Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • pr seh. ya 6 kur. 22-25
  • Kwa Nini Kuna Kuteseka Kwingi na Ukosefu Mwingi wa Haki?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kwa Nini Kuna Kuteseka Kwingi na Ukosefu Mwingi wa Haki?
  • Ni Nini Lililo Kusudi la Uhai?
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mfano Mmoja
  • Kilichoharibu Mambo
  • Kwa Nini Ni Muda Mrefu Hivyo?
  • Mungu Ataingilia Mambo Hivi Karibuni
  • Muda Ambao Mungu Ameruhusu Kuteseka Wakaribia Kwisha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • Sababu Mungu Aliruhusu Taabu
    Amkeni!—1991
  • Je! Mungu Anajali?
    Je! Mungu Anajali?
  • Kuteseka Kote Kutaisha Karibuni!
    Kuteseka Kote Kutaisha Karibuni
Pata Habari Zaidi
Ni Nini Lililo Kusudi la Uhai?
pr seh. ya 6 kur. 22-25

Sehemu ya 6

Kwa Nini Kuna Kuteseka Kwingi na Ukosefu Mwingi wa Haki?

1 Hata hivyo, ikiwa yule Mtu Mkuu Zaidi Sana alikusudia kwamba watu wakamilifu waishi duniani milele katika hali za paradiso na ikiwa hilo bado ndilo kusudi lake, kwa nini hakuna paradiso sasa? Kwa nini, badala ya hivyo, ainabinadamu imepatwa na mateso na ukosefu wa haki kwa karne nyingi?

2 Hapana shaka, historia ya kibinadamu imejawa na taabu iliyoletwa na vita, ushindi wa kikoloni, unyonyaji, ukosefu wa haki, umaskini, misiba, magonjwa, na kifo. Kwa nini mambo mengi sana mabaya yamewapata watu wasio na hatia? Ikiwa Mungu ni mwenye nguvu zote, kwa nini yeye ameruhusu kuteseka kwingi sana kwa muda wa maelfu ya miaka? Kwa kuwa Mungu alibuni na kupanga ulimwengu wote mzima kwa utaratibu mzuri sana, kwa nini yeye angeruhusu mvurugo na uharibifu duniani?

Mfano Mmoja

3 Acha tutumie mfano ili kutoa kielezi kwa nini Mungu mwenye utaratibu angeruhusu mvurugo duniani. Ebu wazia, ukitembea msituni na kupata nyumba. Unapoichunguza nyumba hiyo, unaona kwamba imo katika vurugu. Madirisha yamevunjika, dari limeharibika sana, sebule ya mbao imejaa mashimo, mlango unaning’inia kwa bawaba moja, na mabomba ya maji hayafanyi kazi.

4 Kujapokuwa na kasoro hizo zote, je, ungetoa mkataa kwamba hakuna mbuni mwenye akili ambaye angaliweza kubuni nyumba hiyo? Je! hali hiyo ya vurugu ingekusadikisha kwamba ni nasibu tu ndiyo ingaliweza kutokeza hiyo nyumba? Au ikiwa ungetoa mkataa kwamba mtu fulani aliibuni na kuijenga, je, ungehisi kwamba mtu huyo hakuwa na ustadi na hakutumia akili?

5 Unapolichunguza hilo jengo kwa uangalifu zaidi, unaona kwamba mwanzoni lilijengwa vizuri na linatoa uthibitisho wa utunzaji mwingi wenye kujali. Lakini sasa limeharibika na linaelekea kuangamia. Kasoro hizo na hayo matatizo yangeonyesha nini? Yangeweza kudokeza kwamba (1) mwenye nyumba alikufa; (2) yeye ni mjenzi stadi lakini hapendezwi tena na nyumba hiyo; au (3) yeye alikodisha nyumba yake kwa muda kwa wapangaji wasiothamini. Hali hiyo ya mwisho inafanana na ile inayohusu dunia hii.

Kilichoharibu Mambo

6 Kutoka kwa rekodi ya Biblia ya mapema, tunajifunza kwamba halikuwa kusudi la Mungu watu wateseke au kufa. Wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa, walikufa tu kwa sababu walikosa kumtii Mungu. (Mwanzo, sura 2 na 3) Walipokosa kutii, hawakuwa tena wakifanya mapenzi ya Mungu. Wao walijiondoa chini ya utunzaji wa Mungu. Kama tokeo, walijitenga wenyewe na Mungu, kile “chanzo cha uhai.”—Zaburi 36:9, NW.

