Kwa Nini Ubadili Jinsi Ulivyo?
NI WACHACHE kati yetu ambao hupenda kukubali kwamba tuna udhaifu mbalimbali ulio dhahiri. Ni ya kweli jinsi gani mistari ya mshairi Mskoti Robert Burns: “Laiti uwezo fulani ungetupatia kipawa cha kujiona kama vile wengine watuonavyo sisi”! Ndiyo, sisi huona ni rahisi kupata makosa kwa wengine na huenda tukawa wepesi kuwatolea ushauri kuwaonyesha jinsi ya kufanya maendeleo. Lakini dokezo lolote la kwamba sisi tunahitaji kubadilisha tabia yetu huenda likatukasirisha. Je! lingekukasirisha wewe?
Acha tusimamie hapa kwa muda mfupi na tuwazie ulimwengu mkamilifu ambamo kila mtu ni safi, mwenye afya, furaha na mnyofu; ambamo hata wenye mamlaka ni wenye fadhili na ufikirio, wakipendezwa na kufanyia wengine mazuri; ambamo hamna pupa, na hamna anayetumia mwenzake kujifaidi; ambamo watoto ni watiifu kwa wazazi wao wenye uchangamfu na upendo; ambamo hamna hasira za kufoka—hamna jeuri, hamna uhalifu, hamna ukosefu wa adili; ambamo watu ni watumainifu na wenye kupendeza kwa asili; ambamo maisha yaweza kuonewa shangwe usalama na usitawi.
Je! waweza kujiona ukifaa kuwa katika ulimwengu kama huo, ikiwa ulimwengu huo wa kuwaziwa ungekuwapo? Naam, habari njema kutoka kwenye Biblia ni kwamba ulimwengu huo utakuja kwenye dunia hii karibuni. Kwa hivyo sasa swali la maana ni: Je! wewe una vitabia ambavyo vitakukosesha ustahili kuingia katika jamii hiyo yenye kupendeza? Unafikiri, ingekuwa vigumu jinsi gani kujitahidi kustahili uhai katika paradiso hiyo?—Isaya 65:17-25; 2 Petro 3:13.
Hata sasa, kabla ya dunia hiyo mpya kuja, je! maisha yako yangeweza kufanyiwa maendeleo ikiwa ungefanya jambo fulani kuhusu tabia na hali yako? Ikiwa ndivyo, kwa nini usibadili jinsi ulivyo? Inawezekana kufanya hivyo. Kumbuka kwamba, mavutano fulani yaliunda na kufinyanga tabia yako pale mwanzoni, kwa hivyo kwa kujidhibiti zaidi na kuonyesha upendezi, inawezekana kwako kufanyiza upya tabia yako hata sasa.
Hata hivyo, huenda bado ukapinga: ‘Lakini kweli naweza kubadilika? Nimejaribu hapo kwanza, mara nyingi, nikashindwa. Mimi niko vile tu nilivyo, na hakuna ninaloweza kufanya!’
Fikiria Paulo, mtume wa Yesu Kristo. (Warumi 7:18-21) Paulo alibadilika akaacha kuwa mpinzani wa Wakristo na mwenye jeuri na mwenye kujiona binafsi kuwa mwadilifu, akawa Mkristo yeye mwenyewe. Alibadilika kwa sababu alitaka kikweli. Hakulegea kwa sababu ya vipingamizi au mavutano ya urithi. Hakuamini kwamba utu wake wa zamani ulikuwa umekolea sana usiweze kubadilika. Ilihitaji jitihada nyingi kwa upande wake. Lakini alipata msaada mwingi.—Wagalatia 1:13-16.
Msaada huo ulitoka wapi?