Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g91 6/8 kur. 3-5
  • Maswali Yanayohitaji Kujibiwa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Maswali Yanayohitaji Kujibiwa
  • Amkeni!—1991
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ambayo Watu Wamefanya
  • Fumbo Katika Mwili wa Kibinadamu
  • Jinsi Wengine Wanavyolieleza Hilo
  • Kupata Majibu
  • Je! Kweli Mungu Anatujali?
    Je, Kweli Mungu Anatujali?
  • Ikiwa Muumba Anajali, Mbona Wanadamu Wanateseka Sana?
    Je, Kuna Muumba Anayekujali?
  • Kuteseka Kote Kutaisha Karibuni!
    Kuteseka Kote Kutaisha Karibuni
  • Swali la 3: Kwa Nini Mungu Anaruhusu Niteseke?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1991
g91 6/8 kur. 3-5

Maswali Yanayohitaji Kujibiwa

WAKATI fulani maishani mwako, huenda ikawa uliuliza: ‘Ikiwa Mungu yupo, ni kwa nini yeye ameruhusu taabu nyingi hivyo? Na ni kwa nini yeye ameiruhusu kwa muda mrefu hivyo, katika historia yote ya binadamu? Je! taabu itakuja kwisha?’

Kwa sababu ya kutokuwa na majibu yenye kuridhisha kwa maswali hayo, wengi wanakuwa na uchungu wa moyoni. Wengine hata huacha kuamini Mungu, au humlaumu kwa ajili ya majanga yao.

Kwa mfano, mwanamume mmoja aliyeokoka yale Maangamizi Makubwa, mauaji ya mamilioni yaliyofanywa na Wanazi katika Vita ya Ulimwengu 2, alikuwa na uchungu mwingi sana wa moyoni hata akasema: “Ukiramba moyo wangu, ungekutia sumu.” Mwanamume mwingine aliyetaabika kwa sababu ya mateso ya kuonewa kikabila, yaliyosababisha kifo cha marafiki na washiriki wa familia katika Vita ya Ulimwengu 1, aliuliza hivi kwa uchungu wa moyoni: “Mungu alikuwa wapi tulipomhitaji?”

Kwa hivyo, watu wengi wanashindwa kuelewa. Kwa maoni yao, yaonekana kuwa kinyume kwa Mungu wa wema na upendo kuruhusu mambo mabaya yatukie kwa muda mrefu hivyo.

Ambayo Watu Wamefanya

Ni kweli kabisa kwamba watu wamewatenda wengine maovu makubwa mno katika karne zote—kwa kweli, kwa maelfu ya miaka. Ukubwa na ubaya wa hayo yote hauwaziki.

Kwa kadiri ambavyo ustaarabu ulidhaniwa unaendelea, binadamu walibuni vyombo vya kutisha zaidi kwa ajili ya kuangamiza au kulemaza wengine: mizinga, bunduki zenye kumimina risasi mfululizo, ndege za vita, vifaru, makombora yenye kuruka, vitupa-moto, silaha za kemikali na za nyukilia. Kwa sababu hiyo, katika karne hii karibu watu 100,000,000 wameuawa na vita vya mataifa! Mamia ya mamilioni wengine wamejeruhiwa au wakataabishwa katika njia nyinginezo. Na kiasi cha vitu viliyoharibiwa, kama vile nyumba na mali, hakipimiki.

Fikiria huzuni kubwa, maumivu, na machozi ambayo yamesababishwa na vita! Mara nyingi mno ni watu wasio na hatia wanaotaabika: wanaume na wanawake wazee, watoto, watoto wachanga. Na mara nyingi mno, wengi waliotokeza maovu hayo hawakuadhibiwa.

Ulimwenguni pote, taabu yaendelea mpaka dakika hii. Kila siku, watu wanauawa au kupata madhara mengineyo kwa sababu ya uhalifu. Wanajeruhiwa au kufa katika misiba, kutia ndani ‘vitendo vya asili’ kama vile tufani, mafuriko, na matetemko ya dunia. Wanataabika kwa sababu ya ukosefu wa haki, ubaguzi, umaskini, njaa, au maradhi, au katika njia nyinginezo nyingi.

Mungu mwema angewezaje kuumba kitu—ainabinadamu—ambacho karne baada ya karne, kimetaabika vibaya sana, kwa wingi?

Fumbo Katika Mwili wa Kibinadamu

Fumbo hilo laonyeshwa pia katika mwili wa kibinadamu. Wanasayansi na wengine ambao wamejifunza juu yao hukubali kwamba mwili wa binadamu umefanyizwa kwa njia ya ajabu, ya kustaajabisha.

Fikiria sehemu chache zao za ajabu: jicho la binadamu lenye kustaajabisha, lisiloweza kuigwa na kamera yoyote; ubongo wenye kutisha, ambao hufanya kompyuta za hali ya juu zaidi zionekane kuwa ovyo; jinsi sehemu za mwili zilizotatanika zinavyoshirikiana bila jitihada ya kufikiri; mwujiza wa kuzaliwa, kutokeza mtoto mchanga wa kupendeza—nakala ya wazazi wake—kwa miezi tisa pekee. Watu wengi hukata kauli kwamba ubuni huo wa kiufundi, mwili wa kibinadamu, lazima uwe uliumbwa na Mbuni aliye fundi—Muumba, Mungu Mweza Yote.

