Sehemu ya 6
Sababu Kwa Nini Mungu Ameruhusu Kuteseka
1, 2. Wazazi wetu wa kwanza waliharibuje ule mwanzo mzuri waliopewa na Mungu?
KULITUKIA kosa gani? Ni jambo gani lilitukia ambalo liliharibu ule mwanzo mzuri Mungu aliowapa wazazi wetu wa kwanza katika Paradiso ya Edeni? Kwa nini, badala ya amani na upatani wa Paradiso, uovu na kuteseka vimekuwako kwa maelfu ya miaka?
2 Sababu ni kwamba Adamu na Hawa walitumia vibaya hiari yao. Walikosa kufikiria uhakika wa kwamba hawakuumbwa wafanikiwe bila Mungu na sheria zake. Waliamua kujitenga na Mungu, wakifikiri kwamba hilo lingeendeleza maisha zao. Hivyo wakatoka ndani ya mipaka ya hiari iliyoamuriwa na Mungu.—Mwanzo, Sura ya 3.
Suala la Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote Mzima
3-5. Kwa nini Mungu hakuwaharibu tu Adamu na Hawa na kuanza upya?
3 Kwa nini Mungu hakuwaharibu tu Adamu na Hawa na kuanza upya na watu wengine wawili? Kwa sababu enzi yake kuu ya ulimwengu wote mzima, yaani, haki yake isiyotenganika ya kutawala, ilikuwa imepingwa.
4 Swali lilikuwa hili: Ni nani aliye na haki ya kutawala, na ni utawala wa nani unaofaa? Kuwa kwake mweza yote na Muumba wa viumbe vyote humpa Mungu haki ya kuvitawala. Kwa kuwa yeye ni mwenye hekima yote, utawala wake ndio bora zaidi kwa ajili ya viumbe vyote. Lakini sasa utawala wa Mungu ulikuwa umepingwa. Pia, je, kulikuwako kasoro katika uumbji wake—mwanadamu? Baadaye tutachunguza tujue jinsi suala la uaminifu-maadili wa kibinadamu lilivyohusika.
5 Kwa mwanadamu kujitenga na Mungu, swali jingine lilidokezwa: Je, wanadamu wangekuwa afadhali wasipotawalwa na Mungu? Hakika Muumba alijua jibu, lakini njia hakika ya wanadamu kupata kujua hilo ilikuwa ni kuwaruhusu uhuru wote walioutaka. Walichagua mwendo huo kwa hiari yao wenyewe, hivyo Mungu akauruhusu.
6, 7. Kwa nini Mungu ameruhusu wanadamu uhuru wote kwa muda mrefu sana?
6 Kwa kuruhusu wanadamu wakati wa kutosha wafanye majaribio na uhuru wote, Mungu angethibitisha kwa wakati wote kama wanadamu wangekuwa afadhali chini ya utawala wa Mungu au wakiwa peke yao. Na wakati ulioruhusiwa ungepasa kuwa mrefu vya kutosha kuruhusu wanadamu wafikie kile walichokifikiria kuwa upeo wa mambo waliyotimiza kisiasa, kiviwanda, kisayansi, na kitiba.
7 Kwa hiyo, Mungu ameruhusu mwanadamu fursa kamili hadi leo hii ili kuonyesha bila shaka yoyote kama utawala wa kibinadamu wa kujitegemea bila yeye unaweza kufanikiwa. Hivyo mwanadamu ameweza kuchagua kati ya fadhili na ukatili, kati ya upendo na chuki, kati ya uadilifu na ukosefu wa uadilifu. Lakini amekabiliwa pia na matokeo ya uchaguzi wake: wema na amani au uovu na kuteseka.
Uasi wa Viumbe-Roho
8, 9. (a) Uasi ulitokeaje katika makao ya roho? (b) Ni nani zaidi ya Adamu na Hawa ambao Shetani aliongoza waasi?
8 Kuna jambo jingine la kufikiria. Wazazi wetu wa kwanza sio peke yao walioasi utawala wa Mungu. Lakini ni nani wengine waliokuwako wakati huo? Viumbe-roho. Kabla ya Mungu kuwaumba wanadamu, aliumba namna fulani ya uhai wa hali ya juu, idadi kubwa ya malaika, waishi katika makao ya kimbingu. Wao pia waliumbwa wakiwa na hiari na pia wakiwa na uhitaji wa kutii utawala wa Mungu.—Ayubu 38:7; Zaburi 104:4; Ufunuo 5:11.