7 Kama mashine inayopungua mwendo na kusimama inapoondolewa kutoka kwenye chanzo chayo cha umeme, miili na akili zao zilidhoofika. Likiwa tokeo, Adamu na Hawa walichakaa, wakawa wazee, na hatimaye wakafa. Kisha nini kikatukia? Walirudi mahali ambako walitoka: “U mavumbi wewe, nawe mavumbini utarudi.” Mungu alikuwa amewaonya kwamba tokeo la kukosa kutii sheria zake lingekuwa kifo: ‘Mtakufa hakika.’—Mwanzo 2:17; 3:19.

8 Si wazazi wetu tu wa kwanza waliokufa bali wazao wao wote, jamii nzima ya kibinadamu, imetiishwa pia kwenye kifo. Kwa nini? Kwa sababu kulingana na sheria za urithi-tabia, watoto hurithi tabia za wazazi wao. Na yale ambayo watoto wote wa wazazi wetu wa kwanza walirithi yalikuwa kutokamilika na kifo. Warumi 5:12 hutuambia hivi: “Kama kwa mtu mmoja [Adamu, babu ya ainabinadamu] dhambi iliingia ulimwenguni, na kwa dhambi hiyo mauti; na hivyo mauti ikawafikia watu wote kwa sababu wote wamefanya dhambi [kwa kurithi kutokamilika, yaani, maelekeo yenye dhambi].” Na kwa kuwa dhambi, kutokamilika, na kifo ndivyo vitu pekee ambavyo watu wanajua, wengine huviona kuwa vitu vya kawaida na visivyoepukika. Hata hivyo, wanadamu wa kwanza waliumbwa wakiwa na uwezo na tamaa ya kuishi milele. Hiyo ndiyo sababu kwa nini watu wengi huliona kuwa lenye kutamausha sana lile taraja la kwamba uhai wao utakatizwa na kifo.

Kwa Nini Ni Muda Mrefu Hivyo?

9 Kwa nini Mungu ameruhusu wanadamu wafuate njia yao wenyewe kwa muda mrefu hivyo? Kwa nini yeye ameruhusu kuteseka kuendelee kwa karne hizi zote? Sababu moja kuu ni kwamba suala la maana sana lilizushwa: Ni nani mwenye haki ya kutawala? Je! Mungu apaswa awe ndiye Mtawala wa wanadamu, au wao wanaweza kujitawala wenyewe kwa mafanikio bila kumtegemea?

10 Wanadamu waliumbwa wakiwa na hiari, yaani, wakiwa na uwezo wa kuchagua. Wao hawakufanyizwa kama maroboti (mashine) au kama wanyama, ambao huongozwa hasa na silika. Kwa hiyo wanadamu waweza kuchagua ni nani watakayemtumikia. (Kumbukumbu la Torati 30:19; 2 Wakorintho 3:17) Hivyo, Neno la Mungu hushauri hivi: “[Iweni kama watu] huru, ila wasiotumia uhuru huo kwa kusitiri ubaya, bali kama watumwa wa Mungu.” (1 Petro 2:16) Hata hivyo, ingawa wanadamu wana zawadi nzuri ajabu ya hiari, ni lazima wakubali matokeo ya yale wanayochagua kufanya.

11 Wazazi wetu wa kwanza walifanya chaguo baya. Walichagua mwendo wa kutomtegemea Mungu. Ni kweli, Mungu angaliweza kuwaua hao watu wawili wa kwanza walio waasi mara tu baada ya wao kutumia vibaya hiari yao. Lakini hilo lisingalijibu lile suala kuhusu haki ya Mungu kutawala wanadamu. Kwa kuwa hao watu wawili wa kwanza walitaka kujitegemea bila Mungu, swali hili lazima lijibiwe: Je! mwendo huo ungetokeza maisha yenye furaha na mafanikio? Njia pekee ya kujua hilo ilikuwa ni kuacha wazazi wetu wa kwanza na wazao wao wafuatie njia yao wenyewe, kwa kuwa hilo ndilo lililokuwa chaguo lao. Wakati ungeonyesha kama wanadamu waliumbwa ili kufanikiwa katika kujitawala bila kumtegemea Muumba wao.

