Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g92 2/8 kur. 8-10
  • Porojo Jinsi ya Kuepuka Kujiumiza Mwenyewe na Wengine

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Porojo Jinsi ya Kuepuka Kujiumiza Mwenyewe na Wengine
  • Amkeni!—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • ‘Shughulikia Mambo Yako Mwenyewe’
  • Kwa Nini Porojo Ni Mbaya?
    Amkeni!—1999
  • Porojo—Zina Madhara Gani?
    Amkeni!—1990
  • Porojo—Kwa Nini Zavutia?
    Amkeni!—1992
  • Ninaweza kuzuiaje porojo?
    Amkeni!—2007
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1992
g92 2/8 kur. 8-10

Porojo Jinsi ya Kuepuka Kujiumiza Mwenyewe na Wengine

MRADI kuna watu, kutakuwa porojo. Hata ulimwengu mpya ulio kamili ambao umetabiriwa katika Biblia unaelekea hautakosa porojo.a (2 Petro 3:13) Mazungumzo ya vivi-hivi, yasiyo ya maana sana kuhusu marafiki na watu tunaofahamiana nao ni sehemu ya msingi ya jinsi tunavyopashana habari na kudumisha uhusiano mwema.

Hata hivyo, hakuna udhuru wowote unaoweza kutolewa kamwe kwa porojo zenye nia ya kuumiza, zenye kudhuru, au zenye uchongezi! Mazungumzo ya aina hiyo huumiza na kujeruhi; yaweza hata kuharibu maisha, mahusiano, na sifa nzuri. Kwa hiyo wewe waweza kuepukaje kuvuka mpaka wa maadili na kujiingiza katika porojo zenye kudhuru? Wewe waweza kujilindaje mwenyewe kutokana nazo? Baadhi ya mashauri bora zaidi yaliyopata kutolewa juu ya habari hiyo yameandikwa katika Biblia. Acheni tutazame baadhi tu ya mashauri hayo.

Dhibiti Ulimi Wako: Imesemwa kwamba “mazungumzo ni mazoezi ya akili, lakini porojo ni mazoezi ya ulimi tu.” Kwa kweli, mazungumzo mengi yenye kuumiza huonyesha, si nia ya kutaka kudhuru wengine, bali kukosa kufikiri kabla ya kusema. Wengine hupayukapayuka mambo yanayohusu wengine; wanatia chumvi, wanapiga chuku, na kupotoa bila kufikiria matokeo. Huwafunulia wengine makosa ya marafiki zao, wenzi wao, na watoto wao bila hata kufahamu hasara wanayoleta.

Hivyo Biblia hutoa shauri hili: “Katika wingi wa maneno hapakosi kuwa na maovu; bali yeye azuiaye midomo yake hufanya akili.” (Mithali 10:19) Kwa maneno mengine, fikiri kabla ya kusema. Fikiri kabla hujasema jambo kuhusu mtu mwingine. Jiulize: ‘Je, ninaweza kurudia maneno hayo mtu huyo akiwepo? Mimi ningehisije kama hilo lingesemwa juu yangu? (Mathayo 7:12) Zaburi 39:1 yasema: “Nalisema, Nitazitunza njia zangu nisije nikakosa kwa ulimi wangu; nitajitia lijamu kinywani, maadamu mtu mbaya yupo mbele yangu.”

Ni kweli kwamba, kuna hali ambazo kudhibiti ulimi wako huenda kukawa karibu kusiwezekane. Kwa mfano, huenda ukawa una shuku zenye nguvu juu ya makosa mazito yaliyotendwa dhidi yako au familia yako. Huenda ukawa huna ithibati yoyote, lakini unahisi uhitaji wa kuchukua hatua. Je! lingekuwa jambo la uchongezi kuzungumza jambo hilo na rafiki unayemtumaini au na mtu fulani katika mamlaka? Je! wewe ni mpiga porojo mwenye nia ya kudhuru ikiwa unamwendea mtu fulani kupata mashauri? Kwa wazi sivyo. Biblia hukubali hekima ya kuwa na mashauri. Bila shaka, uamuzi mzuri na usawaziko ni wa maana wakati unaposhughulikia hali ngumu kama hizo.—Mithali 15:22.