9 Biblia huonyesha kwamba uasi ulitokea kwanza katika makao ya roho. Kiumbe-roho alitaka uhuru wote. Hata alitaka wanadamu wamwabudu. (Mathayo 4:8, 9) Mwasi huyo wa roho alipata kuwa kisababishi cha kuongoza Adamu na Hawa waasi, akidai kwa uwongo kwamba Mungu alikuwa akiwanyima kitu fulani chema. (Mwanzo 3:1-5) Kwa hiyo yeye huitwa Ibilisi (Mchongezi) na Shetani (Hasimu). Baadaye, alishawishi viumbe-roho wengine waasi. Wakaja kujulikana kuwa roho waovu.—Kumbukumbu la Torati 32:17; Ufunuo 12:9; 16:14.
10. Uasi wa wanadamu na viumbe-roho ulitokeza nini?
10 Kwa kumwasi Mungu, wanadamu walijitoa waongozwe na Shetani na roho waovu wake. Ndiyo sababu Biblia humwita Shetani “mungu wa huu mfumo wa mambo,” ambaye “amepofusha akili za wasioamini.” Kwa hiyo, Neno la Mungu husema kwamba “ulimwengu wote mzima unalala chini ya nguvu za yule mwovu.” Yesu mwenyewe alimwita Shetani “mtawala wa ulimwengu huu.”—2 Wakorintho 4:4; 1 Yohana 5:19; Yohana 12:31, NW.
Masuala Mawili
11. Shetani alimpinga Mungu kuhusu suala gani jingine?
11 Shetani alizusha suala jingine lililompinga Mungu. Kwa kweli, yeye alishtaki kwamba Mungu alikosea katika ile njia aliyowaumba wanadamu na kwamba hakuna mtu yeyote ambaye angetaka kufanya jambo linalofaa akiwa amesongwa. Kwa kweli, yeye alidai kwamba wakitahiniwa hata wangemlaani Mungu. (Ayubu 2:1-5) Kwa njia hiyo Shetani alitilia shaka uaminifu-maadili wa viumbe vya kibinadamu.
12-14. Wakati ungefunuaje ukweli kuhusu masuala hayo mawili yaliyotokezwa na Shetani?
12 Kwa hiyo, Mungu ameruhusu wakati wa kutosha ili viumbe wote wenye akili waone jinsi suala hili pamoja na lile suala la enzi kuu ya Mungu yangetatuliwa. (Linganisha Kutoka 9:16.) Matukio ya wakati uliopita ya historia ya kibinadamu yangefunua ukweli juu ya masuala hayo mawili.
13 Kwanza kabisa, wakati ungefunua nini kuhusu suala juu ya enzi kuu ya ulimwengu wote mzima, kufaa kwa utawala wa Mungu? Je! wanadamu wangejitawala wenyewe vizuri zaidi ya Mungu? Je! mfumo wowote wa utawala wa kibinadamu pasipo kumtegemea Mungu ungeleta ulimwengu wenye furaha usio na vita, uhalifu, na ukosefu wa haki? Je! mfumo wowote ungeondolea mbali umaskini na kuandaa ufanisi kwa ajili ya wote? Je! mfumo wowote ungeshinda magonjwa, kuzeeka, na kifo? Utawala wa Mungu ulikusudiwa kufanya yote hayo.—Mwanzo 1:26-31.
14 Kuhusu lile suala la pili, wakati ungefunua nini kwa habari ya ubora wa kiumbe cha kibinadamu? Je! lilikuwa kosa Mungu kuwaumba wanadamu katika ile njia aliyowaumba? Je! yeyote wao angefanya jambo linalofaa ikiwa angetahiniwa? Je! kikundi chochote cha watu kingeonyesha kwamba wao wangetaka utawala wa Mungu badala ya utawala wa kibinadamu wa kujitegemea?
[Picha katika ukurasa wa 13]
Mungu ameruhusu wakati ili wanadamu wafikie upeo wa mambo waliyotimiza
[Hisani]
Kurushwa kwa roketi: Kwategemea picha ya NASA