12 Mwandikaji wa Biblia Yeremia alijua matokeo yangekuwa nini. Akiongozwa na roho takatifu ya Mungu yenye nguvu, au kani ya utendaji, yeye aliandika hivi kwa usahihi: “Ee BWANA [Yehova, NW], najua ya kuwa njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu. Ee BWANA [Yehova, NW], unirudi [unikosoe, NW].” (Yeremia 10:23, 24) Yeye alijua kwamba wanadamu lazima wawe na mwongozo wa hekima ya kimbingu ya Mungu. Kwa nini? Kwa sababu tu Mungu hakuumba wanadamu waweze kufanikiwa bila kutegemea mwongozo wake.

13 Matokeo ya maelfu ya miaka ya utawala wa kibinadamu huonyesha bila shaka yoyote kwamba haimo katika uwezo wa wanadamu kuelekeza mambo yao bila kumtegemea Muumba wao. Baada ya wao kujaribu kufanya hivyo, wao tu ndio wenye kulaumika kwa ajili ya matokeo yenye msiba. Biblia hujulisha hili waziwazi: “Yeye Mwamba [Mungu], kazi yake ni kamilifu; maana, njia zake zote ni haki. Mungu wa uaminifu, asiye na uovu, yeye ndiye mwenye haki na adili. Wametenda mambo ya uharibifu, hawawi watoto wake, hii ndiyo ila yao.”—Kumbukumbu la Torati 32:4, 5.

Mungu Ataingilia Mambo Hivi Karibuni

14 Baada ya kuruhusu utawala wa kibinadamu utoe wonyesho wenye kutosha wa kushindwa kwa utawala wa kibinadamu wakati wa karne nyingi, Mungu sasa aweza kusonga mbele na kuingilia mambo ya wanadamu na kukomesha kuteseka, huzuni, magonjwa, na kifo. Baada ya kuruhusu wanadamu wafikie kilele cha mafanikio yao katika sayansi, viwanda, tiba, na nyanja nyinginezo, hakuna tena uhitaji wowote wa Mungu kuruhusu karne zaidi za wakati ili wanadamu wasiomtegemea Muumba wao waonyeshe kama wanaweza kuleta ulimwengu wa kiparadiso, wenye amani. Hawajaweza na hawawezi. Kutomtegemea Mungu kumetokeza ulimwengu usiopendeza, wenye kujaa chuki, na wenye kuleta kifo.

15 Ingawa kumekuwa na watawala wenye moyo mweupe ambao wametamani kusaidia ainabinadamu, jitihada zao hazijafanikiwa. Kila mahali leo kuna uthibitisho wa kuvunjika kwa utawala wa kibinadamu. Hiyo ndiyo sababu Biblia hushauri hivi: “Msiwatumainie wakuu, wala binadamu ambaye hakuna wokovu kwake.”—Zaburi 146:3.

[Maswali ya Funzo]

1, 2. Kwa kufikiria yaliyowapata wanadamu, ni maswali gani yaweza kuulizwa?

3-5. (a) Ni kielezi gani ambacho chaweza kutusaidia kuelewa kwa nini Mungu wa utaratibu angeruhusu vurugu duniani? (b) Ni njia gani kati ya zile nyinginezo ambayo inafana hali inayohusu dunia?

6, 7. Ni nini kilichowapata Adamu na Hawa walipovunja sheria ya Mungu?

8. Ile dhambi ya wazazi wetu wa kwanza iliathirije familia ya kibinadamu?

9. Kwa nini Mungu ameruhusu kuteseka kuendelee kwa muda mrefu hivyo?

10. Ni uwezo gani waliopewa wanadamu, pamoja na daraka gani?

11. Ni njia gani pekee ya kupata kujua kama mwendo wa kutomtegemea Mungu ungeweza kufanikiwa?

12. Yeremia alikadirije utawala wa kibinadamu, na kwa nini hali iko hivyo?

13. Matokeo ya utawala wa kibinadamu wa maelfu ya miaka umeonyesha nini bila shaka yoyote?

14. Kwa nini Mungu hatakawia tena kuingilia mambo ya kibinadamu?

15. Ni shauri gani la Biblia ambalo tukilifuata, tutafanya vyema?

[Picha katika ukurasa wa 24, 25]

Hata watawala wa ulimwengu wenye moyo mweupe hawajaweza kuleta ulimwengu wa kiparadiso, wenye amani

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki