“Wana Nguvu Nyingi Ajabu za Kiadili”
BAADA ya miaka kama 40 ya kuteswa vibaya katika Chekoslovakia, Mashahidi wa Yehova waliweza kufanya makusanyiko ya mzunguko huko. Moja katika Ostrava, katika Mei 1990, liliripotiwa na Jiří Muladi katika gazeti Nova Svoboda (Uhuru Mpya). Kati ya mambo mengine aliandika:
“Juu ya Watu Wenye Ubinadamu Kabisa”
“Kwa siku tatu kabla ya tukio hilo, watu kama 90 walikutana pamoja kwenye Jumba la Tatran na kulisafisha vema kuliko lilivyokuwa limesafishwa kwa miaka 40. Hata nikijitanguliza kusema ya baadaye zaidi, ni lazima niseme hivi, jumba hilo lilikuwa safi kadiri ile ile baada ya lile [kusanyiko] la siku mbili, bila karatasi yoyote au ncha za sigareti kwenye sakafu. Na hata hivyo, Mashahidi wa Yehova hawavuti sigareti.
“Katika siku ya kwanza ya hilo kusanyiko la mzunguko, kulikuwa na wahudhuriaji 1,600. . . . Walianza kwa wimbo ulioimbwa na wote. Watungaji wengi wa muziki wangeshangaa jinsi nyimbo hizo zilivyokuwa nzuri. . . . Kila kitu kinafanywa bila vishindo vya kujionyesha. Hakukuwa na matangulizi ya kujulisha wenye vyeo vya juu. (Hivyo hata sikujua ni nani aliye na cheo kikubwa zaidi nami nawazia hakuna anayejali hilo.) Hakuna miinamo ya heshima na kutamka shime za utukuzo. Unyenyekevu, fadhili, na hisia-mwenzi.”
Habari Juu ya Mashahidi
“Yehova ndilo jina la Mungu. Katika Biblia ya Kichekoslovakia, jina lake linatafsiriwa (au kubadilishwa) kwa jina Hospodin [Bwana]. Mashahidi wa Yehova husisitiza kutumia jina la kwanza la Mungu, na kwa mishughuliko yao wanajitahidi kushuhudua kuwapo kwa na matendo yake. . . .
“Imani ya Mashahidi wa Yehova inakataza kutumia silaha dhidi ya wanadamu, na wale waliokataa utumishi wa kijeshi wa msingi na hawakufanya kazi kwenye mashimo ya kuchimbua makaa-mawe walipelekwa gerezani, hata kwa miaka minne.
“Kutokana tu na hili ni wazi kwamba wao wana nguvu nyingi ajabu za kiadili. Tunaweza kutumia watu kama hao wasio na ubinafsi katika shughuli za juu zaidi za kisiasa—lakini hatutaweza kamwe kuwaweka hapo. Mashahidi wa Yehova husisitiza kwamba wanadamu wamejitawala wenyewe kwa kujiletea hasara tu wao wenyewe. Ni kweli kwamba wanatambua mamlaka za kiserikali lakini wanaamini kwamba ni Ufalme wa Mungu pekee unaoweza kuondoa matatizo yote ya wanadamu. Lakini tahadhari—wao si washupavu wa kidini wasio na akili. Wao ni watu wanaojali sana binadamu. Na sasa, wewe waweza kufikiria lolote lile kuwahusu.
“Nyongeza: Mimi si mmoja wa Mashahidi wa Yehova, ingawa nakubaliana na mengi ya maoni yao.”
[Picha katika ukurasa wa 12]
Kusanyiko katika Jumba la Lucerna, Prague, Chekoslovakia