Usisikilize Porojo Zenye Kudhuru: Ni nini kingepata ile ‘midomo mikubwa,’ kama hakungekuwako yale ‘masikio makubwa’? Wale ambao hujiingiza wakati wote katika mazungumzo ya kipumbavu huwa sehemu tu ya tatizo lenyewe; wale wanaofurahia kusikiliza wanalaumika pia. Kusikiliza tu kwaweza kuonyesha kibali chako cha kimya na kuchochee kusambazwa kwa porojo zenye kudhuru. Mithali 17:4 husema: “Mtenda mabaya husikiliza midomo ya uovu; na mwongo hutega sikio lake kusikiliza ulimi wa madhara.”

Kwa hiyo wakati mazungumzo kuhusu mtu mwingine yavukapo mpaka, huenda ukahitaji kuonyesha ujasiri na kusema, ‘Acheni tuzungumzie jambo jingine.’ Na ikiwa mzingo wa marafiki wako wathibitika kuwa usiokoma kushughulika na porojo zenye kudhuru, huenda hata ukahitaji kufikiria kutafuta washirika wapya. Biblia husema: “Mpiga porojo hawezi kamwe kuweka siri. Kaa mbali na watu wanaosema sana.” (Mithali 20:19, Today’s English Version) Mara nyingi, ni baada ya muda mfupi tu kabla wewe hujawa jambo kuu la mazungumzo.

Usiwe na Mwitikio-tendo Unaopita Kiasi Upokeapo Porojo: Watu wengi hufurahia porojo mradi hizo haziwahusu wao wenyewe. Kwa upande ule mwingine, tuseme kwamba wewe ndiye umeathiriwa na porojo mbaya au hadithi za uwongo. Nyakati nyingine inawezekana kufuatilia chanzo cha hadithi hiyo na kunyosha mambo kwa utulivu. Lakini namna gani ikiwa huwezi?

Kukasirika kwako hakutimizi lolote. Kwa kweli, “Yeye aonaye hasira upesi atatenda kwa ujinga,” Biblia husema. (Mithali 14:17) Hivyo, Sulemani hutoa shauri hili: “Usitie moyoni mwako maneno yote yaliyosemwa . . . Kwa kuwa mara nyingi moyo wako pia unajua ya kwamba wewe mwenyewe umewatukana watu wengine.” (Mhubiri 7:21, 22) Porojo ni jambo hakika la maisha, na wakati mmoja au mwingine, labda wewe mwenyewe umeshiriki sana katika kupiga porojo. Je! jambo hilo lastahili kweli kukuudhi? Je! linaelekea kuwa litafifia na kwisha baada ya kipindi fulani? Kuna “wakati wa kucheka,” na labda ili kuonyesha kwamba wewe ni mfurahifu, kutolichukua jambo hilo kwa uzito na hata kucheka ndiyo njia bora zaidi ya kukomesha uvumi huo.—Mhubiri 3:4.

Usiongeze Kuni Kwenye Moto: Ikiwa hadithi hiyo haikomi kabisa, jiulize: ‘Je! yaweza kuwa kwamba mimi mwenyewe ndiye ninayewapa wengine sababu ya kupiga porojo? Je! labda mimi ninatenda katika njia ambayo inazusha shaka, nikifanya nionekane kama ninatenda kosa?’ Fikiria hali mbalimbali zifuatazo:

◻ Wafanyakazi wenzi wa mwanamke mmoja humwita mzembe na asiyetegemeka bila yeye kujua—hata ingawa yeye hutimiza kazi yake kwa utimilifu. Kwa nini basi sifa hiyo mbaya? Jambo moja ni kwamba, yeye huonyesha mwelekeo wa kutojali na wa uzembe, ambao waweza kufasiriwa vibaya kuwa uvivu. Mavazi yake ni ya vivi hivi na hayafai kazi anayofanya. Hatimaye, yeye haonyeshi busara anaposhugulikia simu za kibinafsi, akiongea kwa sauti ya juu sana kuweza kuvuta uangalifu wa wafanyakazi wote ofisini. Ndiyo maana kuna porojo hizo!

