemea hasa uzao wa damu na utajiri. Ilikuwa vivyo hivyo katika Venice.’ Yeye aongeza hivi: “Katika nchi fulani kama Prussia ya karne ya kumi na nane, wale wachache walio bora walitegemea uzao wa damu na uhodari wa kijeshi.”
Wazo la kwamba sifa nzuri za ‘watu walio bora’ zilipokezwa wazao wao laeleza sababu ya mazoea ya ndoa ya wafalme wakati wa siku zilizopita. Wakati wa Enzi za Katikati, wazo la ubora mkuu wa kuzaliwa liliongoza. Kufunga ndoa na mtu wa kawaida kulikuwa sawa na kudhoofisha ukuu wa mbari, kuvunja sheria ya kimungu. Wafalme walipaswa kufunga ndoa na wale wa uzawa wa wakuu. Wazo hilo la ubora wa uzao mkuu liliondolewa baadaye na ujiteteaji uliosawazika zaidi—kwamba ukuu ulitegemea nafasi bora zaidi, elimu, vipawa, au mambo yaliyotimizwa.
Kanuni iliyojulikana kuwa ukuu una daraka ilikusudiwa kuhakikisha kufaulu kwa aristocracy. Kwa halisi kumaanisha “ukuu waweka daraka,” ilionyesha “daraka la tabia ya staha, ya ukarimu, na ya adabu iliyoshirikishwa na cheo au uzawa wa juu.” Kwa sababu ya wao “kuwa bora,” wale wa uzawa wa ukuu walikuwa na daraka la kutumikia vizuri mahitaji ya wengine. Kanuni hiyo ilipatikana katika aristocracy kama ile katika Sparta la kale, ambalo mashujaa walo walikuwa na daraka la kuweka faida za wengine mbele ya zao wenyewe, na katika Japan miongoni mwa tabaka ya mashujaa, samurai.
Aristokrasi Zapungukiwa
Kutokamilika kwa utawala wa aristocracy kwaonyeshwa kwa njia rahisi. Katika Rumi ya kale, ni watu wa uzao wa juu peke yao, walioitwa patricians, ndio waliostahili kuwa washiriki wa Senate (bunge) ya Rumi. Watu wa kawaida, waliojulikana kuwa plebeians, hawakustahili. Lakini kinyume cha kuwa wanaume wa “uwezo na ubora wa adili,” kama ambavyo Confucius alivyotaka kwa watawala, washiriki wa senate walizidi kuwa wapotovu na wenye kuonea. Tokeo likawa ugomvi wao kwa wao.
Ijapokuwa vipindi vya badiliko la mara kwa mara, oligarchy ya senate iliendelea, angalau hadi Julius Caesar aliposimamisha utawala wa kiimla miaka michache kabla ya kuuawa kwake katika 44 K.W.K. Baada ya kifo chake, serikali ya aristocracy ilianzishwa tena, lakini kufikia 29 K.W.K. mahali payo palikuwa pamechukuliwa na nyingine. Collier’s Encyclopedia yaeleza hivi: ‘Kwa ukuzi wa mamlaka, utajiri, na ukubwa wa kijiografia wa Rumi, aristocracy ilikuwa imekuwa oligarchy iliyopotoka, na kukosa kwayo roho ya raia kulionyeshwa na ukosefu wa heshima ya umma. Kuanguka kwayo kulitokeza mornachy yenye mamlaka kamili.’
Kwa miaka 1,200 hivi iliyofuata, serikali za aristocracy, zijapokuwa za mornachy kwa jina, zilikuwa ndiyo kawaida ya Ulaya. Baada ya muda mabadiliko mengi ya kisiasa, kiuchumi, na kitamaduni yalirekebisha mfumo huo polepole. Lakini wakati wa kipindi hicho chote, aristocracy ya Ulaya iliendelea kuwa yenye nguvu, ikiwa na uwezo wa kushikilia mashamba na kuongoza vyeo vya kijeshi, huku ikiwa ya kikupe zaidi na zaidi, kugharimisha mno, yenye kiburi mno, na ovyo-ovyo.
Katika miaka ya 1780 aristocracy ilipatwa na pigo kali. Kwa kujikuta ndani ya matatizo ya kifedha, Louis wa 16 wa Ufaransa, alisihi washiriki wa aristocracy ya Ufaransa waachane na baadhi ya mapendeleo yao yaliyogharimiwa na kodi. Lakini badala ya kumwunga mkono, walijifaidi na matatizo yake, wakitumaini kumwangusha mfalme huyo na kupata tena sehemu ya uwezo wao wenyewe uliopotea. ‘Kwa kutoridhika na serikali ya watu, kupitia mfalme, kwa ajili ya aristocracy, wao [aristocracy] walitafuta serikali ya watu, kupitia aristocracy, kwa ajili ya aristocracy,’ aeleza Herman Ausubel, profesa wa historia katika Chuo Kikuu cha Columbia. Nia hiyo ilisaidia kuchochea Mapinduzi ya Ufaransa ya 1789.
Matukio hayo katika Ufaransa yalitokeza mabadiliko makubwa yaliyofika ng’ambo ya mipaka hiyo. Aristokrasi hiyo ilipoteza mapendeleo yayo ya pekee, mfumo wa feudal ulikomeshwa, Tangazo la Haki za Binadamu na Raia lilipitishwa, na pia katiba. Kuongezea hayo mamlaka ya makasisi yalipunguzwa na amri.
Serikali kupitia wachache—hata ikiwa wachache hao walifikiriwa kuwa bora zaidi—ilikuwa imepimwa katika mizani na walio wengi na ilikuwa imepatikana imepungukiwa.
Mwishowe Kupata ‘Walio Bora’
Uhakika ulio wazi kwamba ‘walio bora’ huwa sikuzote hawaishi kulingana na jina lao waonyesha udhaifu mmoja ulio mkubwa wa ‘serikali kupitia kwa walio bora zaidi,’ yaani, tatizo la kuamua hasa ni nani ‘walio bora zaidi.’ Ili kutimiza matakwa ya walio bora zaidi kutawala, mengi yatakwa zaidi ya kuwa tajiri, kuwa wa damu ya ukuu, au kuwa na uwezo wa ushujaa wa kijeshi.
Si vigumu kutambua ni nani walio bora zaidi kama madaktari, wapishi, au watengeneza viatu. Tunaangalia tu kazi yao na vitu walivyotengeneza. “Hata hivyo, kwa habari ya serikali, hali hiyo si rahisi hivyo,” asema Profesa Friedrich. Tatizo ni kwamba watu hawakubaliani serikali yapasa kuwaje na inayopasa kufanya. Pia, miradi ya serikali hubadilika daima. Kwa hiyo, ni kama Friedrich anavyosema: “Shaka laendelea kuwako juu ya ni nani wachache walio bora zaidi.”
Kwa ‘serikali kupitia walio bora zaidi’ iwe bora zaidi kikweli, wale wachache walio bora wangepaswa wachaguliwe na mtu mwenye maarifa yanayozidi ya kibinadamu na asiyekosea katika kuamua. Wale waliochaguliwa wangepaswa kuwa watu wenye ukamilifu wa adili usioweza kuvunjwa, waliojitoa kabisa kwa miradi isiyobadilika ya serikali yao. Nia yao ya kuweka hali njema ya wengine mbele ya ile yao wenyewe ingepasa kuwa isiyotilika shaka.
Biblia yaonyesha kwamba Yehova Mungu amechagua jamii kama hiyo—Mwana wake Yesu Kristo na wachache wa wafuasi wake waaminifu—na amewaweka watawale juu ya dunia kwa miaka elfu moja. (Luka 9:35; 2 Wathesalonike 2:13, 14; Ufunuo 20:6) Si wakiwa wanadamu wenye kukosea, bali wakiwa viumbe wa kiroho wasioweza kufa ambao hawawezi kukosea, Kristo na watawala wenzake watamiminia dunia baraka za amani ya kudumu, usalama, na furaha, mambo ambayo yatarudisha ainabinadamu kwenye ukamilifu. Je! serikali yoyote ya kibinadamu—hata ‘serikali ya walio bora zaidi’—inaweza kutoa mengi kadiri hiyo?
[Sanduku katika ukurasa wa 26]
Oligarchy ya Ki-Siku-Hizi
‘Mielekeo ya oligarchy . . . imeonekana katika miundo yote mikubwa ya bureaucracy ya mifumo ya kisiasa iliyopiga hatua kubwa. Jumuiya ya ki-siku-hizi yenye kutia mambo mengi yenye kuongezeka na serikali yake hukabidhi mamlaka makubwa zaidi na zaidi mikononi mwa wasimamizi na halmashauri za wataalamu. Hata katika tawala za kikatiba, hakuna jibu lenye kuridhisha kikamili limepatikana kwa swali juu ya jinsi wafanya maamuzi hao wa bureaucracy wanaweza kuhesabiwa daraka na mamlaka yao kuwekewa mipaka kwa njia yenye matokeo, wakati uo huo, isihatarishe utumikaji na usawaziko wa utaratibu wa kufanya maamuzi.’—The New Encyclopædia Britannica.
[Picha katika ukurasa wa 25]
Aristotle aliamini kwamba aristocracy na demokrasi zikiunganishwa zingetokeza namna bora zaidi ya serikali
[Hisani]
National Archaeological Museum, Athens