Vijana Wanauliza
Vipi Juu ya Vilabu vya Usiku
“TUNAHITAJI vitumbuizo.” “Tunaenda tu kucheza dansi.” “Kila mtu anaenda.” “Twataka tu kujifurahisha.” Vijana kadhaa walimweleza ripota wa Amkeni! kwa nini wamekuwa wazoevu kwa vilabu vya usiku. Vilabu kama hivyo vya usiku vinapendwa na vijana wengi, na ikiwa vinapatikana katika jamii yenu, huenda hata wewe ukawa umefikiria kuenda pia.
Leo, vijana wengi wanaendea aina ya vilabu vifuatavyo, kama inavyoelezwa katika gazeti Friday: “Wakati wa tafrija ni wakati wowote na wakati wowote ni usiku huu. Kwa wasiozuiwa, tafrija hazikomi kamwe. Harara ya dansi inakumba mji kwa furiko la vinywaji baridi, taa za usiku zenye kumetameta na muziki wenye kudunda ambao haukuwachi ukae chini. ‘Vilabu sasa vina jambo kwa upendezi wa kila mtu. . . . Kuna vilabu ambavyo hutumikia wataalamu wachanga, wanafunzi wa chuo, wagoni-jinsia-moja na umati mkuu wa watu wenye umri mkubwa.”
Kwa habari ya umati unaopendelea mambo ya kisasa, kuna vilabu ambavyo huhitaji ada kubwa ya kuwa mshirika, mavazi yenye bei ghali sana, na hata aina ya mwenendo unaotakikana ili kukubaliwa. Kwa wale wasio matajiri, kuna vilabu ambavyo havina wingi wa vitu ambavyo hutoa mazingira ya tafrija kwa bei ya chini. Na kwa vijana wachanga zaidi (au wasio na vipengee) kuingia katika vilabu vya watu wazima, kuna “vilabu vya maji ya matunda” na “vilabu vya soda,” ambavyo hudhaniwa kuwa havina kileo
Si vigumu kuelewa ni kwa nini vilabu vya usiku vina mvuto wenye nguvu kwa vijana wengi. Wakati ungali mchanga, ni asili kupenda kuwa na wakati wa tafrija. (Linganisha Mhubiri 11:9.) Usiku wa kucheza dansi huenda ukawa wenye kuleta afya kuondoa mikazo ya shule na kazi. Lakini je, vilabu vya usiku ni vyenye kufaa jinsi gani?
Sonya, mwanamke mchanga ambaye alikuwa na uzoevu wa vilabu vya usiku, akubali: “Wazo hilo laonekana kuwa wazi vya kutosha. Unaenda huko kucheza dansi na kujifurahisha mwenyewe. Lakini mara nyingi hugeuka kuwa zaidi. Unaanza kwenda usiku wakati muziki na umati ni wenye kuchemka zaidi. Upesi unajua wale wote wa kawaida, na wewe pia ni wa kawaida. Wazo ni kucheza dansi—na kukutana na mtu. Na ikiwa hilo ndilo kusudi lako au sivyo, ni kusudi lao sikuzote.” Je! Sonya anatia chumvi?
Vilabu vya Usiku Leo
Tamasha ya disko mwongo uliopita ilikuja kuwa na sifa mbaya kama msingi kwa adili chafu ya ngono, dawa za kulevya, na hata ugoni-jinsia-moja.a Na mambo yamebadilika kidogo tangu wakati huo. Ingawa muziki (katika United States, kwa kawaida unaitwa muziki wa nyumbani au muziki wa dansi tu) na hatua za kucheza dansi zimebadilika, mazingira katika michezo mingi ya usiku ni mshtuo wa kukumbusha juu ya tamasha ya disko isiyo na adili.
Katika makala kwenye gazeti Life juu ya muziki wa vilabu, mmoja wa wafuatiaji wa vilabu vya usiku asema: “Muziki wa dansi katika asili yake kabisa umekuwa na hisi ya kikabila—mdundo wenye kupigapiga na vipigo vya kimahaba, ukivutavuta hadi namna ya raha ya kupita kiasi inaingia. Kitu fulani kimekuwa kikikosekana katika miji mikubwa, na muziki wa nyumbani unajaza nafasi hiyo iliyo tupu.” David Piccioni mtumbuizaji wa muziki wa New York asema: “Lengo ni kujipoteza usiku wote.”
Kuhusu vichaa vya dansi vya karibuni kama vile lambada isiyo na adili, gazeti Mademoiselle lilitangaza hivi: “Ngono: Imetoka kwa vyumba vya bafu na imerudi mahali pake—kwenye sakafu za kuchezea dansi. Katika siku za zamani (miaka ya 70) sakafu ya kuchezea dansi ilikuwa kwa ajili ya kuamshana nyege na vyumba vya bafu vilikuwa vya ngono na dawa za kulevya. Sasa kwa vile kila mtu anajali juu ya UKIMWI, vyumba vya bafu ni vya kujipambia na sakafu za kuchezea dansi ndipo unaweza kuona watu wakifanya ngono. Au wanasingizia kufanya ngono.” Ndiyo, muziki waweza kutumiwa kutokeza nia ya kupoteza vizuizi vya adili na huamsha nyege.
Kukutana na Nani?
Vilabu vingine vyajulikana kama mahali pa kukutania mtu wa jinsia tofauti. Hata hivyo, ni watu wa aina gani huenda ukakutana nao? Msichana mmoja ambaye alikuwa akizuru mzunguko wa vilabu vya usiku akubali: “Watu wengi pale wana maisha yasiyo na adili na wanapendezwa na kufanya ngono na mtu fulani. Wakivutiwa na wewe, watakununulia vinywaji, vinywaji, vinywaji na kukukaribia usiku wote wakisema mambo mazuri, matamu wakitumaini kwamba utakubali wanayotaka.”
Mahali pengine hata pametengenezwa ili kuwe na utendaji wa ukosefu wa adili. Doris, mwanamke mchanga ambaye pia alikuwa wa kawaida kwa vilabu vya usiku, asema: “Kuna vilabu ambavyo vina sehemu za kujilazia na viti vya kimapenzi ambapo wengi huenda kupiga busu na kugusana. Watu wengi waliooa wako hapo bila wake zao. Wengine wanatumaini kukutana na mtu ili wawe na usiku mmoja pamoja au wawe na uhusiano, na wengine wanatafuta mwenzi.” Amalizia Doris: “Mazingira katika vilabu vya usiku huendekeza sana uasherati. Kileo kinatumiwa katika kiwango kikubwa hadi saa za asubuhi, na chochote kinaendelea.”
Tamasha ya vilabu vya usiku pia imeunganishwa na utumizi mkubwa wa dawa za kulevya. Mwenye kilabu mmoja aliripotiwa kuwa alisema: “Mwendo huo . . . umefungamanishwa kabisa na dawa za kulevya.” Dawa za kulevya na vileo vyaweza kupatikana hata katika mahali panapodhaniwa kuwa hakuna kileo. Jesse, aliyekuwa wa kawaida katika vilabu vya usiku, aongeza: “Moshi wa marijuana na sigareti mara nyingi huijaza hewa. Wengi wa watu pale wanajipamba katika njia ya kuamsha mwili: nguo zenye kubana na kuonyesha, mitindo michafu, vito vyenye kupita kiasi.”
Uwe Mwenye Hathari
Kutoka siku za zamani, muziki na kucheza dansi kumetumiwa kuvuta watu kwenye utovu wa mwenendo. Kwa mfano, tunasoma kwamba Waisraeli wakati mmoja ‘waliketi kula na kunywa. Halafu wakaondoka wacheze.’ Hii ilitia ndani muziki uliopotoka na kucheza dansi kusikozuiwa. Hata hivyo, ‘kucheza’ huku kulikuwa mwanzo wa kuabudu sanamu na mwenendo mlegevu usio na kizuizi.—Kutoka 32:6, 17-19, 28.
