Sababu Mungu Aliruhusu Taabu
“Kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu. Ee BWANA [Yehova, NW], unirudi kwa haki.”—Yeremia 10:23, 24.
MANENO hayo yaliandikwa maelfu ya miaka baada ya binadamu kuumbwa. Yeremia alitambua kwamba hadi kufikia siku yake, historia ya binadamu ilikuwa ni msiba ikilinganishwa na mwanzo mzuri ambao Mungu aliwapa wazazi wetu wa kwanza.
Aliyoonelea Yeremia yamethibitishwa na kumbukumbu ya miaka ya ziada zaidi ya 2,500 ya historia tangu wakati wake. Msiba huo wa kibinadamu umekuwa mbaya hata zaidi. Kosa lilikuwa nini?
Matumizi Mabaya ya Hiari
Wazazi wetu wa kwanza walisahau uhakika wa kwamba hawakuumbwa wafanikiwe bila ya Mungu na sheria zake. Wao waliamua kujitegemea pasipo Mungu, wakifikiri hilo lingefanya maisha yao kuwa bora zaidi. Lakini hilo lilikuwa ni matumizi mabaya ya uhuru wao. Walivuka nje ya mipaka ya hiari iliyowekwa na Mungu.—Mwanzo, sura 3.
Ni kwa nini Mungu hakuharibu Adamu na Hawa tu aanze tena na wanadamu wawili wengine? Kwa sababu enzi kuu yake ya ulimwengu mzima wote na njia yake ya kutawala vilikuwa vimetiliwa shaka. Kuwa kwake Mungu Mweza Yote na Muumba wa viumbe kwampa haki ya kuvitawala. Kwa kuwa yeye ni Mwenye Hekima Yote, utawala wake ndio bora zaidi kwa viumbe vyote. Lakini sasa utawala wa Mungu ulikaidiwa.
Je! wanadamu wangeweza kuendelea vizuri zaidi badala ya kutawaliwa na Mungu? Bila shaka Muumba alijua jibu la swali hilo. Njia hakika kwa wanadamu kujua ilikuwa ni kuwaruhusu wawe na uhuru usio na mipaka ambao waliutamani. Kwa hiyo, sababu moja, kati ya nyinginezo, ambayo Mungu ameruhusu uovu na taabu ni kuonyesha bila shaka yoyote kama utawala wa kibinadamu usiomtegemea waweza kufaulu.a
Adamu na Hawa walijiletea taabu na wazao wao. ‘Walivuna walichopanda.’ (Wagalatia 6:7) “Wametenda mambo ya uharibifu, hawawi watoto wake [Mungu], hii ndiyo ila yao.”—Kumbukumbu la Torati 32:5.
Wazazi wetu wa kwanza walikuwa wameonywa kwamba kutotegemea utawala wa Mungu kungetokeza kifo chao. (Mwanzo 2:17) Hilo lilithibitika kuwa kweli. Kwa kumwacha Mungu, waliacha chanzo cha afya na uhai. Walidhoofika hadi kifo kikawapata.—Mwanzo 3:19.
Baada ya hapo, Mungu aliruhusu wakati wa kutosha kwa familia ya kibinadamu ili kuonyesha kikamili kama mfumo wowote wa kisiasa, kijamii, au kiuchumi waliobuni bila ya utawala wake ungeweza kuthibitika kuwa wenye kuridhisha kikamili. Je! wowote wa mifumo hiyo ungeleta ulimwengu wenye furaha, wenye amani usio na uhalifu au vita? Je! kuna wowote ambao ungesitawisha fanaka ya kimwili kwa wote? Utawala wa Mungu ulikuwa umebuniwa ili utimize mambo hayo yote.—Mwanzo 1:26-31.
Ambayo Kupita kwa Wakati Hufundisha
Upesi historia ikaonyesha ukweli wa Warumi 5:12: ‘Mauti iliwafikia watu wote.’ Mstari huo waeleza kwamba “kwa mtu mmoja dhambi iliingia ulimwenguni, na kwa dhambi hiyo mauti.” Wazazi wetu wa kwanza walipoasi utawala wa Mungu, wakawa na kasoro, wasiokamilika. Kasoro hiyo ndiyo waliyopokeza wazao wao. Kwa sababu hiyo, sisi sote tumezaliwa na kasoro, tukiwa na mwelekeo wa kupatwa na ugonjwa na kifo.
Pia kupita kwa wakati kumefunua jinsi watu waliolemewa mno na dhambi hutendeana mmoja na mwenzake. Kumekuwako vita vingi mno vyenye ukatili visivyohesabika, chuki za kikabila na kidini, kuteswa kwa wazushi, uhalifu wa aina zote wenye kutisha, na vitendo vya ubinafsi na pupa. Kuongezea hayo, umaskini na njaa vimetatiza mamilioni yasiyohesabika ya watu.
Wakati wa maelfu ya miaka yaliyopita, ainabinadamu imejaribu kila namna ya serikali inayowazika. Hata hivyo, moja baada ya nyingine zimeshindwa kutosheleza mahitaji ya binadamu. Hivi majuzi, serikali za Ukomunisti zimekataliwa katika mabara mengi. Katika mataifa ya kidemokrasi kuna uhalifu tele, umaskini, hali ya kiuchumi isiyo imara, na ufisadi. Kweli kweli, namna zote za serikali ya kibinadamu zimethibitika kuwa zimepungukiwa.
Zaidi ya hayo, Mungu ameruhusu wakati kwa wanadamu wafikie kilele cha ufanisi wao wa kisayansi na kimwili. Lakini je! ni maendeleo halisi wakati mahali pa uta na mshale pamechukuliwa na makombora ya nyukilia? wakati watu wanapoweza kusafiri angani lakini wasiweze kuishi pamoja duniani kwa amani? wakati mamilioni ya watu wanahofu kutoka nje usiku kwa sababu ya uhalifu?
Jambo ambalo mtihani wa wakati huonyesha ni kwamba haiwezekani kwa binadamu ‘kuelekeza hatua zake’ kwa kufaulu kama vile isivyowezekana kwao kuishi bila chakula, maji, na hewa. Sisi tumebuniwa tutegemee Mfanyizaji wetu kwa ajili ya uongozi kama vile kwa hakika tuliumbwa tutegemee chakula, maji, na hewa.—Mathayo 4:4.
Kwa kuruhusu uovu na taabu, Mungu ameonyesha kwa safari moja ambayo haitarudiwa tena, yale matokeo yenye kusikitisha ya kutumia vibaya hiari. Hiyo ni zawadi yenye thamani sana hivi kwamba badala ya kuwanyang’anya binadamu, Mungu amewaruhusu waone maana ya kuitumia vibaya.
Kuhusu hiari, kichapo “Statement of Principles of Conservative Judaism” chasema hivi: “Bila ya uwezekano halisi wa watu kufanya uchaguzi mbaya wanapokabiliwa na wema na uovu, wazo lote la uchaguzi halina maana. . . . Nyingi za taabu za ulimwengu zatokana moja kwa moja na matumizi mabaya ya hiari tuliyopewa.”
Kwa hakika, Yeremia alikuwa sahihi aliposema: “Kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” Na Sulemani pia alikuwa sahihi aliposema hivi: “Mtu mmoja ana mamlaka juu ya mwenziwe kwa hasara yake.”—Mhubiri 8:9.
Kwa mkazo, hilo laonyesha kutoweza kwa mwanadamu kuondoa taabu. Hata Sulemani, pamoja na hekima, utajiri, na nguvu zake zote hakuweza kunyoosha huzuni inayoletwa na utawala wa kibinadamu.
Basi, Mungu atamalizaje taabu? Je! atakuja kulipa wanadamu ridhaa kwa ajili ya taabu yao ya wakati uliopita?
[Maelezo ya Chini]
a Kwa mazungumzo kamili zaidi ya masuala yote yaliyohusika, ona kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani, sura 11 na 12, kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Picha katika ukurasa wa 9]
Mungu aliipa ainabinadamu mwanzo mkamilifu, lakini historia yaonyesha kwamba bila ya kutegemea Mungu wanadamu hawawezi ‘kuelekeza hatua zao’ kwa kufanikiwa