Sehemu ya 7
Matokeo ya Uasi Yamekuwa Nini?
1-3. Wakati umemthibitishaje Yehova kuwa sahihi?
KUHUSU suala la haki ya Mungu ya kutawala, matokeo ya karne hizo zote za utawala wa kibinadamu wa kujitegemea bila Mungu yamekuwa nini? Je! wanadamu wamethibitika kuwa watawala bora kuliko Mungu? Tukihukumu kwa kumbukumbu la ukatili waliotendeana wanadamu, hakika sivyo.
2 Wazazi wetu wa kwanza walipokataa utawala wa Mungu, msiba ulifuata. Walijiletea kuteseka juu yao wenyewe na familia nzima ya kibinadamu iliyotokana nao. Na hawakuwa na wa kulaumu ila wao wenyewe. Neno la Mungu husema: “Wametenda mambo ya uharibifu, hawawi watoto wake, hii ndiyo ila yao.”—Kumbukumbu la Torati 32:5.
3 Historia imeonyesha usahihi wa onyo la Mungu kwa Adamu na Hawa kwamba ikiwa wangejiondoa chini ya uandalizi wa Mungu, wangedhoofika na hatimaye kufa. (Mwanzo 2:17; 3:19) Walijiondoa chini ya utawala wa Mungu, na baada ya wakati walidhoofika na wakafa.
4. Kwa nini sisi sote huzaliwa tukiwa wasiokamilika, tukiwa na maelekeo ya kupatwa na magonjwa na kufa?
4 Yaliyowapata baadaye wazao wao wote yalikuwa kama Warumi 5:12 hueleza: “Kwa mtu mmoja [Adamu, kichwa cha familia ya ainabinadamu] dhambi iliingia ulimwenguni, na kwa dhambi hiyo mauti; na hivyo mauti ikawafikia watu wote kwa sababu wote wamefanya dhambi.” Hivyo wakati wazazi wetu wa kwanza walipoasi uangalizi wa Mungu, walipata kuwa watenda dhambi wenye kasoro. Kupatana na sheria za urithi, wangeweza kupitisha tu matokeo ya kutokamilika kwa wazao wao. Ndiyo sababu sisi sote tumezaliwa tukiwa na kasoro, tukiwa na maelekeo ya kupatwa na magonjwa na kifo.
5, 6. Historia imeonyesha nini kuhusu jitihada za mwanadamu za kuleta amani na ufanisi wa kweli?
5 Karne nyingi zimepita. Milki zimekuja zikaenda. Kila aina ya serikali iwazikayo imejaribiwa. Hata hivyo, tena na tena, mambo mabaya mno yameipata familia ya kibinadamu. Baada ya miaka elfu sita, mtu angefikiri kwamba wanadamu wangalikuwa wameendelea kufikia hatua ya kusimamisha amani, haki, na ufanisi duniani pote na kwamba kufikia sasa wangalikuwa wamefaulu kusitawisha zile sifa zifaazo za fadhili, huruma, na ushirikiano.
6 Hata hivyo, ukweli ni kinyume kabisa. Hakuna aina ya serikali ya kibinadamu iliyopata kubuniwa ambayo imeleta amani ya kweli na ufanisi kwa ajili ya wote. Katika karne hii ya 20 pekee, tumeona mauaji ya kukusudia yaliyopangwa kwa utaratibu ya mamilioni wakati wa ule Mteketezo Mkuu na machinjo ya zaidi ya milioni 100 katika vita. Katika wakati wetu idadi zisizohesabika za watu zimeteswa-teswa, zikauawa kimakusudi, na kutiwa gerezani kwa sababu ya kutovumiliana na tofauti za kisiasa.
Hali Ilivyo Leo
7. Hali ya familia ya kibinadamu leo yaweza kuelezwaje?
7 Kwa kuongeza, fikiria hali ya familia ya kibinadamu kwa ujumla leo. Uhalifu na jeuri vimeenea pote. Matumizi mabaya ya dawa za kulevya yanaathiri watu wengi sana. Magonjwa yenye kupitishwa kingono yanaenea pote na kuathiri wengi sana. Ule ugonjwa wenye kuogopwa sana wa UKIMWI unaathiri mamilioni ya watu. Makumi ya mamilioni ya watu wanakufa kwa njaa ua magonjwa kila mwaka, huku idadi ndogo ikiwa na utajiri mwingi mno. Wanadamu wanachafua na kuiharibu dunia. Maisha ya familia na kanuni za kiadili zimeharibika kila mahali. Kweli kweli, maisha leo huonyesha utawala mwovu wa ‘mungu wa huu mfumo wa ulimwengu,’ Shetani. Ulimwengu ambao yeye ni bwana wao ni baridi, mkatili, na mfisadi kabisa.—2 Wakorintho 4:4, NW.