Vijana Wakristo basi ni lazima wajiepushe kujiingiza katika hali ambayo kwa haraka ingekuwa ‘ulafi,’ au ‘karamu potovu.’ (Wagalatia 5:19, 21; Byington) Wakorintho wa kwanza 15:33 hutukumbusha: “Msidanganyike; mazungumzo [mashirika, NW] mabaya huharibu tabia njema.” Je! mtu anaweza kujitumbukiza mwenyewe katika mazingira ya karamu yenye watu mmoja mmoja ambao “akili zao zimetiwa giza, nao wamefarikishwa na uzima wa mungu” na asiathiriwe vibaya? (Waefeso 4:18, NW) Na kama vile mwanamke mmoja mchanga anavyokubali: “Mashirika na urafiki wa ndani waweza na mara nyingi hutokea [pamoja na wengine wa kawaida katika vilabu vya usiku].” Hili laweza kuathirije hali yako ya kiroho?
Hata hivyo, wengine huenda wakafikiri, kwamba jibu ni kuenda pamoja na kundi la Wakristo wenzi. Hata hivyo, uadilifu unaweza kusitawi tu katika mazingira ya Kikristo. (Yakobo 3:18) Na mazingira katika vilabu vingi vya usiku yamefanyizwa kuamsha hisia ambazo ni za “dunia, ya tabia ya kibinadamu, na Shetani,” badala ya kiroho.—Yakobo 3:15.
Inakubalika, si vilabu vyote vya usiku ambavyo hufikia kiwango kilichozungumzwa hapo, wala si jambo la akili kutoa lawama juu ya mikahawa yote yenye dansi au vitumbuizo. Lakini Paulo atushauri ‘kuhakiki ni nini impendezayo Bwana.’ (Waefeso 5:10) Na ikiwa unaalikwa mahali penye sifa isiyojulikana au yenye kutiliwa shaka, ni lazima uwe mwenye hadhari sana kuhusiana na kukubali mwaliko.—Mithali 14:15.
Labda unaweza kujiuliza maswali kama: Ni akina nani wanaenda, na wana sifa gani? Je! wazazi wako na watu wengine wazima wenye kuhusika wanajua nini juu ya mahali penyewe? Pana mazingira ya aina gani? Ni watu wa aina gani wamepazoea? Je! ni mahali pa vijana tu? Ikiwa ndivyo, paelekeaje kuwa na mazingira yenye kufaa? Ikiwa kuna vitumbuizo, ni vitumbuizo vya aina gani? Ni muziki wa aina gani utakaopigwa? Je! ni mahali ambapo panaruhusu wateja uhuru zaidi au mahali pa kukaa peke yao, au ni pale ambapo mtachanganyika na wengine?
Doris, aliyetajwa mbeleni, akubali: “Shetani hufanya vilabu vya usiku vionekane kuwa vyenye kuvutia, kutia furaha, uzuri wa kudanganya, raha—kwa vyovyote iwezekanavyo ili kutuvuta.” Lakini usidanganywe na kumetameta kwa vilabu vya usiku! Vimethibitika kuwa mtego wa kufisha kwa vijana wengi. Tafuta njia zenye kukubalika, zenye faida za kujitumbuiza mwenyewe.b
[Maelezo ya Chini]
a Ona Amkeni! ya Machi 22, 1979 (Kiingereza).
b Kwa madokezo kuhusu haya, ona ukurasa 37 wa kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza Majibu Yanafanyayo Kazi, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Picha katika ukurasa wa 26]
Wengi walio wazoevu wa vilabu vya usiku wanapendezwa sana na ngono haramu kuliko vitumbuizo