◻ Mwanamume mwuuzaji katika duka fulani ndiye anayezungumzwa na kila mtu katika jumuia yake ndogo. Watu hupiga porojo kwamba yeye si mwaminifu kwa mke wake. Mwanamume huyo hukataa katakata hoja hizo zisizo za kweli. Ni nini sababu yenyewe ya uvumi huo? Ni sifa yake ya kuzoeleana isivyofaa na wateja wanawake.

◻ Msichana mmoja tineja anasemwa kuwa ni mwenye kukosa adili. Wengine hudai kuwa yeye ana wapenzi kadhaa na kwamba yeye hutumia kokeni. Hadithi hizo zote ni za uongo. Lakini anajulikana kwa kushirikiana na watu wanaoshughulika na dawa za kulevya. Yeye hupita kiasi katika mavazi yake, mtindo wake wa nywele, na rangi zake za uso.

Basi ikiwa watu wanapiga porojo juu yako, inaweza kuwa msaada kuchunguza kama tabia yako, jinsi unavyoshughulika na wengine, hata mavazi na mapambo yako, yanaongeza kuni kwenye moto kwa njia fulani. Labda mabadiliko fulani katika mtindo-maisha wako yaweza kukomesha uvumi huo. “Moto hufa kwa kukosa kuni,” yasema Biblia. (Mithali 26:20) Isitoshe, ikiwa matendo yako yanakaribia kuwa ya kukosa adabu, sikuzote kuna hatari halisi ya kuteleza na kufanya mabaya—kukifanya kile kilichokuwa mwanzoni uvumi kuwa jambo halisi.—Linganisha Wagalatia 6:7, 8; 1 Wakorintho 10:12.

‘Shughulikia Mambo Yako Mwenyewe’

Porojo haziwezi kuisha. Hata hivyo, ni lazima zitambuliwe kwa sababu ya uwezo wazo wa kuharibu. Unaweza kuepuka na hata uepushe wengine maumivu ya moyoni na majonzi mengi kwa kufuata tu maneno haya ya hekima: “Mambo yo yote yaliyo ya kweli, yo yote yaliyo ya staha, yo yote yaliyo ya haki, yo yote yaliyo safi, yo yote yenye kupendeza, yo yote yenye sifa njema, ukiwapo wema wo wote, ikiwapo sifa nzuri yo yote, yatafakarini hayo . . , na Mungu wa amani atakuwa pamoja nanyi.”—Wafilipi 4:8, 9.

Naam, Mungu mwenyewe anapendezwa na jinsi tunenavyo juu ya wengine. Yesu Kristo alionya: “Kila neno lisilo maana, watakalolinena wanadamu, watatoa hesabu ya neno hilo siku ya hukumu. Kwa kuwa kwa maneno yako utahesabiwa haki, na kwa maneno yako utahukumiwa.”—Mathayo 12:36, 37; linganisha Zaburi 52:2-5.

Je! wataka kuwa na uhusiano mwema pamoja na wengine, kuwa na amani ya akili, na, la maana hata zaidi, kuwa na msimamo mzuri pamoja na Mungu? Basi fuata shauri la Neno la Mungu lililopuliziwa: “Muwe na nia ya kuishi maisha ya utulivu, kila mmoja ashughulikie mambo yake mwenyewe.” (1 Wathesalonike 4:11, Habari Njema kwa Watu Wote) Pendezwa na watu wengine, lakini ufanye hivyo katika njia yenye fadhili na staha. Hivyo utaepuka kabisa porojo zenye nia ya kuumiza, zenye kudhuru.

[Maelezo ya Chini]

a Kwa habari zaidi, ona kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc., sura 19.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Ondoka mahali penye mazungumzo yenye kudhuru

[Picha katika ukurasa wa 10]

Je! mwenendo wako usio wa busara wafanya watu wapige porojo juu yako?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki