Kuna Faraja Gani kwa Wenye Kupatwa na Msiba?
KWA wale ambao hukabiliwa na kifo cha ghafula cha wapendwa wao katika aksidenti zinazohusiana na kileo, huwa “hakuna wakati wa kusema ‘Kwaheri,’ . . . au ‘Nakupenda,’” ataarifu Janice Lord, mwandishi wa Survivor Grief Following a Drunk-Driving Crash.
Kama vile tumekwisha kuona, wale ambao hubaki hai baada ya msiba huwa na mengi kushughulika nayo: mshtuo, hofu, hasira, na kupoteza tumaini. Vifo vya wapendwa kwa njia hiyo husababisha hisia ya hasara ya kudumu. Waliobaki hai baada ya msiba wanaweza kuhisi kwamba sikitiko walilopata haliwezi kamwe kuondolewa kabisa.
Zikitambua uchungu unaosababishwa na hasara kama hizo, mamlaka nyingi hufanyia kazi kupitisha sheria au hali ambazo huenda zikapunguza idadi ya juu yenye kushtua ya wanaokufa kila mwaka. Kwa mfano, ofisa mmoja alitaja udhaifu wa kitabia wa wale waliokuwa na hatia ya kunywa na kuendesha gari na akapendekeza kwamba kuwe na vituo vya kuripoti kwa ajili yao, ambapo, kwa kushauriwa katika elimu na kazi na dawa ya kulevya, ‘wangeweza kusaidiwa na kupewa nguvu’ ili washinde udhaifu wao.
Ni Nini Hasa Kinachohitajiwa?
Hata iwe ni ya kutamanika namna gani, hakuna binadamu au shirika lolote la kibinadamu liwezalo kufutia mbali uchungu uliotiwa wale waliopatwa na msiba, wala binadamu hawawezi kuleta wafu kwenye uhai tena. Kinachohitajiwa kumaliza hasara hiyo yote ni zaidi sana ya kile binadamu wanachoweza kuandaa. Kinachohitajika hasa ni mpango tofauti kabisa katika ulimwengu, mpango ambao hautakuwa na msingi wa mawazo ya ‘furaha kwa bei yoyote ile’ yaliyo ya kibinafsi na yenye uharibifu ambayo huua wengi mno.
Je! kuna msingi wowote hakika wa kutumaini ule ulimwengu bora zaidi ambapo misiba kama hiyo itakuwa ni mambo yaliyopita? Ndiyo, kunao. Kwa kweli kuna tumaini la hakika la ulimwengu mpya hapa duniani ambapo misiba hiyo itakoma, ulimwengu ambao hata waliokufa kwenye aksidenti watarudishwa kwenye uhai. Ni shangwe kama nini wakati hao watakapounganishwa tena na wapendwa wao! Utakuwa ni ulimwengu mpya, ambapo baadaye, kumbukumbu la huzuni ya misiba iliyopita itafutiliwa mbali.
Tumaini hilo la ulimwengu mpya lapatikana katika Neno la Mungu lililovuviwa, Biblia, ambayo hutaarifu hivi: ‘[Mungu] atameza mauti hata milele; na Bwana MUNGU [Yehova, NW] atafuta machozi katika nyuso zote.’ (Isaya 25:8) Hiyo itatia ndani kurudisha wafu kwenye uhai tena kutoka makaburini. Ni kama vile mtume Paulo alivyoandika: “Nina tumaini kwa Mungu . . . ya kwamba kutakuwa na ufufuo wa wafu, wenye haki na wasio haki pia.” (Matendo 24:15) Yesu na mitume walionyesha jambo hilo kwa kufufua wafu.—Luka 7:11-16; 8:40-42, 49-56; Yohana 11:1, 14, 38-45; Matendo 9:36-42; 20:7-12.
Uhai duniani katika ulimwengu mpya, kutia na uhai kwa wafu watakaofufuliwa kutoka makaburini, utakamilishwa kwa uzuri na ukamilifu wa kibinadamu. Uwezo wa Mungu wa kuponya utafanya akili na miili ya wote wanaoishi wakati huo kuwa salama salimini: “Wala hapana mwenyeji atakayesema, mimi mgonjwa.” “Ndipo macho ya vipofu yatafumbuliwa, na masikio ya viziwi yatazibuliwa. Ndipo mtu aliye kilema ataruka-ruka kama kulungu, na ulimi wake aliye bubu utaimba.”—Isaya 33:4; 35:5, 6; ona pia Mathayo 15:30, 31.
Biblia pia inaeleza hali ya wakati ujao wa ainabinadamu duniani kwa kutaja kwamba Mungu “atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.” (Ufunuo 21:4) Mwandalizi wa manufaa hayo bora sana na hali hizo zenye kufurahisha ambazo zitakuja atangaza rasmi hivi: “Mambo ya kwanza hayatakumbukwa, wala hayataingia moyoni. Lakini furahini, mkashangilie daima, kwa ajili ya hivi niviumbavyo.”—Isaya 65:17, 18.
Mambo hayo yote yatatendeka kwa mamlaka ya nani? Ni kwa mamlaka na uwezo wa Mpaji wa tumaini, yule Muumba wa ulimwengu wote mzima, Yehova Mungu. Yeye ahakikisha katika Neno lake kwamba mfumo huo mpya ambao “haki yakaa ndani yake” hivi karibuni utakuja kuchukua mahali pa mfumo huu wa mambo uliopo wenye ubinafsi na jeuri, mfumo ambao tayari upo kabisa katika “siku za mwisho.”—2 Petro 3:13; 2 Timotheo 3:1-5, 13; Mithali 2:21, 22.
Faraja Kutoka kwa Neno la Mungu
Kama ilivyo na watu wengineo wengi, Mashahidi wa Yehova pia hawakingwi na misiba ya nyakati zetu, wala wao hawatarajii ulinzi wa kimungu kutokana na kifo, iwe kwa aksidenti au vyovyote vile katika ulimwengu huu wenye hatari. Wanajua kwamba hayo si mapenzi ya Mungu kwa wakati huu. Mhubiri 9:11, NW inataarifu hivi: “Wakati na tukio lisilotazamiwa huwapata wote.” Na bado, Mashahidi wameelekeza uangalifu kwa Neno la Mungu kwa muda mrefu, kwa sababu ahadi zake hutoa faraja ya kudumu kwa wote wanaozithamini.
Mmoja wa Mashahidi wa Yehova aliathiriwa sana wakati dereva aliyepumbaa-pombe alipoua shemeji yake na kuwacha mke wake (dada ya shahidi huyo) akiwa amelemaa kiakili kutokana na jeraha baya sana la kichwa hivi kwamba alihitaji kutunzwa kila wakati. Wao pia walikuwa ni Mashahidi wa Yehova. Mwanamke huyo aeleza:
“Mara nyingi nilikuwa nikilia na kukasirika katika sehemu kubwa ya mwaka. Nilimkasirikia huyo kijana aliyesababisha msiba huo, na kukasirikia wazazi wake kwa kutomchunga zaidi. Nyakati nyingine hata hiyo kasirani ilielekezwa kwa Mungu na malaika kwa kutozuia jambo hilo lisitendeke. Hasara kweli kweli ya watu wawili wazuri waliokuwa wakimtumikia!
“Ni kweli, nilijua kwamba Mungu hakuhusika moja kwa moja na pia hakupenda mambo hayo yatendeke. Lakini nilikuwa nimehisi kwamba aliongoza hatua zetu zote na kutulinda kwa dhara kama hilo. Sasa nilitambua kwamba ilikuwa ni lazima niwe na maoni yaliyosawazika zaidi kwa tukio hilo, na nikaanza kutafuta majibu.
“Ilinichukua muda kuondolea mbali uchungu huo na hivyo kuweza kutumia akili kwa jambo hilo. Nilihisi kama Asafu, aliyesema katika Zaburi 73 kwamba ilionekana kama kwamba ni waovu ndio waliopendelewa. Lakini katika zaburi hiyo hiyo, Neno la Mungu laendelea kuonyesha kwamba sivyo, kwamba Mungu hapendelei waovu, na kwamba kwa wakati wake, watakuja kuangamia.
“Nikaja kung’amua kwamba ni kufikiri kwangu wala si Mungu, ndiko kulikuwa na makosa. Nilikuwa nikitumia maandiko vibaya. Mungu hatoi ahadi ya uhuru kutokana na aksidenti, ugonjwa, au kifo kwa wakati huu lakini anaahidi baraka kama hizo kwa wakati ujao, kwa ulimwengu wake mpya. Mara nilipoelewa yale hasa Neno la Mungu lilikuwa likisema kuhusu kulindwa kwetu na Mungu sasa kwa njia ya kiroho, bali si kwa kimwili, hasira yangu ilipoa. Sasa hata ningeweza pia kukaza fikira kwenye chanzo halisi cha misiba, yule Shetani Ibilisi, ambaye alikuwa ni muuaji na mwongo kutokea wakati aliasi dhidi ya Mungu. Biblia huelewesha wazi kwamba Shetani ndiye mungu wa ulimwengu huu ambao umejawa sana na taabu.—Yohana 8:44; 2 Wakorintho 4:4.
“Mara nilipothamini zaidi ukweli wa sababu ya kuwapo kwa taabu, sababu ya Mungu kuiruhusu, na jinsi atakavyoimaliza, ikawa wazi kwamba Mungu si adui yetu bali yeye ndiye mkombozi wetu!
“Pia, ilikuwa ni faraja kubwa kujua kwamba kupitia roho takatifu yake, Yehova hutegemeza wale wanaomtumikia. Biblia inatuhakikishia kwamba roho takatifu itatupatia ‘uwezo unaopita ule wa kawaida.’ Kwa njia hiyo yeye atupatia nguvu ya kuvumilia yasiyoweza kuvumilika. Na pia atufariji na lile tumaini la kuona wapendwa wetu katika ufufuo. Hivyo twaweza kushinda dhiki yetu.”—2 Wakorintho 4:7.
Wakati Ujao Bora
Kwa muda wa miaka ambayo imepita, misiba ya aina nyingi imepata wengi kutia ndani Mashahidi wa Yehova. Jambo hilo lahakikisha ukweli wa Neno la Mungu kwamba wakati na tukio lisilotazamiwa huwapata wote. (Mhubiri 9:11) Lakini mambo yaliyoonwa na watumishi wa Mungu pia huhakikisha ukweli wa Neno la Mungu kwamba Yehova hufariji na kutegemeza watu wake katika wakati wao wa uhitaji na pia anahakikisha wakati ujao bora katika ulimwengu wake mpya, ambapo misiba kama hiyo itakuwa jambo lililopita.
Kwa kweli inafariji kujua kwamba katika ulimwengu mpya wa Mungu wenye uadilifu, kutakuwa na upendo wa kweli kwa wanadamu wenzetu na staha kwa zawadi yenye thamani ya uhai. Sifa hizo nzuri zitachukua mahali pa ubinafsi na utumiaji wenye ubinafsi wa udhaifu wa kibinadamu ili kupata faida ambao sasa umejaa katika ulimwengu huu. Mengine yatakayotoweka ni mahangaiko, misongo, na hofu za ulimwengu wa sasa ambazo husukuma wengi waone uhitaji wa kutumia kileo kupita kiasi au kutumia dawa za kulevya nyinginezo.
Hata sasa, Mashahidi wa Yehova hufanyiza udugu wa ulimwenguni pote ambao umefungamanishwa pamoja na kani ya nguvu ya kuunganisha ya upendo. (Yohana 13:34, 35) Wale walio sehemu ya udugu huo huandaa mfumo wa utegemezo ulio thabiti wa kusaidia watu mmoja mmoja ambao wamepatwa na maafa. Wanafurahi kusaidia yeyote yule anayetamani kufarijiwa kama vile wao wamefarijiwa.—2 Wakorintho 1:3, 4.
[Picha katika ukurasa wa 24 ]
Biblia inaahidi kwamba kutakuwako ufufuo wa wafu