8. Kwa nini hatuwezi kuita mambo ambayo ainabinadamu imetimiza kuwa maendeleo ya kweli?
8 Mungu ameruhusu wakati wa kutosha ili wanadamu wafikie upeo wa maendeleo yao ya kisayansi na ya vitu vya kimwili. Lakini je, ni maendeleo ya kweli wakati bunduki mimina-risasi, vifaru, ndege za kuangusha mabomu, na makombora ya nyukilia vimechukua mahali pa uta na mishale? Je! ni maendeleo wakati watu wanapoweza kusafiri kuingia katika anga za juu lakini hawawezi kuishi pamoja kwa amani duniani? Je! ni maendeleo wakati watu wanapoogopa kutembea barabara za mji usiku, au hata wakati wa mchana katika mahali fulani?
Yale Ambayo Wakati Umeonyesha
9, 10. (a) Karne za wakati zilizopita zimeonyesha nini waziwazi? (b) Kwa nini Mungu hatawanyang’anya wanadamu hiari?
9 Yale ambayo mtihani wa karne nyingi za wakati umeonyesha ni kwamba haiwezekani wanadamu kuelekeza hatua zao kwa mafanikio pasipo utawala wa Mungu. Haiwezekani kwao kufanya hivyo kama vile isivyowezekana kwao kuishi bila kula, kunywa, na kupumua. Ushuhuda ni wazi: Sisi tulikusudiwa tuwe tukitegemea mwongozo wa Muumba wetu kama vile tulivyoumbwa tuwe tukitegemea chakula, maji, na hewa.
10 Kwa kuruhusu uovu, Mungu ameonyesha mara moja kwa wakati wote yale matokeo yenye kuhuzunisha ya kutumia vibaya hiari. Na hiari ni zawadi yenye thamani kubwa sana hivi kwamba badala ya kuwanyang’anya wanadamu, Mungu amewaruhusu waone kuitumia vibaya kwamaanisha nini. Neno la Mungu hunena kweli linaposema: “Kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” Pia linasema kweli wakati linaposema: “Mwanadamu ametawala wanadamu kwa kumwumiza.”—Yeremia 10:23, UV; Mhubiri 8:9, NW.
11. Je! namna yoyote ya utawala wa kibinadamu imeondolea mbali kuteseka?
11 Ruhusa ya Mungu ya utawala wa kibinadamu kwa miaka elfu sita yaonyesha kwa nguvu nyingi kwamba mwanadamu ameshindwa kukomesha kuteseka. Hakuna wakati wowote ambapo amefanya hivyo. Mathalani, katika siku zake Mfalme Sulemani wa Israeli, akiwa na hekima, utajiri, na uwezo wake wote, hakuweza kukomesha kuteseka kulikotokana na utawala wa kibinadamu. (Mhubiri 4:1-3) Hali kadhalika, katika siku zetu viongozi wa ulimwengu, hata wakiwa na maendeleo ya kiufundi, hawawezi kuondolea mbali kuteseka. Hata jambo baya zaidi, historia imeonyesha kwamba wanadamu waliojitenga na utawala wa Mungu wameongeza kuteseka badala ya kukuondolea mbali.
Maoni ya Mungu ya Muda Mrefu
12-14. Ni matokeo gani ya muda mrefu yanayokuja kutokana na Mungu kuruhusu kuteseka?
12 Tumeumizwa kwa sababu ya Mungu kuruhusu kuteseka. Lakini yeye amechukua maoni ya muda mrefu, akijua matokeo mazuri ambayo yatakuja mwishowe. Maoni ya Mungu yatanufaisha viumbe, si kwa miaka michache au maelfu machache, bali kwa mamilioni ya miaka, naam, kwa umilele wote.
13 Hali ikitokea katika wakati wowote ujao kwamba mtu fulani atumia vibaya hiari yake kutilia shaka njia ya Mungu ya kufanya mambo, haingekuwa lazima kumpa wakati wa kujaribu kuthibitisha maoni yake. Akiwa amekwisha ruhusu waasi maelfu ya miaka, Mungu amesimamisha kiolezo cha kisheria kinachoweza kutumiwa muda wote wa umilele popote katika ulimwengu wote mzima.
14 Kwa sababu Yehova ameruhusu uovu na kuteseka wakati huu, itakuwa imekwisha thibitishwa vya kutosha kwamba hakuna jambo lisilopatana naye liwezalo kufanikiwa. Itakuwa imekwisha onyeshwa pasipo shaka yoyote kwamba hakuna mpango wowote wa kujitegemea wa wanadamu au wa viumbe-roho unaoweza kuleta manufaa za kudumu. Hivyo, wakati huo Mungu atakuwa na haki kabisa kuponda upesi mwasi yeyote. “Wote wasio haki atawaangamiza.”—Zaburi 145:20; Warumi 3:4.
[Picha katika ukurasa wa 15]
Baada ya wazazi wetu wa kwanza kuchagua kutomtegemea Mungu, hatimaye wao walizeeka wakafa
[Picha katika ukurasa wa 16]
Utawala wa kibinadamu pasipo Mungu umethibitika kuwa wenye msiba
[Hisani]
Picha ya Coast Guard, U.S.