“Mashahidi wa Yehova Kutoka Urusi Siku Nyangavu Zaidi Ziko Mbele”
HICHO ndicho kilichokuwa kichwa kikuu cha habari katika gazeti la Kiingereza The Warsaw Voice la Agosti 19, 1990, lililochapishwa katika Polandi. Mwandishi, Anna Dubrawska, alisema juu ya Mkusanyiko wa “Lugha Iliyo Safi” wa Mashahidi wa Yehova katika Warsaw katika Agosti 1990. Yeye alihoji Mashahidi kutoka Urusi, baadhi yao wakiwa wametumia miaka 15 katika magereza na kambi za mateso kwa sababu ya imani zao za kidini. Lakini sasa walikuwa wanakazia mabadiliko mema yaliyokuwa yakifanyika nchini mwao.
Grigor Goryachek, mfanyakazi wa ujenzi katika Crimea aliyelelewa akiwa Shahidi, alihamishiwa Siberia kwa miaka 15. Alisema: “Sasa tunatazamia kuja kwa siku bora zaidi.” Shahidi mwingine, Anton Pohanich, alisema: “Nyakati bora zaidi zipo hapa tayari. Sasa mimi ninaweza kuchukua ujumbe wetu mlango kwa mlango kwa uhuru, jambo ambalo halingewezekana hapo mbeleni.”
Dubrawska ananukuu Igor Cherny, Shahidi wa miaka 17 kutoka Caucasus: “Kwa miaka 70 watu, hasa wachanga wamekuwa mbali sana na Mungu hivi kwamba sasa wanataka kurudi Kwake kwa kadiri iyo hiyo, au angalau wasikie juu Yake kama kianzilishi.”
Kichapo cha Polandi Dziennik Wieczorny (Gazeti la Jioni) kiliripoti, chini ya kichwa Rodość braci (Shangwe ya Akina Ndugu), kwamba mfanyakazi wa stediamu ya Zawisza katika jiji la Bydgoszcz alisema: “Mimi nina furaha kwa lugha safi inayotumiwa pamoja na tabia njema inayoonyeshwa na vijana.”
Akiandika katika gazeti la kila siku la Polandi Trybuna chini ya kichwa Glosiciele Królestwa (Wahubiri wa Ufalme), Zofia Uszynska alisema hivi kuhusu mkusanyiko huo: “Katika muda wa dakika 30 nilipewa vyakula na kahawa mara kumi. Mara tano mtu fulani alitaka kuniachia kiti chake. Kwa muda wa siku nne zenye kufuatana watu zaidi ya 30,000 walishiriki katika sikukuu ya [kidini] katika Stediamu Dziesieciolecia katika Warsaw. Wanawake wakiwa katika hali ya mimba iliyoendelea sana, familia zenye watoto wachanga, watu wazima na vijana. Aliyekuwa mchanga zaidi kwa waliobatizwa alikuwa na miaka 11, hali yule mzee zaidi alikuwa na umri wa karibu miaka 80.”
Makala hiyo iliendelea kusema: “Warusi elfu kadhaa [kwa hakika zaidi ya 16,000] walikuja kwenye mkutano wa mwaka huu. Mwaka jana kulikuwako Warusi 6,000. Maofisa wa mipaka wa Kirusi waliruhusu mabasi yote yapite bila uhitaji wa kungoja ili yakaguliwe yakiwa katika mistari mirefu ya kilometa nyingi. Wajumbe kutoka kotekote Urusi walikuja: kutoka Vladivostok, Khabarovsk, Vorkuta. Wengine walisafiri kwa gari moshi muda wa siku nne au tano.”
Gazeti hilo hilo linamnukuu Ivan M. Grevniak akisema: “Niliona ukosefu wa haki katika kile ambacho mapapa na mapadri walifanya, na nilitafuta unyofu.” Habari hiyo yaendelea kusema: “Yeye alitambua upatano kati ya maneno na matendo katika tabia ya Mashahidi wa Yehova.” Halafu Ivan akaongezea: “Mimi ninamshukuru Mungu kwamba aliniruhusu nijifunze kweli.”
Trybuna inaripoti kwamba Ivan ni mzee katika kundi lililoko Lvov, ambako “kuna makundi 13 na waamini wa kidini zaidi ya 2,000. . . . ‘Kila mahali katika kila kikundi cha kidini kuna roho ya utaifa. Hata hivyo, roho hiyo inakosekana kati ya waamini wenzi,’ asema Grevniak.”
Umoja huu ulionyeshwa katika mkusanyiko wa Warsaw wa Mashahidi wa Yehova ambapo programu ilitolewa sawia katika Kipolandi na Kirusi katika sehemu tofauti za stediamu. Hakukuwa na kutopatana kokote kwa kitaifa.
Zofia Uszynska pia alivutiwa na ule mpango uliohitajika ili kuwapa makao, kuwalisha, na hata kuwatunza kitiba watu zaidi ya 35,000 waliohudhuria mkusanyiko. Yeye amalizia: “Mimi sijawahi kushiriki mkutano wa watu wengi ambao ulikuwa mwema na wenye urafiki jinsi hii.”
Gazeti la kila siku la Kipolandi Sztandar Mlodych (Kiwango cha Ujana) lilizungumzia kazi iliyofanywa ili kuitayarisha stediamu iwafae wageni wengi hivyo: “Wakiwa wahudumiaji jamii . . .wafuasi wa Yehova walijenga upya mabenchi ya kuketia, wakatengeza mashimo ya kupitia chini na vyoo, wakaondoa takataka kwenye uwanja wa nyasi. Wao walichangia kwenye gharama za mkusanyiko kutoka kwa mifuko yao wenyewe. Mashahidi wa Yehova walitayarisha nafasi za kulala zapata 22,000 kwa ajili ya wageni, wakashugulikia mahali pa kulala pa raia wa Kirusi, na walikuwa na utunzaji wao wenyewe wa kitiba.”
Kwa kweli Mashahidi wa Yehova tayari wanaona “siku nyangavu zaidi” katika Ulaya Mashariki na wanasali kwamba msimamo wao mpya uliopatikana wa kukubaliwa kisheria katika nchi kama vile Romania, Hungari, na Polandi utaenea karibuni kufikia Czechoslovakia, Albania, na Bulgaria.—2 Wathesalonike 3:1; 1 Timotheo 2:1, 2.
[Picha katika ukurasa wa 23]
Mashahidi wa Kirusi katika Mkusanyiko wa “Lugha Iliyo Safi” katika Warsaw, kutia ndani na wanaotaka kubatizwa (juu na picha ndogo iliyotiwa ndani), msemaji wa Kirusi, programu, na wajumbe wa Kirusi mbele ya mabasi yao