Hata hivyo, kwa kusikitisha, mwili uo huo wa kustaajabisha huchakaa. Baada ya muda unapatwa na magonjwa, uzee, na kifo. Mwishowe unaoza na kuwa mavumbi. Inasikitisha kama nini! Wakati tu mtu anapopaswa kufaidika na makumi mengi ya miaka ya ujuzi na kuwa mwenye hekima zaidi, mwili unakwisha. Mwisho wao ni kinyume cha kusikitisha kama nini, inapolinganishwa na afya, nguvu, na uzuri ambao mwili ulikuwa nao pale mwanzoni!

Ni kwa nini Muumba wa upendo angefanyiza mwili wa kibinadamu ulio mzuri hivyo, lakini ndipo tu mwisho wao uwe wa kuhuzunisha hivyo? Ni kwa nini yeye aumbe kitu kinachoanza kutenda vizuri sana, chenye uwezo mwingi sana uwezao kutumiwa, lakini kinachokuwa na mwisho mbaya hivyo?

Jinsi Wengine Wanavyolieleza Hilo

Wengine wamesema kwamba uovu na taabu ni vyombo vya Mungu vya kufanya tabia yetu iwe bora zaidi kupitia matatizo. Kasisi mmoja Mmethodisti alidai hivi: “Kuwalipa wema kwa mabaya ni sehemu ya mpango wa Mungu wa wokovu.” Yeye alimaanisha kwamba ili wawe na sifa nzuri na kuokolewa, lazima watu wema wataabike kwa sababu ya matendo mabaya ya watu, hilo likiwa ni sehemu ya mpango wa Mungu.

Lakini je! baba wa kibinadamu mwenye upendo angejaribu kufanya tabia ya watoto wake kuwa bora zaidi kwa kupanga waletewe madhara na mhalifu mkatili? Fikiria, pia, vijana wengi waliouawa katika misiba au wanaouawa au kufa katika vita. Wachanga hao wanaokufa hawangekuwa na nafasi zaidi ya kufanya tabia yao kuwa bora kwa sababu wangekuwa wafu. Kwa hiyo wazo la kwamba taabu huruhusiwa kusudi tabia iwe bora zaidi si la akili kamwe.

Hakuna baba yeyote wa kibinadamu mwenye akili na mwenye upendo angetaka taabu au afa lipate wapendwa wake. Kwa kweli, baba ambaye angeruhusu wapendwa wake wataabike kusudi ‘wawe na tabia bora’ angeonwa kuwa asiyefaa, hata asiyesawazika kiakili.

Basi ingeweza kusemwa kwa kufaa kwamba Mungu, yule Baba mkuu zaidi mwenye upendo, Muumba mwenye hekima yote wa ulimwengu wote mzima, alipanga kimakusudi taabu iwe sehemu ya ‘mpango wake wa wokovu’? Kufanya hivyo kungekuwa ni kumwekelea sifa ya ukatili sana na yenye kutisha, sifa ambayo sisi sote hatuikubali hata kati ya wanadamu wa chini.

Kupata Majibu

Twaweza kugeukia wapi tupate majibu yanayohusu Mungu kuruhusu taabu na uovu? Kwa kuwa maswali hayo yamhusu Mungu, ni jambo la akili tuone yeye mwenyewe atoa majibu gani.

Twapataje majibu yake? Kwa kwendea chanzo ambacho Mungu husema alikibuni kiwe kiongozi kwa binadamu—Biblia Takatifu, Maandiko Matakatifu. Hata mtu awe anafikiri nini juu ya chanzo hicho, chastahili kuchunguzwa, kwa maana, kama mtume Paulo alivyosema: “Kila andiko, lenye pumzi ya Mungu, lafaa . . . kwa kuwaonya watu makosa.” (2 Timotheo 3:16) Pia yeye aliandika hivi: “Mlipopata lile neno la ujumbe la Mungu mlilosikia kwetu, mlilipokea si kama neno la wanadamu, bali kama neno la Mungu.”a—1 Wathesalonike 2:13.

Kupata majibu ya maswali juu ya kuruhusiwa kwa taabu ni zaidi ya kuwa matumizi ya akili tu. Majibu hayo ni ya muhimu ili tuelewe yanayoendelea sasa hivi katika tamasha ya ulimwengu, yatakayotukia katika wakati ujao ulio karibu, na jinsi kila mmoja wetu anavyoguswa na hilo.

Twapaswa kuruhusu Biblia, uwasiliano wa Mungu kwa familia ya kibinadamu, ijisemee. Basi, hiyo yasema nini juu ya jinsi taabu ilivyoanza na ni kwa nini Mungu huiruhusu?

Ufunguo wa kuelewa jibu hilo wahusiana na jinsi ambavyo tumefanyizwa kiakili na katika maono ya moyoni. Biblia huonyesha kwamba Muumba alitia ndani ya muundo wetu tukiwa wanadamu sifa hii ya maana sana: tamaa ya uhuru. Acheni tufikirie kifupi yanayohusika katika hiari ya wanadamu na jinsi hilo linavyohusiana na Mungu kuruhusu taabu.

[Maelezo ya Chini]

a Kwa ajili ya mazungumzo ya uthibitisho wa kwamba Biblia ina pumzi ya Mungu, ona kitabu The Bible—God’s Word or Man’s?, kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki